SURA YA KWANZA

UANDISHI

1.0 Uandishi maana yake nini?

Uandishi ni uwakilishaji wa lugha kwa njia ya

maandishi kwa kutumia ishara na alama - yaani

mfumo wa uandishi wa lugha husika. Lugha kwa

mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu ni “mpangilio

wa sauti na maneno unaoleta maana ambao

hutumiwa na watu wa taifa au kundi fulani kwa ajili

ya kuwasiliana” (KKS: 201). Tafsiri ya lugha na ile

ya uandishi zikiwekwa pamoja, tunaweza kufafanua

kuwa, uandishi ni njia ya mawasiliano ambayo

wanajamii hutumia lugha ili kuwasilisha mawazo

yao kwa njia ya maandishi. Maandishi yanalenga

kumpata msomaji atakayesoma kile kilichoandikwa

na mwandishi; na kinyume chake kuna masimulizi

ambayo yanalenga kumpata msikilizaji. Kwa hiyo,

tuna msomaji kwa upande mmoja na msikilizaji kwa

upande wa pili. Yote hayo yanawezeshwa na

uwepo wa lugha.

Uandishi upo wa aina mbalimbali kama vile:

uandishi wa habari, uandishi wa kiweledi, uandishi

wa kitaaluma, na uandishi wa kubuni


(www.wikipedia.com). Uandishi utakaoelezewa kwa

kina na kwa mapani ni ule wa kubuni-yaani

unaolenga kuwaelimisha watunzi chipukizi wajue

namna ya kutunga kazi za kubuni ambazo ni

riwaya, hadithi fupi, ushairi, tamthiliya, maigizo ya

jukwaani, redioni, televisheni na filamu. Lakini

halitakuwa jambo baya kama tutaangalia aina

zingine za uandishi ili tuwe na mawanda mapana

katika uandishi wa kubuni na usio wa kubuni.

Uandishi wa habari unahusika na uchunguzaji na

utoaji taarifa za matukio, mambo, au mwelekeo wa

jamii kwa hadhira pana. Lengo la uandishi wa

habari ni kuwataarifu wananchi kuhusiana na jambo

husika (Pardue OWL, 1995 -2016). Uandishi wa

habari huhusisha fani nyinginezo kama vile: uhariri,

upigaji picha, na filamu ya makala yaani

inayoonesha hali halisi (dokyumentari).

Kwa mujibu wa Rioba, Kilimwiko, na Karashani

uandishi wa habari unachukuliwa kama taaluma ya

mawasiliano inayojihusisha na ukusanyaji, tathmini,

na usambazaji wa habari au utoaji wa maoni

kuhusiana na jambo livumalo katika jamii.

Wanaendelea kumwelezea mwandishi wa habari

kwamba, ni mtu anayejihusisha na uandaaji wa

maudhui ya vyombo vya habari kama vile

kuzikusanya habari, kuzitathmini, kuzichakata au

kuzisambaza, na kutoa maoni kuhusiana na jambo

lililopo katika jamii (2000:1 Tafsiri yangu).

Uandishi wa kiweledi ni uwanja unaoibukia; ni

uwanja unatumia mikabala ya kitaaluma katika

kutoa mafunzo ya jinsi ya kutumia lugha (ritoriki)

kwa lengo ya kushawishi hadhira-kupitia katika

uandishi. Waandishi wa kiweledi wanaweza

kuajiriwa na kufanya kazi katika kampuni za

uchapishaji, serikalini, wanahabari, maafisa

masoko, wanasheria, walimu, au katika vyombo

vya mawasiliano (Alganquin College, 2016).

Uandishi wa kitaaluma ni ule unaoelezea jambo

kiyakinifu kwa kutumia muhtasari (ikisiri). Uandishi

wa kitaaluma unatumia mtindo ambao ni wa makini

sana, na unalenga kutazama jambo kiyakinifu-ili

kuijulisha hadhira nini kinaendelea kutokana na

uchunguzi; na kujenga hoja na mawazo kuhusiana

na jambo lililochunguzwa. Mathalani, uandishi wa

kitaaluma unakusudia kuziba pengo ambalo

limekuwepo katika taaluma bila kurudia yaliyoonwa

na watafiti wengine. Uandishi huu unapatikana

katika maeneo ya kitaaluma; na unasambaa kwa

hadhira pana kwa kupitia kwa waandishi wa habari,

vitini mbalimbali, hotuba, na majarida (Pardue

OWL, 1995 - 2016).

Uandishi wa kitaaluma unapaswa kuwa na lengo la

utafiti; na umuhimu wa kufanya utafiti huo uelezwe

kinagaubaga na uwasilishwe kwa ufasaha, ili

kumwezesha mtafiti mwingine kuurudia utafiti huo

na kupata matokeo yaleyale ili kujiridhisha (Pardue

OWL, 1995 - 2016).

Uandishi wa kubuni unachukuliwa kuwa ni pamoja

na uandishi wowote ule wa kubuni au usio wa

kubuni ambao sio wa kitaaluma (yaani uandishi

ambao haufuati kaida za kitaaluma); na sio wa

kiweledi (yaani haufuati kaida za kiweledi ambazo

zinalenga kuandika kwa kushawishi wasomaji); na

sio wa kihabari (yaani haufuati kaida za uandishi

wa habari ambazo ni kukusanya taarifa,

kuzitathmini, kuzisambaza, na kutoa maoni).

Uandishi wa kubuni ni ule unaojitokeza katika

riwaya, hadithi fupi, ushairi, tamthiliya, na filamu;

vitu hivi ni miongoni mwa aina mbalimbali za

uandishi wa kubuni.

Paul Engle katika makala yake ya “The Writer on

Writing” anaelezea uandishi wa kubuni (ashakum si

matusi) kwamba, ni sawa na kufanya mapenzi kwa

kuwa inastaajabisha kuona mtu anapagawa

(1963:3); sawasawa na uandishi wa kubuni

ambapo mtu anapagawa na kujikuta anabuni

matukio na kusimulia hadithi kwa namna akili yake

inavyomtuma. Kwa maneno mengine Engle (1963)

anastaajabu kuhusiana na ubunifu kufundishwa -

kwakuwa yeye anaona ni uwezo alionao mtu ndani

yake ambao unamfanya aandike na kubuni matukio

mbalimbali bila ya kufunzwa.

Kwa mujibu wa Semzaba (1997:75), anasema

“sanaa huanza na hisi ambazo kila mtu anazo”.

Nukuu hiyo ina maana kuwa, ubunifu wowote ule

unatokana na hisi ambazo zinamsukuma mtunzi.

