fasihi simulizi na utamaduni wa jamii zinavyohusiana

 

 ELEZA UHUSIANO KATI YA FASIHI SIMULIZI  NA UTAMADUNI WA  JAMII.

Fasihi simulizi ni sanaa inayotumia lugha ya mazungumzo ya ana kwa ana katika kufikisha ujumbe uliokusudiwa kwa hadhira husika. Hii ni sanaa ambayo ujumbe wake upo katika mfumo mzima wa pande mbili za mawasiliano kuwepo pamoja ana kwa ana hii ikimaanisha fanani yaani mtu anayerithisha (msimuliaji) na Hadhira yaani mtu anayerithishwa (msimuliwaji). Kwa njia hii fasihi simulizi hushirikisha au huwafikia watu wengi na mawazo ambayo jamii iliyakubali, imeyakubali, inaendelea kuyakubali yatokeapo na inayapitisha na au kuyakabidhi kwa kuendelezwa kutoka kizazi kimoja hadi kizazi kingine kwa njia ya mdomo.

Utamaduni ni jinsi binadamu anavyokabili maisha katika mazingira yake.Hiyo inajumlisha ujuziimanisanaamaadilisheriadesturi n.k. ambavyo mtu anajipatia kama  mwanajamii.

Kama sifa  maalumu ya binadamu, inayomtofautisha na wanyama, utamaduni ni suala la  msingi katika anthropolojia, ukihusisha yale yote yanayopokezwa katika jamii fulani, kama vile lugha inayounganisha watu wanaohusika  nao ,fasihi, mafungamano, ndoa,michezo,ibada, sayansi na teknolojia.

Utamaduni ulioendelea unaitwa pia "ustaarabu". Kila utamaduni unabadilikabadilika mfululizo: ndani ya watu husika, baadhi wanachangia na

kuunga mkono mabadiliko, wakati wengine wanayakataa. Ujuzi mpya na teknolojia, pamoja na mahitaji  ya uchumi, ni kati ya mambo yanayosukuma zaidi kubadili kiasi fulani utamaduni.

Hakuna  jamii  isiyokuwa  na  fasihi simulizi ,  kwa  sababu  iliibuka  pale  jamii  zilipoanza  kutumia  lugha  kama  chombo  cha  mawasiliano.  Kwa  muda  mrefu,  fasihi kwa ujumla  imechukuliwa  kwamba  jukumu  lake  ni  kuburudisha  na  kustarehesha. Majukumu  haya  mawili  yanatokana  na  maumbile  ya  sanaa  hii. Fasihi simulizi  imetumiwa  kuamsha  hisia  za  burudani  na  kustarehesha  kwa  matumizi  ya  simulizi,  nyimbo,  ngano,  vitendawili  na  maigizo. Lakini  tutazamapo  fasihi simulizi   yoyote  ile,  tunaona  kwamba  haikosi  kufundisha  jambo,  au  kimakusudi  ama  kisadfa.

 

Fasihi  simulizi  ni  sanaa  inayotuchorea  taswira  ya  uhalisi  wa  maisha   ya  binadamu,  hivyo  inawasilisha  hali,  maingiliano,  mivutano  na  mikinzano  miongoni  mwa  binadamu  na  mazingira  yake.  Msikilizaji   wa  kazi  ya  fasihi  huingiliana  na  tajriba  za  hali  inayowasilishwa  na  wahusika  wa  kazi  hiyo  kama  walivyosawiriwa. 

Vilevile, hukata  kauli  kuhusu  ukweli;  uhalisi;  na  ubora  wa  yale  anayokumbana  nayo. Waandishi  wengi  hujaribu  kusimulia  maisha  katika  mapana  na  marefu  yake  na  kwa  lugha  teule,  ili  kugusa  hisia  za  msomaji  au  msikilizaji.


Fasili nyingi za fasihi zimeegemea kuileza katika uhusiano wa fasihi simulizi na jamii. Fasili hizi zimeonyesha kwamba fasihi simulizi  ni taasisi ya jamii na uhusiano wake na jamii hauwezi kupuuzwa. Mmoja wa wanaounga mkono dhana hii ni Escarpit, R (1974:4) anayesema kwamba: Fasihi hasa simulizi lazima ichukuliwe kama iliyo na uhusiano usiotatanika na maisha ya kijamii. 

Kutokana na maelezo haya tunaweza kuona wazi kuwa fasihi simulizi katika swala zima la jamii ni kwamba imekuwa kielelezo mwafaka cha kuona kwamba jamii inakuwa na kuchongeka ifaavyo. Ni ukweli usiopingika kuwa fasihi simulizi ni kioo cha jamii.Hija hii inapigiwa upato tunaposhuhudia namna tamaduni, mila, miiko na hali halisi ya maisha katika jamii zetu inavyopitishwa kutokakizazi kimoja hadi kingine.

 

Hili linajitokeza katika tanzu mbalimbali za fasihi simulizi zikiwemo methali, nahau,misemo, mafumbo na kadhalika. kwa mfano methali zipo zile zenye chuku ambazo hutumiwa sio tu kupamba lugha ambayo ni sehemu ya  utamaduni wa jamii bali pia hutumiwa kuonyesha utabaka wa wanajamii pamoja na shughuli ambazo wana-jamii wanazozifanya.

 

Kulingana na Wamitila K.W (2000) anaeleza kuwa chuku ni udanganyifu   au  maneno  yasiyo  ya  kweli.   Msemo   'kupiga  chuku’  unaelezewa   kuwa  hali  ya  kuongezea,  kuzidisha  au  kuitia chumvi  habari   fulani.  Katika  chuku,   huwa  kuna  ukweli  fulani  unaotakiwa   kuwasilishwa   ila  umejificha  ndani  kwa  ndani  kwa  kutiliwa  chumvi  mno.   Mathalani,  watu  wahudhuriapo  mkutano  fulani , hali  hiyo  inaweza  kupigwa  chuku  kwa  kusemwa  hivi:  'Watu  walijaa  hivi  kwamba  hapakuwa  na  nafasi  ya  kutema  mate  au  nzi  kupita.’  

 

Ukweli  katika  kauli  hii  ni  kuwa   mkutano  unaozungumziwa   ulihudhuriwa  na  watu  wengi   lakini  haiwezekani  wingi  huo  kuikosesha  hadhira  nafasi  ya  kutema  mate  au  nzi  nafasi  ya  kupita.  Chuku imetumiwa hapa  kushadidia  wingi wa  wahudhuriaji.

 

Utakuta kwamba methali zilizo na chuku na vitanza ndimi kwa upande wake zimetumiwa sana katika jamii.  Vitanza  ndimi  ni  mbinu  ambayo   hujitokeza  sana  katika mashairi   na  methali  za  jadi.   Jamii  nyingi  za  Kiafrika zilikuwa  na  mazoea  ya  kuchezea  maneno  katika hali ya kujiburudisha. 

 

Tukitazama kwenye methali zilizona chuku na vitanza ndimi, tunapata kuwa haliya maisha hasa utabaka hujitokeza wazi kabisa.Chuku na  vitanza  ndimi  vilitumiwa  katika  methali  zilizoonyesha  na zinazoonyesha  utabaka  miongoni  mwa  wanajamii mbalimbali,  zilizozisuta  tabia  fulani  kama  vile  kiburi  na  tadi,  zilizoonyesha na zinazoonyesha   ushirika   katika  kazi  miongoni  mwa  nyingine. 

 

Mbinu  hizi   zilizifanya  methali  hizo  kuwa  na  urefu  usiokuwa  wa kawaida   japo  zimeendelezwa kwa kifupi katika kamusi  za  methali . Mfano : Kuku  wa  mkata   hatagi   na  akitaga  haangui  na  akiangua  vifaranga  huchukuliwa  na  mwewe.  Watu  wengine  huisema  methali  hii  hivi:  Kuku  wa  mkata,  kata na  akita  haangui  na  akiangua, vifaranga  huchukuliwa  na  mwewe. 