Hisi hizo ni lile wazo linalomsumbua akilini ambalo

anataka aliwasilishe ili hadhira ifahamu kilichopo

moyoni mwa mwandishi. Semzaba anaendelea

kuelezea kuwa, mtunzi huchagua umbo la

kuwasilishia wazo lake kama ni hadithi fupi, riwaya,

tamthiliya, ushairi (kimapokeo au kimasivina). Yote

haya yanategemeana na uchaguzi wa mtunzi.

Mtu mwingine aliyejadili kuhusu uandishi wa kubuni

ni Khamis (1983:246). Yeye anaona kuwa, uandishi

wa kubuni ni namna mtunzi anavyoweza kuyasawiri

maisha ya mwanadamu na kuyatungia taswira

ambazo ziko mbali na mazoea ya mwanadamu;

kwakuwa, ni maisha kulingana na anavyoyaona

mwandishi katika dunia iliyomo kichwani mwake.

Naye Kezilahabi anaelezea kuwa, uandishi wa

kubuni ni sawa na ufuaji chuma; ambapo, mfua

chuma ana uwezo wa kutengeneza umbo lolote

kutokana na chuma hicho. Sawa na mwandishi

kwani yeye hutunza visa vingi kichwani mwake na

anao uwezo wa kuvifua visa hivyo na kutengeneza

kazi mbalimbali zenye kuisaidia jamii kwa njia

mbalimbali kama vile hadithi, michezo ya kuigiza na

kadhalika (Kezilahabi, 1983:237).

Tafsiri zote zilizodondolewa hapo juu, Wikipedia,

Engle, Semzaba, Khamis, na Kezilahabi

hazipishani sana katika kuelezea nini maana ya

uandishi wa kubuni. Kwa maneno mengine,

uandishi wa kubuni unaweza kuelezwa kuwa ni

mchakato ambao unatokana na kipaji au kipawa na

kujipika (kwa kusoma kazi nzuri za wengine), na

kujibidiisha ili uweze kuishi maisha yote kiubunifu -

yaani yaliyopita, yaliopo, na yajayo. Mwandishi wa

kubuni anatakiwa aweze kuchanganya maisha

halisi na ya kubuni ili aweze kutoa kazi bora.

Baada ya kupitia maana za aina mbalimbali za

uandishi, na ili kuweza kwenda sambamba katika

kozi hii ya uandishi-hatuna budi kuelewa mambo ya

msingi yakiwemo: hatua za kuandika insha,

matumizi ya alama za uandishi na uakifishi, na

makosa ya kawaida ya kiuandishi ambayo

yanafanya msomaji ashindwe kuelewa barabara

lengo la mwandishi.

1.2 Hatua za uandishi wa insha na muundo

wake

Uandishi wa kubuni ni aina mojawapo ya uandishi

wa insha. Hivyo, hatuna budi kujifunza namna ya

kuandika insha na miundo ya insha. Baadaye

tutajifunza matumizi sahihi ya alama za uandishi na

uakifishaji; na mwishowe tutaangalia makosa

mbalimbali yanayojitokeza katika uandishi wa

insha.

Katika mchakato wa uandishi, zipo hatua kadhaa

za kuzingatiwa ili insha yako au andiko lako liwe

zuri. Mahenge (2011) anabainisha hatua hizo kama

ifuatavyo:

Kwanza, ni kuchagua mada – hapa unapaswa

ujiulize swali la msingi ambalo ni: je unataka

kuandika juu ya kitu gani? Au jambo gani?

Mathalani, unataka kuandika kuhusu upishi wa

mlenda au mchunga.

Pili, ni kuiwekea mada yako mipaka – hapa inabidi

utambue kuwa mada yako itagusia mambo gani -

labda utataka kuongelea kuhusu mlenda. Je, ni

mlenda upi? Je, utatoa mifano mahsusi au ya jumla

ambayo inapatikana katika sehemu fulani? Labda

ni mazingira yapi utayachukua kama mfano wako –

je ni Kweditilibe, Kwedibangala, Kwamasukuzi, au

Kwedikwazu? Hii ni muhimu kwa sababu huwezi

kuandika katika insha moja kila kitu kilichopo

duniani kinachohusiana na mada yako.

Tatu, ni kuamua lengo la insha – je, lengo

unalolitaka ni lipi? Je unataka kushawishi?

Kuhamasisha? Kueleza na kufafanua? Au

kufundisha? Je, unataka kugusa hisia za wasomaji

wako? Chukulia mfano wa kadi za mialiko na kisha

linganisha na matini za kisayansi au hadithi na

kadhalika. Katika aina hizo za uandishi kunautofauti

wa malengo, na kwa namna hiyo hata uandishi

wake hutofautiana.

Nne, ni kuuamua mpangilio wa insha - je unataka

insha yako iwe na mpangilio gani? Je, unataka

ianzie na chanzo ambacho kitatuwezesha

kufahamu matokeo? Au utaanza na matokeo ya

jambo fulani na kisha ndipo utufahamishe kuhusu

chanzo chake au sababu za utokeaji huo?

Unaweza kufikiria kuhusu riwaya ya Mzimu wa

Watu wa Kale ambayo inaanza na mwisho na

kurudi mwanzo au riwaya ya Nyota ya Rehema

ambayo inaanza na mwanzo na kuendelea hadi

mwisho. Ni uchaguzi wako kuamua unataka

mpangilio wa kazi yako uweje.

Tano, ni kupanga insha kividokezo - yaani

kubainisha dondoo zitakazogusiwa katika uandishi

wako. Hapa unapanga kwamba, katika utangulizi

utazungumzia nini? Katika kiini utataja hoja au

sababu gani kwa mifano madhubuti; na katika

hitimisho, utatoa maoni gani au utasema nini ili

lengo lako litimie?

Sita, ni kuandika insha kwa umbo lililopendekezwa

na Aristotle – yaani umbo la: mwanzo, kati, na

mwisho kama ulivyo muundo wa tamthiliya ya

Kigiriki. Hii ina maana kwamba, katika sehemu ya

mwanzo - unatambulisha wahusika na mada

pamoja na mahusiano waliyonayo wahusika wako

ili kuweze kujengeka migogoro. Katika sehemu ya

katikati inatakiwa uikuze migogoro iweze kukua na

kubadili mwelekeo wa mchezo. Katika hitimisho

inatakiwa litolewe suluhisho au hitimisho la

mgogoro ambapo kunatakiwa kuwe na mshuko wa

mgogoro. Huu ndio muundo wa tamthiliya au drama

kwa mujibu wa Aristotle.