Vitanza  ndimi(ambavyo ni sehemu ya mojawapowa vipera vya fasihi simulizi)   katika  methali   hii   ni  mkata, kata, akita ,  taga  angua na vifaranga.  Jamii  nyingi  za  Kiafrika  ziliuchukulia  umaskini    kama  hali  ya  majaliwa.   Ulimnyima  mwanajamii  uwezo  wa  kushiriki  katika  shughuli  za  kiuchumi  katika  jamii  yake.  Ilisadikika   kuwa   maskini  asingeweza  kufanikiwa  kwa  vyovyote  vile  na  katika  lolote   alilokusudia  kulifanya  licha  ya  kutia  juhudi.  

 

Kutokuwa na  uwezo  wa  mtu  maskini  kumepigwa  chuku   sana   katika  methali  hii.  Hali  hii  pengine   ndiyo  inayotudokezea  kwa  nini  pengo  kati  ya  walalahoi   na   walalaheri   liliendelea   kupanuka  kila  uchao  katika  jamii  kwa  ile  kasumba   iliyoyatawala   mawazo  ya  Mwafrika  kuwa  umaskini  wake  ulikuwa  kudura  kutoka  kwa  Maulana.   

 

Chuku  katika  methali  hii   inatekeleza  dhima  ya  kutudhihirishia   kuwa  ni  muhali   sana  kwa  mtu  maskini  kuweza  kufanikiwa  maishani   kwa  sababu   ya  hali   tofauti  zinazomzunguka   kama  vile uwezo  wake  mdogo,  ukosefu  wa  raslimali  muhimu  ,   kudhulumiwa   na  mwenye  nguvu  ambaye  hapa  analinganishwa  na   mwewe  na  kasumba  yake  mwenyewe.

 

Kupitia kwenye mifano hii, ni wazi kuwa jamii husika inaweza kupitisha na kirithisha amali zake mbalimbali kwenye kizazi kipya.

Urathi huu ni nguzo muhimu sana katika kuhakikisha kuwa jamii inazidi kuwa na mwelekeo ufaao wa kimaisha.

Vile vile fasihi simulizi tangu awali hadi sasa imekuwa mbinu bora zaidi ya kuwafundisha wanajamii.Tukitazama hapo awali, tanzu mbalimbali za fasihi simulizi zilikuwa zikitolewa kulingana na muktadha wa tukio husika. Kwa mfano nyimbo ziliimbwa kulingana na matukio husika. Baadhi ya matukio yaliyoangaziwa  katika Nyimbo ni kama  zile Nyimbo za tohara(nyiso) katika jamii ya Wabukusu.

Nyimbo hizi zilifunzwa na wakongwe hasa  nyakanga au kungwi  katika swala zima la kuwaandaa vijana wa kiume katika mpango mzima wa kuwadariji kutoka utotoni hadi ukubwani. Zilikuwa na maudhui ya kuwafanya kuwa na ujasiri wa kukutana na kisu cha ngariba pamoja na Kuwapa kitambulisho cha kuwa wana-jamii waliokamilika. Wale walioonekana kuwa waoga vile vile waliimbiwa zaoza kuwakejeli kadamnasi ya jamii. Kwa kufanya hivyo jamii husika iliweza kuwarithisha wanajamii tamaduni na mila zao katika shughuli kama hizo.

Fasihi simulizi vile vile imekuwa katika mstari katika kuielekeza jamii huku  ikiimarisha wajibu wa wanajamii mbalimbali.Kupitia tanzu mbalimbali za fasihi simulizi,  jamii imewezakuelewa wajibu wao kikamilifu. Hililimewekawaziwajibu wakila mmoja katika jamii awe mtoto wa kike,kiume, mzazi wa kiemeau kike n.k.

 

Vijana Wavulana walipewa mafunzo bora ya kuwawezesha kuwa mstari wa mbele katika Kuhakikisha kuwa majukumu yote ya kiume yanatiliwa mkazo kabisa. Hii ilikuwa pamoja na kuilinda jamii kutokana na mashambilizi ya kila aina,

 

Fasihi simulizi vile vile ni hazina kubwa ya kuhifadhi historia ya jamii.Hii inajitokeza katika masimulizi ya majagina kama Fumo Lyongo, Luanda Magere na kadhalika. Kupitia kwa masimulizi haya jamii inajitambua vyema kule ilikotoka, namna ilivyokuwa na kule  inakodhamiria kuenda katika siku zake za halafu.   

Methali ni miongoni mwa kauli teule zinazotumiwa katika mawasiliano ya jamii. Kila jamii huwa na methali zake. Kwa sababu, methali zimefundika hekima na hutumiwa katika kuelimisha, kubainisha na kuhifadhi falsafa ya watu katika muktadha wa utamaduni. Vile vile, methali zinapotumiwa huufanya ujumbe unaowasilishwa kuwa bayana, kueleweka na kuweza kufafanuliwa kwa kuzingatia uhalisi wa maisha. Kwa kuzingatia hayo, ujumbe katika methali hupata ufasiri usiokuwa na utata.

Kimsingi methali ni zao la utamaduni na hazijafungika katika ufinyu wa mawasiliano ya jamii (Parker, 1972). Kwa hivyo, methali huweza kupatanishwa na takribani kila kipengele katika maisha ya watu. Kutokana na umaarufu wake katika mawasiliano ya watu, zimekuwa zikirithishwa na kutumiwa kimapokeo kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Kadhalika, methali hujibainisha zaidi katika tamathali za usemi ambapo huwa ni kauli za kimafumbo zitumikazo katika kufafanua maswala ya uadilishaji na uielekezaji wa wanajamii kuhusu maisha.

Ni katika muktadha huu ambapo hadhira huhitaji kupiga bongo ili kuweza kuupata uzami wa ujumbe unaowasilishwa. Kulingana na Wamitila (2000) na Wafula (1994), methali ni kauli zilizokubalika katika utamaduni wajamii. Isitoshe, methali ni kauli ambazo zimejengeka katika miundo mahususi inayotambuliwa na kukumbukwa kwa urahisi. Kwa hivyo, hutumiwa kwa malengo ya kuwaelekeza, kuwasuta, kuwakejeli na kuwashauri watu.

Endapo maswala yanayoshughulikiwa yanagusia hisi; ujumbe huo huwasilishwa kiistiari, kitashihisi, kitashibihi, kijazanda na kitaswira ili kuepukana na kutonesha hisi za wale wanaohusika.

Kimapokeo, methali zimekuwa zikitumika katika mawasiliano ya kila siku kutokana na tajiriba inayotokana na utamaduni na uhalisi wa maisha. Kwa hivyo, ni kauli zinazoweza kutumiwa katika mawasiliano ili kupatanisha ujumbe unaoibuliwa na yale yaliyopo katika jamii. Tangu jadi, tamaduni za kilimwengu zimekuwa zikitilia mkazo maswala ya umoja na utangamano.

Hayo ni baadhi ya mambo ya msingi ambayo yamekuwa yakipewa kipaumbele siyo tu katika jamii hizo za awali bali pia katika jamii za sasa. Wanajamii wamekuwa wakiunda kauli mbalimbali katika uwasilishaji wa swala hilo. Isitoshe, methali zinapotumika kwa mwafaka huusisitiza zaidi ujumbe unaowasilishwa. Kadhalika, methali hutumika katika kutekeleza mambo mawili: kubainisha na kuwaelekeza watu.

Matarajio ni kwamba, watu waweze kuzingatia busara inayoibuliwa na zaidi kuchukua hatua inazostahili ili kujenga mahusiano ya ushirika, upendo na amani kama ilivyodhinishwa katika utamaduni wao. Katika muktadha migogoro na migaragazo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi ambayo imekuwa ikishuhudiwa kila kuchao katika jamii imejengewa muktadha wa kurejelea katika methali zilizopo.

Methali vile vile hutumiwa katika sala zima la kudhihirisha amali za kijamii . Mfano ni methali isemayo  ,  'Kinyozi   hajinyoi  na   akijinyoa   hajitakati  na  akijitakata  hujikata’.   Kihunzi katika  methali   hii  kimeegemezwa  katika   maneno  kujitakata  na  kujikata.  Methali   yenyewe  inatilia  chumvi   hali   ya   kinyozi   mzoefu  wa  kuwanyoa  wengine  kukosa  uwezo  wa  kujinyoa. 