Saba, ni kupitia insha na kuifanyia marekebisho. Ni

vema kuandika na kuivumbika kazi yako - yaani

kuiweka kama vile umeisahau ili muda upite na

mawazo yako yawe mapya unapoisoma. Vile vile

waweza kumpa mtu mwingine akusomee ili

kusaidia kuona makosa ambayo yatasaidia

kuiboresha kazi yako.

1.3 Matumizi ya alama za uandishi

Alama za uandishi ni alama zinazosaidia katika

mchakato wa kuandika ili uweze kueleweka.

Mathalani, hakuna mtu awezaye kuzungumza kwa

dakika moja nzima bila kuvuta pumzi au kuhema!

Vivyo hivyo kazi ya alama za uandishi ni kuweka

pumziko fupi au pumziko kamili katika insha ili

msomaji aweze kukielewa kile kisemwacho.

Alama za uandishi zipo nyingi kwa kuzitaja ni

pamoja na: kituo (.); koma (,); nukta pacha (:);

swali (?); nukta mkato (;); mshangao (!); funga

na fungua semi (“ ”); mkato wa juu ('); kimstari

au haifa (-); deshi (...); mabano ( ); mabano ya

pande nne ([ ]); slashi (/). Ili kujijuvya kuhusiana

na matumizi sahihi ya alama za uandishi na

uakifishi, wanafunzi wanashauriwa wasome vitabu

vifuatavyo: Uandishi wa Kiswahili cha BAKITA,

Utungaji (1) cha Steven Mrikaria, Utungaji (2)1 cha

John Kiango na Mwenge wa Uandishi cha Wamitila

ambavyo kwa pamoja vinaelimisha juu ya matumizi

sahihi ya alama za uandishi. Vitabu hivi

vinapatikana katika duka la vitabu la TUKI

(TATAKI).

1.4 Uakifishaji

Uakifishi ni matumizi sahihi ya alama za uandishi.

Endapo mwandishi atatumia vibaya alama hizi, basi

atajikuta ameingia katika makosa na kumfanya

asieleweke. Makosa ya uakifishi hutokea kwa

kushindwa kutumia vizuri alama za uakifishi ili

kuonesha uhusiano wa neno na neno katika

sentensi au kati ya sentensi. Kama vile: kushindwa

kutumia kiusahihi kituo (.); koma (,); nukta pacha

(:); swali (?); nukta mkato (;); mshangao (!); funga

na fungua semi (“ ”); mkato wa juu ('); kimstari au

haifa (-); deshi (...); mabano ( ); mabano ya pande

nne ([ ]); slashi (/).

Vilevile, tunapoangalia suala la uakifishi pia

tunaangalia ujenzi wa aya. Aya inaundwa na wazo

moja. Aya inajengwa na sentensi mbalimbali

ambazo zinasaidiana kulikamilisha wazo husika.

Utungaji 2:Stadi za Lugha ya Kiswahili. Kiango, J.G.

TUKI. Dar es Salaam. 2009

Endapo mwandishi atachanganya mawazo mawili

kwenye aya moja, hapo atakuwa anafanya makosa

ya uakifishi kwa kuwa atamfanya msomaji

achanganyikiwe. Ni kama katika uzungumzaji, kwa

kawaida watu humaliza wazo moja kabla ya

kuingilia jingine. Na inapotokea mzungumzaji

akachanganya mawazo mawili kwenye

mazungumzo, wasikilizaji watamuuliza ‘una maana

gani’ au ‘sikuelewi’ na ndipo atagundua kuwa

amemchanganya msikilizaji. Hivyo itambidi arejee

kwenye mada husika ili aweze kwenda sambamba

na msikilizaji wake. Vivyo hivyo katika uandishi.

Ili uweze kuandika aya nzuri, inakupasa uzingatie

mambo yafuatayo:

Kwanza, kuwe na muunganiko wa mawazo kati ya

sentensi moja na nyingine; au kati ya aya na aya;

na kati ya aya zote zinazojenga wazo kuu. Ni

kanuni ya msingi katika uandishi wowote ule ambao

ni makini kwani hakupaswi kuwe na mgongano wa

hoja katika andiko husika. Ni muhimu kila sentensi,

aya, au kifungu cha maneno kihusike katika

kuifanya matini au andiko litiririke kimawazo.

Pili, usichanganye mawazo mawili au zaidi katika

aya moja – hili nalo ni tatizo linalowakumba

waandishi wengi ambao bado ni chipukizi. Kila aya

inapaswa ibebe wazo moja, na ukiona kuna wazo

tofauti linakujia – basi huna budi kulianziashia aya

yake na hivyo kuliongezea sentensi kadhaa ili

liweze kukamilika.

1.5 Makosa katika uandishi wa insha

Katika uandishi wa aina yoyote ile, matatizo

hayakosi na inabidi ufanye uhakiki mara

unapomaliza kuandika insha yako. Lengo ni

kuhakikisha kuwa wasomaji wako wanapata

ujumbe uliokusudia bila kupoteza au kuharibu,

maana kutokana na makosa ya kizembe. Miongoni

mwa matatizo au makosa haya ni pamoja na:

makosa ya kisintaksia yaani kukosekana

upatanisho wa kisarufi kati ya kiima na kiarifu;

kukosea herufi za uakifishi; makosa ya herufi;

kutonyooka kwa wazo; kukosa muunganiko wa

mawazo; kuchanganya mawazo mawili au zaidi

katika aya moja; na uwasilishaji mbaya au mbovu

(Mahenge, 2011).

Matatizo mengine ni kama vile: kutokuwa makini

katika uandikaji wa sentensi; kukosekana

usambamba wa njeo, hali, na kauli; matumizi

mabaya ya kauli ya kutenda na kutendwa;

kukosekana kwa uhusiano kati ya kichwa cha

habari na habari yenyewe; matatizo ya tafsiri;

matatizo ya finyazo; na athari ya matamshi katika

maandishi.

Makosa ya uakifishi hutokea kwa kushindwa

kutumia vizuri alama za uakifishi ili kuonesha

uhusiano wa neno na neno katika sentensi au kati

ya sentensi. Kama vile: kushindwa kutumia

kiusahihi kituo (.); koma (,); nukta pacha (:); swali

(?); nukta mkato (;); mshangao (!); funga na fungua

semi (“ ”); mkato wa juu ('); kimstari au haifa (-);

deshi (...); mabano ( ); mabano ya pande nne ([ ]);

slashi (/). Ili kujijuvya kuhusiana na matumizi sahihi

ya alama za uandishi na uakifishi, wanafunzi

wanashauriwa wasome kitabu kiitwacho Uandishi

wa Kiswahili na Utungaji (1) cha Steven Mrikaria

na Utungaji (2) cha John Kiango ambavyo kwa

pamoja vinaelimisha juu ya matumizi sahihi ya

alama za uandishi.

Matatizo mengine ni ya herufi au makosa ya

kiherufi kwani ni vigumu kujua wakati unaandika

kazi. Ili kuepukana na tatizo hili, unashauriwa

kuangalia kwenye kamusi yale maneno usiyo na

uhakika nayo ili ujue herufi zake kama ni sahihi au

la. Unaweza kufanya kosa hili kwa kudondosha

herufi mojawapo katika neno bila kufahamu

kwamba umekosea. Mara nyingi matatizo haya

hutokea pale ambapo hutarajii kufanya kosa. Yote

haya yanachangia katika kumpotosha msomaji

(Mahenge, 2011).

Kukosekana upatanisho wa kisarufi kati ya kiima na

kiarifu nalo ni tatizo wanalokumbana nalo

waandishi wa Kiswahili. Mathalani, kama una

sentensi inayosema: “watoto zake wanalia kila

mara”. Hapa upatanisho wa kisarufi kati ya nomino

na kitenzi haupo kwa kuwa sio sahihi kusema

‘watoto zake’ kwa kuwa kimilikishi hicho ‘zake’

kinatumika katika ngeli nyingine na sio ngeli ya

kwanza inayohusika na viumbe hai. Kiusahihi

ilipaswa sentensi hii isomeke hivi: “watoto wake

wanalia kila mara” (Mahenge, 2011).

Kutonyooka kwa wazo ni tatizo jingine ambalo

linawakumba waandishi wengi wanaojifunza stadi

hii ya uandishi. Ili msomaji aweze kukusoma na

kukufuatilia kwa kile unachokisema – ni muhimu

uhakikishe wazo lako limenyooka. Je,utawezaje

kufikia usahihi huo? Mbinu ipo nayo ni kumpa mtu

mwingine ambaye ni tofauti na wewe ili akusomee

kazi yako na kukukosoa pale ambapo panampa

utata wa aina yoyote ile. Kwa kufanya hivyo,

itakuwezesha kuandika mawazo ambayo

yamenyooka (Mahenge, 2011).

Kukosekana muunganiko wa mawazo kati ya

sentensi moja na nyingine; au kati ya aya na aya;

na kati ya aya zote zinazojenga wazo kuu. Ni

kanuni ya msingi katika uandishi wowote ule ambao

ni makini kwani hakupaswi kuwe na mgongano wa

hoja katika andiko husika. Ni muhimu kila sentensi,

aya, au kifungu cha maneno kihusike katika

kuifanya matini au andiko litiririke kimawazo

(Mahenge, 2011).

Kuchanganya mawazo mawili au zaidi katika aya

moja – hili nalo ni tatizo linalowakumba waandishi

wengi ambao bado ni chipukizi. Kila aya inapaswa

ibebe wazo moja, na ukiona kuna wazo tofauti

linakujia – basi huna budi kulianziashia aya yake na

hivyo kuliongezea sentensi kadhaa ili liweze

kukamilika (Mahenge, 2011).

Uwasilishaji mbaya au mbovu wa andiko lako

unaweza kumfanya msomaji ashindwe kusoma na

kuitupilia mbali kazi yako. Ni lazima kwa mwandishi

yoyote yule kuhakikisha kwamba anajua masharti,

kanuni, na miongozo mbalimbali inayomwezesha

kuandika kazi vizuri na kuipangilia kwa ustadi ili

imvutie msomaji wake (Mahenge, 2011).

Kukosekana usambamba wa njeo, hali, na kauli ni

tatizo jingine linalojitokeza katika uandishi.

Kwakuwa, wakati mwinginr utakutana na sentensi

katika magazeti ya Kiswahili zinampishano wa njeo.

Mathalani, tunasikia mara kwa mara waandishi wa

habari wakisoma habari zao kama ifuatavyo: ‘watu

200 kujeruhiwa vibaya kwenye ajali ya meli ya MV

Spice Islander’. Tatizo lililopo la kinjeo linahusiana

na matumizi ya ‘ku’ katika kitendo cha kujeruhiwa

ambayo kiusahihi inamaanisha watu hao bado

hawajajeruhiwa na kwamba ni matarajio

watajeruhiwa – haya ni makosa kwa kuwa lengo la

habari ni kuripoti kuhusu ajali iliyotokea na kujeruhi

watu 200. Kwa hiyo, kiusahihi habari hiyo

ingesomeka kuwa ‘watu 200 wamejeruhiwa katika

ajali ya meli ya MV Spice Islander iliyotokea

Zanzibar’.

Kukosekana kwa uhusiano kati ya kichwa cha

habari na habari yenyewe – hili ni tatizo ambalo

linajitokeza sana katika habari za kwenye magazeti.

Japokuwa waandishi katika uwanja huu wanalitetea

jambo hilo kuwa ni mbinu ya kuuza magazeti –

lakini sisi tunasema wamepitiliza kwa kuwa

wangeweza kutengeneza vichwa vyenye mvuto

hata bila ya kuvipotosha. Upotoshaji huu unaweza

kuwafanya waonekane ni ‘waongo’ au ‘wambeya’.

Mathalani, utakutana na habari inayosema

“Kanumba amcharaza baba yake laivu”. Msomaji

atapata shauku ya kununua gazeti hili ili aone ni

kwa vipi kijana huyu amekosa adabu kiasi hicho –

cha kumfanya amcharaze baba yake. Kinyume

chake, ukifungua na kuisoma habari hiyo, inaelezea

mkasa tofauti; kwamba, Kanumba alihojiwa na

mwandishi wa gazeti xyz kuhusiana na ‘mahusiano’

yake na mzazi wake. Alichofanya msanii huyu nguli

ni kubainisha kwa kina kuwa mzazi huyu

alimtelekeza wakati yuko mdogo baada ya baba

huyo kuona mke mwingine. Kwa hiyo, katika habari

hiyo hakuna jambo lolote linalohusiana na

Kanumba kumcharaza baba yake.

Matatizo ya tafsiri nayo yamekuwa yakiwasumbua

waandishi wengi. Matatizo haya yanajitokeza

katika miktadha mbalimbali ya kutafsiri kisisisi bila

kuzingatia miundo ya lugha chanzi na ile ya lugha

lengwa. Kwa mfano, imekuwa ni kawaida katika

vyombo vya habari kusoma habari kama hizi:

“Zantel yatoa kumi milioni kusaidia watoto yatima”.

Hili ni kosa la kimuundo kwa kuwa muundo wa

lugha chanzi unaanza kutaja kivumishi kabla ya

nomino – yaani ‘ten million’; wakati lugha lengwa

ina muundo unaotangulizi nomino kabla ya

kivumishi – yaani ‘milioni kumi’. Kwa hiyo,

kutokuzingatia kanuni za kiisimu za lugha lengwa

na lugha chanzi ni tatizo kubwa ambalo linasumbua

waandishi wengi wa habari za magazetini hapa

nchini Tanzania (Mahenge, 2011).