Pale  ambapo  kinyozi   mwenyewe  atajibidiisha  kujinyoa  huenda   asifikie  usafi  unaohitajika  na  iwapo  usafi  huo   utafikiwa,  basi   kinyozi  huyo  atajikata.   Dhima  ya  chuku  katika  methali   yenyewe  ni   kutudhihirishia  kwamba  hapana   mtu  hata  mmoja  ambaye  anaweza  kujidai  kuwa  mjuzi  wa  kila  jambo  kwani  uwezo  wa  binadamu  una  kikomo.  

 

Lengo kuu la matumizi  ya  chuku na  vitanza  ndimi  katika  methali  za  Kiswahili  lilikuwa  ni  kuburudisha  ,  kufurahisha  na kuteka  nadhari  ya  hadhira  ili  iweze  kupata  ujumbe   uliojitokeza  katika  methali  zenyewe.   Mbinu  hizo  aidha  'ziliutohoa’  na  kuuficha  ukali  ambao   iwapo  ungesemwa   bayana,   ungeibua   hisia   kali.

Kwa yakini na si yamkini fasihi  simulizi ni taasisi ya kijamii, inayotumia lugha kama mtambo wake. Isitoshe, fasihi simulizi  huwakilisha maisha. Maisha kwa upana wake huhusu uhalisi wa kijamii, hata ingawa ulimwengu halisi na hata ulimwengu wa ndani wa mtu binafsi ni mambo yanayoweza kuzingatiwa katika fasihi. Mbali na hayo twafahamu kwamba iwapo fasihi simulizi hulenga watu fulani, basi bila shaka hiyo fasihi yahusu jamii fulani lau sivyo hapana haja kutungia watu kazi isiyowahusu ndewe wala sikio. 

 

Jambo jingine la kutaja hapa ni kwamba mtunzi mwenyewe wakazi ya fasihi simulizi ima yawe mafumbo, ngano, nyimbo n,k ni mwanajamii kwa ambavyo ana nafasi na tabaka fulani katika jamii yake; yeye hutambuliwa na jamii kama mmoja wao. Hawezi kuepuka nafasi hiyo yake katika jamii wala hawezi kukwepa athari ya jumuiya katika utunzi wake kwani kama mtoto mchanga yeye anafundishwa maadili na itikadi za jamii yake ili kuweza kuenea katika jamii hiyo. Na kama ambavyo tumetaja tayari, mtunzi hulenga hadhira fulani hata iwe ndogo vipi. 

Mara nyingi fasihi hutokana na uhusiano wa karibu sana na taasisi maalum za kijamii. Taasisi za kiuchumi, kisiasa, na kijamii zimekuwa na uhusiano mkubwa sana na utoaji wa fasihi na kila kazi ya fasihi kwa njia moja au nyengine, hudhihiri ukweli huu. Maendeleo na mabadiliko ya jamii yametokea kuwa maendeleo na mabadiliko ya fasihi hivi kwamba hatuwezi kutenganisha fasihi na jamii inamoibukia. Uhusiano huu unatokea kwa sababu pindi maisha ya jamii yabadilikapo, mielekeo, tamaduni na hata maadhili ya jamii hubadilika pia. Aidha, mabadiliko ya fasihi toka simulizi hadi andishi ni zao la mabadiliko katika maisha ya jamii ambapo taaluma ya kusoma na kuandika ilitokea. Kwa hivyo fasihi inalo jukumu kuu katika jamii ambalo sio la kibinafsi, bali ni la kijamii. Katika kuiunga mkono kauli hii, Wellek na Werren (1949:95) wanasema kwamba: Uhusiano kati ya fasihi ima iwe Andishi au simulizi  na jamii hujadiliwa kwa kuanza na kauli aliyoitoa De Bonald kwamba `fasihi ni kielelezo cha jamii'. 