Matatizo ya finyazo nayo yanajitokeza sana katika

mazungumzo ya watumiaji lugha ya Kiswahili.

Wazungumzaji wanasahau kwamba finyazo ile

inasimamia jina la kampuni, chama, au chombo

chochote kile cha serikali au binafsi; wanachofanya

ni kuipachika finyazo hiyo katika ngeli isiyohusika.

Tutatoa mifano ili tuweze kueleweka: “CHADEMA

yashinda Tarime”. Hapa pana kosa la ngeli ambalo

limekuwepo kutokana na matumizi ya finyazo

ambayo yamemchanganya mtumiaji wa lugha na

kumfanya asahau kuwa finyazo hiyo inasimama

badala ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo

na kwamba, kipatanisho chake ni cha ngeli ya

KI/VI. Kwa usahihi kichwa hicho cha habari

kilipaswa kuandikwa hivi: “CHADEMA chapata

ushindi Tarime” (Mahenge, 2011).

Mwisho, ni athari ya matamshi katika maandishi.

Hili nalo limekuwa ni tatizo linalowasumbua

waandishi wengi katika uandishi wa Kiswahili. Kuna

baadhi ya wazungumzaji wa lugha ya Kiswahili

wanashindwa kuongea kwa ufasaha kutokana na

athari ya lugha mama – na jambo hili linajitokeza

katika uandishi wao. Kuna watu hawana ‘h’ au

mahali ambapo hapatakiwi kuwe na ‘h’ wao

wanaipachika. Kwa mfano, baadhi ya

wazungumzaji ambao asili yao ni Wahaya huwa

wanashindwa kuzingatia matumizi sahihi ya ‘h’ na

kinyume chake. Si ajabu ukamsikia mtu akisema

‘hasili ya binadamu ni sokwe mtu’ badala ya

kusema: ‘asili ya binadamu ni sokwe mtu’. Mifano

iko mingi tu kama vile ya Wachaga, Wamasai,

Wakurya, Wasukuma, Wanyamwezi na wengineo

kwa kuwataja kwa uchache. Kila mmoja katika

makabila tuliyoyataja na yale ambayo

hatukuyataka, asipozingatia matumizi sahihi ya

lugha ya Kiswahili - atajikuta akifanya makosa

ambayo hakukusudia kuyafanya (Mahenge, 2011).

1.6 Hitimisho

Baada ya kukupitisha katika nadharia ya uandishi

kwa ujumla, pamoja na matumizi ya alama za

uandishi na uakifishi; na vilevile makosa ya

kawaida ya kiuandishi na namna ya kuyaepuka,

sasa ni wakati muafaka wa kukudadavulia kwa kina

kuhusu ‘uandishi wa kubuni’ katika miktadha

mbalimbali.

Ninaposema miktadha mbalimbali ninamaanisha

uandishi katika filamu, ushairi, riwaya, tamthiliya, na

drama. Twende pamoja katika aina hizo za

uandishi. Lakini kabla ya kulifiia hilo, itakuwa vizuri

kama nitakupitisha katika hatua muhimu ya ‘namna

ya kuanza kuandika’. Kwa maneno mengine,

sehemu inayofuatia itakuwa ni mbinu na nyenzo za

kuanza kuunga na kuandika kazi yako.

SURA YA PILI

UNAANZAJE KUTUNGA KAZI YA KISANAA?

2.0 Utangulizi

Nimekuwa na kawaida ya kusikia watu wakiniuliza

‘unaanzajeanzaje kutunga na kuandika’? Leo

nitakupatia siri ya mafanikio ambayo inaniwezesha

kutunga, na huenda na watunzi wengine wana siri

zao ambazo huenda ni tofauti kabisa na siri zangu.

Jambo la msingi ni kufanyia kazi mbinu au siri

nitakazokujulisha. Kuna vitu nimeviita ‘kanuni’

navyo nitakufafanualia hapa chini:

2.1 Kanuni Zinazokuwezesha Kubuni / Kutunga

Kutokana na uzoefu wangu mdogo, kuna kanuni

tano ambazo ninaona ni muhimu ili kumwezesha

mtunzi chipukizi atunge kazi yake. Sijaona mahali

popote ambapo nimesoma na kukuta zinaitwa

‘kanuni’ ila ni mimi mwenyewe matakwa yangu

ndiyo yamenifanya niziite hivyo.

Kanuni ya kwanza: utafiti. Mwandishi

unatakiwa ufanye utafiti ili uweze kupata taarifa

sahihi za jambo ambalo unataka kuliandikia

simulizi. Unaweza ukaniuliza utafiti nitaufanyia

wapi? Kuna sehemu kadhaa ambazo zinaweza

kukusaidia kupata tarifa unazozitaka. Mojawapo ni

kujisomea. Soma vitu mbalimbali kama ni vitabu,

magazeti, majarida, mitandao na kadhalika.

Ukikutana na maarifa yanayokuvutia yaandike. Pia

unaweza kufanya utafiti kwa kuwaulizauliza watu

kuhusu jambo husika. Unapopewa taarifa hizo

ziandike. Tatu ni kwa kufanya ziara katika maeneo

mahususi ili uweze kupata data unayoihitaji.

Tembelea sokoni ukakutane na wamachinga

ambao wamepanga bidhaa zao barabarani na mara

mgambo wanawafukuza na kuwapora mali zao, na

kuzifanya ni za kwao! Ukienda huko na kuulizauliza

utapata mengi. Yaandike na utunze kumbukumbu

kwani utayahitaji siku moja.

Kanuni ya pili: uwe na kumbukumbu. Ili uwe

mtunzi mzuri unatakiwa upambane na tatizo la

kusahausahau. Ukiwa msahaulifu sana hata mahali

ulipoandika dondoo zako kwa ajili ya hadithi

utapasahau. Ukiona kiwango cha kusahau kinazidi

kuongezeka, tafadhali anza kula vyakula asilia.

Kula dona, kula mchemsho, punguza kula vitu vya

kiwandani. Fanya mazoezi kama vile kuruka kamba

au kukimbia n.k. Kwa namna fulani, utaifufua

kumbukumbu yako.

Kanuni ya tatu: kuza stadi yako ya uandishi

ili uweze kujieleza kwa maandishi. Inakubidi

ujifunze namna ya kutumia alama za uandishi na

uakifishi ili unapoandika usifanye makosa. Lakini

vilevile ni kuhusu namna wenzako wanavyoandika

kazi zinazowavutia wasomaji. Hakikisha unafanya

mazoezi ya kutosha ya kuandika na kuwaomba

watu wakusomee kazi na kukushauri. Pia soma

insha zinazoelekeza namna ya kuandika vizuri.