Kwa hivyo ni muhimu kuichukulia fasihi kama zao la jamii ambalo pia huathiri na kuathiriwa na jamii.  Hata katika nyingi za tahakiki za fasihi ambazo twaweza kuziita za kijamii (kama za Ki-marx) pamesisitizwa kauli kwamba mtunzi anapaswa kuendeleza maisha ya wakati wake kwa ujumla wake; kwamba anapaswa kuwa kiwakilishi cha wakati wake na jamii yake. Kwa maoni ya waitifaki wa tahakiki hizi, `uwakilishi' huelekea kumaanisha kuwa mtunzi anapaswa kutambua na kuona hali halisi za maisha katika jamii yake na kuzizingatia katika utunzi wake. Maoni ya Hegel na Taine katika Wellek na Warren (1949:95) ni mfano unaochangia zaidi kauli hii wanaposema: 

Katika uhakiki wa Kihegel na hata ule wa Taine, utukufu wa kijamii na wa kihistoria huenda sambamba na utukufu wa kisanaa. Msanii huendeleza ukweli, na

huo ukweli ni wa kijamii na kihistoria. Tunaloweza kuongeza ni kwamba pana tatizo linalokumba juhudi yoyote ya  kujaribu kutenganisha fasihi na jamii kwani fasihi huathiriwa na mandhari ya  kijamii pamoja na mabadiliko na maendeleo yake. Isitoshe, mtunzi ni mwanajamii anayetumia lugha ya jamii kutunga kazi yake ili kuwafifikia wanajamii husika. Ukweli huu wanaogusia waandishi hawa utategemea mtizamo, matarajio, na tajiriba za anayehusika kwani hali mbali mbali

katika jamii hutoa maana mbali mbali kwa watu mbali mbali hata kama ni wa

jamii moja. Hivyo basi ukweli hubainika tu kimuktadha. 

 

Wale wanaosisitiza kigezo cha fasihi na jamii katika kuieleza fasihi, wametoa kauli kwamba pana aina mbali mbali za fasihi ambazo zinachukuana na jamii mbalimbali. Dhana kama vile fasihi ya kirusi, fasihi ya kiafrika, fasihi ya kiingereza n.k. ni baadhi ya mifano ya kazi za fasihi zinazohusishwa na jamii fulani. Fasihi kama hizi hulenga jamii fulani pana zenye kaida na maadili yanayopatana katika muundo wa kijumla kwani katika jamii hizo huwa kuna vijamii vidogo vidogo. Kwa mfano katika fasihi ya Kiafrika pana fasihi ya jamii ya nchi mbali mbali ambazo zimeibuka kihistoria kwa jinsi maalum ambao ni tofauti na ya nchi nyengineyo.

Na katika nchi hizo pana vijamii vingine vidogo vidogo vinavyobainishwa na lugha, mazingira, na itikadi. Hivyo kutaja kwamba pana fasihi ya kirusi ni kutoa kauli ya kijumla tu. Vile vile pana fasihi zinazochukuana na mifumo mbali mbali ya maendeleo ya kijamii kama vile fasihi ya kibwanyenye, fasihi ya kisosholisti, fasihi ya kikapitolisti n.k. 

Ama kwa hakika mojawapo ya majukumu ya fasihi ni kule kuihifadhi historia ya jamii husika. Yaani kwa kuitazama kazi ya fasihi twaweza kupata picha maalum ya historia ya jamii husika. Kwa mfano katika fasihi ya kiswahili twaweza kupata vipindi maalum vya kihistoria, Mashetani (Ebrahim Hussein) ni mfano wa Kipindi cha Ukoloni-Mamboleo, na utenzi wa Al-Inkishafi (Sayyid Nassir) ni kielelezo cha historia ya Mji wa Pate. Hivyo basi twaona kwamba kauli kuwa fasihi ina uhusiano mkubwa na jamii ni dhana yenye mashiko sana. 


Hata hivyo hatulengi kusema kwamba kazi ya fasihi ni hitoria kwa kule kuhitajika kutoa picha halisi ya maisha ya wakati husika, kwani japo mada ni matukio halisi ya kihistoria, namna ya kusawiri mada hizo na matini maalum (kati ya mengi) yaliyozingatiwa, ndiyo yaibainisha kama kazi ya fasihi. Maoni yaliyotolewa hapa ni mwongozo wa kuitazama fasihi katika vigezo ambavyo bila shaka huathiri fasihi.