Kanuni ya nne: kuwa mbunifu. Kama

unataka kuwa mwandishi huna budi kuwa na mbinu

za ‘kiubunifu’ ambazo zinakuwezesha kuugeuza

uongo na kuufanya uwe ukweli. Ukweli katika

‘ulimwengu wa hadithi’. Ni ukweli ambao

unapatikana kutokana na ‘mantiki’ ya hadithi

kwamba A imesababisha B na kisha ikasababisha

C. Kwa hiyo huo ndio ‘ukweli’ ninaoumaanisha.

Ukweli ndani ya hadithi yaani kwa kimombo

(believability of what you are saying). Ni jinsi

unavyowashawishi wasomaji au watazamaji wako

na wakashawishika – ndipo huo ‘ukweli’

unapopatikana.

Kanuni ya tano: isuke ploti yako ili iweze

kugusa hisia na hivyo kumvutia hadhira wa kazi

yako. Ploti ni ule mtiririko wa hadithi

unavyoupangilia kutoka mwanzo wa hadithi yako

hadi unapofikia mwisho. Je, ule mpangilio wako wa

visa na vituko unakupatia ucheshi? Je, msomaji

akisoma atachekeshwa? Je, ataumizwa kihisia na

atalia? Je, atakasirika? Kwa hiyo unatakiwa uweze

kuisuka ploti yako ili uibue hisia mbalimbali kwa

hadhira.

Ukishakuwa na ‘kanuni’ zako, hakikisha

unaandamana na ‘mwandani’ wako ili uweze

kunakili kila kitu muhimu ambacho kitakusaidia

kupata visa na vituko vya kuichangamsha kazi

yako. Mwandani huyu wa mtunzi ni shajara na

kalamu. Hakikisha popote unapokwenda una hivi

vitu viwili ili uweze kuandika na kunukuu dondoo

muhimu za kukusaidia.

Mara nyingi niwapo daladalani, na hasa

nikipata kiti nikakaa au nikikosa kiti na nikasimama,

ndipo hapo ninapopata visa na vituko vya

kuandikia. Wakati mwingine utasikia watu

‘wakitukanana’ au ‘wakizodoana’ kwa sababu

wamekanyagana miguuni, hapo ndipo hupata

vituko kutokana na maneno yanayowatoka

vinywani mwao. Mimi huyaandika maneno hayo na

wakati mwingine nikiumba wahusika wangu katika

hadithi huwa ninawapa maneno yaleyale

yaliosemwa na watu halisi.

Ninafurahia sana kuwa abiria ndani ya gari

kwa kuwa ninapata fursa ya kubuni hadithi au

tamthiliya. Kutokana na hili, mara nyingi ninapanda

daladala kwa kuwa ninapata fursa ya kuvinjari na

kusawiri wahusika wangu wa hadithini; tofauti na

kuendesha gari ambako kunanikosesha fursa hiyo

kwa kunitaka niwe makini. Jambo hili la kuvinjari

wahusika wangu, wakati mwingine hunilazimu

‘kujipitiliza’ kituo ilimradi tu mtiririko wangu wa

simulizi ufikie mahali pazuri. Yaani wakati mwingine

badala ya kushuka chuo kikuu huamua kupitiliza

hadi mwisho wa gari na kisha kugeuza upya na

kurudi tena chuo na hapo ndipo hushuka. Yaani

mzuka unapokujia ndipo hapohapo pa

kugangamala na kuweka mambo sawa. Kuhusu

kuwa dereva ipo siku nitarejea ulingoni!

2.2 Utaanzaje?

Anza kuchagua ‘nafsi’ ambayo utaitumia katika

kusimulia. Je, unataka kusimulia visa na mikasa

hiyo kwa kutumia nafsi ya kwanza? Nafsi ya

kwanza ni ile inayotumia ‘ni’ katika vitenzi. Kwa

mfano ni ukisema ‘nitakununulia gauni’...ile ‘ni’

iliyojitokeza hapo ndiyo hiyo nafsi ya kwanza. Nafsi

ya kwanza inaonesha simulizi iko karibu na

mwandishi na kwa namna fulani anayoyaandika

yanamhusu au amepitia uzoefu huo.

Au la unataka kusimulia kwa nafsi ya tatu? Nafsi

ya tatu ni ile inayosimulia hadithi kwa kutumia ‘a’

yaani kitenzi kinachukua kiambishi hicho cha awali.

Kwa mfano ni ukisema ‘akamnunulia gauni’

ambayo inamaanisha ni mtu mwingine. Au

unaweza ukatumia nafsi ya pili ambayo inaonesha

unamwambia msomaji ‘wewe’. Kwa mfano ni

ukisema ‘ukamnunulia gauni’. Je, umeona tofauti?

Kama hujaona tofauti, nitarudia hapa chini kama

ifuatavyo:

 Nikamnunulia gauni...[mimi]

 Akamnunulia gauni....[yeye]

 Ukamnunulia gauni....[wewe]

Ukishachagua nafsi unayotaka kuitumia anza

kuandika sentensi yako. Kuchagua nafsi fulani ya

usimulizi hakumaanishi kuwa umebanwa usitumie

nafsi zingine, la hasha! Utazitumia kwa uhuru ila

jambo la msingi uhakikishe simulizi haipotezi

mwelekeo. Kama ulikuwa unasimulia kuwa ni tukio

linalokuhusu, {yaani mimi} msomaji atatarajia aone

hadi mwisho simulizi imekuwaje japokuwa hapa na

pale utachanganya nafsi hizo katika kusimulia.

Baada ya kuchagua nafsi ya usimulizi, anza

kuviungnisha visa vyako kimantiki. Kwa mfano,

kwenye shajara yako kuna visa mbalimbali

ambavyo uliviokota barabarani, kanisani, msikitini,

dukani, sokoni, buchani, darasani, ofisini,

daladalani na kadhalika. Visa hivi na vituko na

daiolojia huenda uliviandika katika shajara yako.

Sasa vipitie uvisome na uone ni kwa namna gani

utavipangilia na kuvifanya vilete maana kimantiki?

Baada ya kuzipitia dondoo hizo, bila shaka

umeshajikumbusha mikasa na visa mbalimbali

ulivyowahi kuvirekodi.

Kinachofuata ni kuwaumba wahusika wako

ili uweze kuwabebesha majukumu mbalimbali.