Iwapo tutakubali kwamba kazi ya fasihi simulizi  si amali ya mtu binafsi, basi tutakuwa tayari tumeonyesha kwamba fasihi na jamii ni vitu visivyotengana. Na hata pakitokea kwamba maisha ya mtu binafsi yametumiwa kama nguzo ya kutunga kazi ya fasihi, hatuwezi kusahau kwamba tajiriba zake zimepaliliwa na maisha yake kama mwanajamii, awe anachukua au kukiuka maadili na matarajio ya jamii hiyo. 

Hitimisho.

Kutokana na ufafanuzi huu, tunaweza kusema kuwa fasihi simulizi ina uhusiano mkubwa na utamaduni. Maana kati ya vipengele vya utamaduni kimoja ni lugha. Lugha kama sehemu ya utamaduni ina tabia ya kuwapambanua watu. Japo siku hizi kuna jitihada ya watu kujifunza lugha mbali mbali, lakini lugha ya kujifunza haiwi yako, na mara nyingi wenyeji wa lugha hiyo uliyojifunza huweza kujua kuwa wewe si mmoja wao.

Kwa kuwa lugha ni kipengele kimojawapo cha utamaduni, na kwa kuwa fasihi hutumia lugha, basi fasihi na ni sehemu ya utamaduni. Na iwapo utamaduni ni utashi na uhai wa taifa, ni mti wa mgongo wa taifa, basi hapana budi fasihi nayo kuwa sehemu ya uhai na utashi wa jamii hiyo.Fasihi (na maelezo haya yaweza kuingia katika fasihi kwa jumla, fasihi maandishi na fasihi simulizi) si sehemu tu ya utamaduni, bali ni chombo cha utamaduni pia. Ndiyo chombo cha kukuzia, kuhifadhia, kuendelezea na kuelezea huo utamaduni. Ni chombo cha pekee kati ya taaluma mbali mbali za utamaduni. Hutokea hivyo kwa kuwa taaluma hii huhusika na jinsi lugha inavyosema na jambo linalosemwa. Kwa hivyo hutoa tafsiri mbali mbali ambazo pengine taaluma zingine hushindwa kuzitoa.

 

 

 

Marejeleo

o   Kirumbi, P. S. 1975. Misingi ya Fasihi Simulizi. Nairobi: Shungwaya Publishers.

o   Matteru, M. D. 1983. Fasihi Simulizi na Uandishi wa Kiswahili, katika Fasihi: Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI. Uk. 26 – 37.

o   Mlacha, S. A. K. 1995. Fasihi Simulizi na Usuli wa Historia ya Pemba. Katika: Lugha, Utamaduni na Fasihi Simulizi ya Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI/ITAA. Uk. 16-26.

o   Msokile, M. 1992. Kunga za Fasihi na Lugha. Kibaha: EPD.

o   Wamitila K. W. 2003. Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi, Kenya: Focus Publications. Wamitila, K. W. 2003. Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Fasihi. Nairobi, Kenya: Focus Publications.

o   Gazeti la Mtanzania la tarehe 13.06.03.

o   Kimani N. 2006. Fasihi Simulizi na Nadharia ya Fasihi ya Kiafrika, katika Fasihi ya Kiswahili. Nairobi: Twaweza Communications. Uk. 1 – 10.

o   Senkoro, Fikeni (2004b). “The role of language in education and poverty alleviation: Tool for access and empowerment” in Justian Galabawa and 20 Anders Narman Education Poverty and Inequality (eds), DSM: KAD Associates. (pp 46-58).

o   Mulokozi, M. M. (1989). Tanzu za Fasihi Simulizi: Katika Mulika 21. TUKI. Dar es Salaam.

o   Mulokozi, M.M. (1996). Utangulizi wa Fasihi Simulizi ya Kiswahili. TUKI. Dar es Salaam.

o   Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Focus Publications Ltd.Nairobi.

o   TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. (Toleo la Pili). East Africa: Oxford University Press na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI).

 

 

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

HIZI HAPA SMS TAMU ZA KUMTAKIA USIKU MWEMA MPENZI WAKO

SMS na MESEJI 900+ za mapenzi

MIAKA 22 SASA TANGU KUZAMA KWA MELI KUBWA YA MV BUKOBA, TANZANI TUMEJIFUNZA NINI?