Majukumu hayo ndiyo yatakayokuongoza ili uumbe

wahusika kadhaa (idadi). Kwa mfano, katika jamii

uliona mkasa mmoja wa kijana mmoja wa kike

ambaye alikataliwa na kijana aliyempa mimba, na

kisha siku mzozo ulipotokea kulikuwa na watu

kadha wa kadha walioshuhudia n.k. Basi hapo

tayari una mhusika mvulana, msichana, mpitanjia,

n.k n.k n.k. Hapo sasa unaukuza mgogoro kuwa

itakuwaje akienda kwao (yule binti akienda kwa

wazazi wake), na ndugu n.k. Jaribu kuunganisha

visa na mikasa ili itiririke na kuvutia hisia za

wasomaji.

Mwisho ni kuanza kuipangilia hadithi yako

au filamu au drama ili mtiririko uvutie. Kwa mfano,

haitakuwa na maana kama utatuandikia hadithi

ambayo visa vyake vimekaa shaghalabaghala. Kwa

mfano, unatumbia msichana amefukuzwa na

wazazi wake baada ya kugundulika ana mimba. Ila

tulipokuwa tunasoma hadithi hatujaona hata mahali

pamoja ambapo umetuonesha kuwa binti huyo

alikuwa na mpenzi na hatimaye akaanza

mahusiano na huyo mvulana. Kwa hiyo,

kunahitajika mantiki ya hadithi yako, yaani tuone

msichana na mvulana wakianza kupendana; kisha

tuone mahusiano; kisha tutakapoambiwa binti

kapata mimba tutaelewa kwamba ilianzajeanzaje,

yaani kunakuwa na ‘mantiki’ ya kimtiririko ambayo

ndiyo inawezesha kupatikana ‘ukweli wa hadithi’.

Kinachofuata...

Anza sasa kuandika... anza....anza....anza...

(chagua umbo unalolitaka uandikie. Je, unataka

kuandika riwaya, hadithi fupi, shairi, drama ya

jukwaani, runingani, au redioni? Au je unataka

kuandika filamu? Uchaguzi ni wako. Amua na

uanze kuandika).

SURA YA TATU

UANDISHI WA MISWADA YA FILAMU

Usuli wake

3.0 Filamu ni Nini?

Filamu imeelezewa na watu mbalimbali na kwa

namna tofauti. Miongoni mwa watu hao ni Kasiga

(2013) ambaye anasema kuwa, filamu ni dhana

inayohusishwa na hadithi zinazotambwa kupitia

picha jongefu zilizorekodiwa kutoka kwenye

mazingira fulani, zikiwahusisha waigizaji, mazingira

yao, desturi zao pamoja na utamaduni uendao

sambamba na mawasilisho ya maudhui

yaliyosanwa kwenye sanaa hiyo.

Mtu mwingine ambaye anafasili filamu ni

Kileo (2012) ambaye anasema kwamba, filamu

kama kipengele cha fasihi ni utanzu wa drama

ambao una nafasi kubwa katika kufikisha ujumbe

kwa hadhira kwa njia ya maneno na matendo ya

waigizaji. Japokuwa Kasiga amejitahidi kutaja

mambo muhimu yanayohusiana na filamu, lakini

bado kuna vitu vya msingi ameviacha. Hajaelezea

sifa ya ujumuishi (maltimodo) ambayo

inaipambanua filamu na aina zingine za sanaa.

Tunaweza kusema kwamba, filamu ni utanzu

wa fasihi unaotumia picha jongefu na mbinu za

kifilamu ili kuwasilisha hadithi inayosimuliwa na

watu wengi ambao ni mwandishi, mpigapicha,

msimulizi, mhariri na mwigizaji. Wote hawa

wansaidiana ili kusimulia hadithi. Mbinu hizi za

kifilamu ni aina ya picha inayopigwa (ndogo,

kubwa, kubwa sana); mahali inapopigiwa (juu,

chini, kawaida); mpangilio wa vitu mbele ya kamera

(mizensini); mapigo, sauti na midundo; mwangaza

au giza; mtazamo (POV), ploti, uhusika wa

wahusika na msimulizi (Murray, 1987). Filamu si

utanzu wa drama japokuwa inatumia waigizaji

kama inavyofanyika katika drama.

3.1 Filamu ni Fasihi?

Kuna uhusiano mkubwa sana kati ya filamu na

fasihi. Uhusiano huo unatokana na ukamilishanaji

wa pande zote mbili kama anavyoelezea Perrier

(1992) kwamba, fasihi inatoa mwangaza kuhusu

filamu, na filamu inathibitisha thamani ya fasihi. Mtu

mwingine ambaye anaonesha uhusiano huo ni

Jann (2001) anayeelezea kuwa, filamu kama ilivyo

drama na tanzu simulizi kama vile riwaya, zote

zinatumia usimulizi ili kufikisha ujumbe kwa

hadhira. Hii ina maana kuwa, fasihi (tukichukulia

mfano wa riwaya) ina mambo yanayoingiliana na

filamu.

Kazi zote zinatumia wahusika, msimulizi,

ploti, lugha na mtazamo ili kusimulia hadithi. Katika

riwaya, mwandishi anatumia sura wakati kwenye

filamu anatumia fremu. Hadhira ya kiriwaya

inatumia macho kusoma hadithi, wakati hadithi ya

kifilamu inatumia macho kutazama filamu. Kwa

hiyo, kuna mwingiliano kati ya fasihi na filamu.

Kasiga (2013) anaelezea kuwa, uhusiano wa filamu

na fasihi unatokana na kuwapo hadithi

inayotambwa, wahusika, matumizi ya hisia na

taswira mbalimbali, pamoja na daiolojia zenye

maneno kutoka katika lugha yoyote izungumzwayo

na wanadamu.

Kitu muhimu ambacho Kasiga hajakitaja

waziwazi ni aina mbili za lugha zinazotumika katika

kusimulia hadithi ya kifilamu. Lugha ya kwanza ni

hiyo aliyoitaja ambayo inatumiwa na waigizaji

kupitia daiolojia au maneno waliyopewa

kuzungumza; lakini lugha ya pili ni lugha ya kifilamu

ambayo inatumiwa na mwongozaji, mpiga picha na

mhariri ili kusimulia hadithi. Hii lugha ya kifilamu

inahusisha matumizi ya vitu kama mwangaza au

giza; maleba; midundo, milio na sauti; mpangilio wa

vitu mbele ya kamera (mizensini); rangi mbalimbali;

mahali pa kupigia picha (kamera engo) na aina ya

picha inayopigwa (kamera shoti – ni kitu kizima; ni

saizi ya pasipoti, ni ya sura tu, ni ya pua tu n.k).

Kwa hiyo, kwa kuwa fasihi ni sanaa

inayotumia lugha ili kufikisha ujumbe wake katika

jamii, basi, tunaweza kusema kuwa, filamu ni fasihi

inayotumia lugha za aina mbili ili kufikisha ujumbe

wake kwa hadhira. Hivyo, filamu si tawi la fasihi

simulizi (Kasiga, 2013) na wala si utanzu wa drama

(Kileo, 2011) ila “filamu ni fasihi ya picha jongefu

inayosimuliwa na watu wengi kwa kutumia lugha za

aina mbili” (Mahenge, pendekezo la PhD, 2014-

2016, UDSM).

Syd Field (1994:180 - 203) anadadavua

vipengele muhimu ambavyo vinatakiwa viwemo

katika mswada wa filamu; na vilevile anaelezea jinsi

wazo linavyopatikana; hadithi ya filamu

inavyosukwa; jinsi wahusika wanavyopaswa

kujengwa na hulka zao tofauti; jinsi ya kuisuka ploti

katika filamu na jinsi ya kuuandika mswada wa

filamu. Kuna vipengele muhimu ambavyo

vinatakiwa viwemo katika mswada wa filamu

ambavyo ni: kutaja namba ya onesho, mahali

onesho linapofanyikia, muda ambao onesho

linafanyika na kama ni nje au ndani. Maelekezo

mengine ni namna ya kuandika majina ya wahusika

na mazungumzo yao, na maelekezo mengine

yanayosaidia kuingia kwenye uhusika wa upande

mmoja; na kumsaidia mwongozaji kwa upande

mwingine.

3.2 Ufundi wenyewe

3.2.1 Namna ya kuanza kuandika wazo

Katika utungaji wa filamu, anaza kuandika ikisiri

(sinopsis) ambayo haizidi maneno 50. Yaani huu ni

muhtasari tu wa kazi yako inahusu nini. Haya ndiyo

yale maneno unayoyaona kwenye kasha la filamu.

Sema kwa ufupi sana filamu yako inahusu nini.

Kwa mfano: Tumiya anapendana na

kimwana mmoja huko kijijini. Tumiya anakwenda

kutoa mahari na anakuta kimwana ameshaolewa

na Njemba. Tumiya anapigana na Njemba na

anapelekwa polisi. Kesi inasomwa na Tumiya

anakosa dhamana. Tumiya anafungwa na baada

ya mizei 3 anaachiliwa. Tumiya anarudi mjini na

kukuta amefukuzwa kazi. Nini kitaendelea?

3.2.2 Kuza wazo lako

Andika kwa dondoo mawazo makuu ambayo

yatahusika katika filamu. Yaani ile hadithi yako

itakavyokuwa, mambo yatakayohusika, wahusika

watakaoshiriki, nk. Hakikisha unalipanua wazo lako

katika sentensi moja. Kila sentensi unayoiandika

ibebe wazo moja na uipe namba yake. Upanuzi huu

wa wazo usizidi kurasa tatu. Yaani hizi ni dondoo

muhimu tu bila kufafanua.

Kwa mfano ukisema: (1) Tumiya anakwenda

kijijini kuposa. (2) Binti aliyetaka kumposa

ameshaolewa na njemba moja. (3) Ugomvi

unazuka Tumiya na njemba iliyomwoa kimwana

wake (4). Njemba inampeleka Tumiya polisi

kumshitaki (5). Tumiya anawekwa lupango kwa

kusababisha vurugu (n.k n.k n.k sasa endelea hadi

mwisho wa simulizi yako).

Baada ya hapo ndio sasa unaanza

kuidadavua hadithi yako ya filamu katika kila

onesho kama tutakavyoonesha hapa chini kwenye

uandishi wake.

3.3.3 Uandishi wake:

Uandishi wa mswada wa filamu ni tofauti sana na

uandishi wa mswada wa mchezo wa redio au

mchezo wa jukwaani au runinga (tamthiliya). Kuna

vitu kadhaa vinavyoandamana na uandishi wa

mswada huu, navyo ni pamoja na:

(i) Kutaja namba ya onesho ambalo

litaonekana baada ya filamu kuwa tayari.

Katika ujengaji wa onesho hili- picha nyingi

hupigwa mpaka pale mpigapicha na

mwongozaji watakapo ridhika na picha

zilizochukuliwa. Kwa lugha ya Kiingereza

huita 'takes' ambapo ina maanisha idadi ya

picha ambazo zitapigwa ili kuja kutengeneza

hadithi nzima. Baada ya kuandika namba ya

onesho kwa herufi kubwa inafuata nukta.

(ii) Inapaswa kutajwa kuwa onesho litafanyikia

wapi? Je ni nje ya nyumba au ni ndani? Pia

inapaswa kuandika eneo hilo kwa herufi

kubwa kisha inafuatia nukta.

(iii) Kisha kitu kinachofuatia ni kutoa ufafanuzi

wa sehemu husika litakapofanyika onesho

hilo. Baada ya kusema kuwa ni ndani au nje

- yabidi kufafanua kuwa ni sehemu gani

hasa? Je ni shambani, jikoni, sebuleni au

bafuni?

(iv) Mwisho katika kukamilisha jina la onesho ni

kutaja wakati wa onesho hilo: je ni usiku,

asubuhi, jioni, au mchana? Ni lazima hali ya

asili ya maziingira isaidie kuonesha uhalisia

wa muda. Kama ni vigumu kuipata hali

halisia inawezekana kufanya ufundi na

utundu mbalimbali kupitia kompyuta ili

kupata picha zitakazoleta ukubalifu na

kuaminika kwa watazamaji. Jambo hili la

kukosa mbinu na maarifa ya kutengeneza

filamu zinazo ‘aminika’, linafanya kazi nyingi

za wasanii wa hapa nyumbani Tanzania

watengeneze filamu ambazo zinaonekana

zinadanganya, kiasi kwamba, hata mtoto

mdogo, anaweza kugundua udhaifu

unaowasilishwa katika kazi hizi. Kwa mfano,

wahusika wanajibizana kuwa ni ‘asubuhi’

wakati kwenye picha jongefu inaonesha

tayari ‘giza’ limeingia. Haifai kamwe

kudanganya namna hiyo! Kama msanii

ameamua kujikita katika uwanja huu ni

lazima ajifunze A, B, C, D’s za kazi hii ya

utengenezaji wa filamu ambapo ‘believabiliy’

ni kitu cha lazima ili ukweli wa hadithi

upatikane.

(v) Maelekezo ya matendo ya mhusika

yanaandikwa katika hati ya kawaida ambayo

sio ya mlalo. Maelekezo haya yanaandikwa

tangu pale karatasi inapoanzia na kuendelea

hadi inapoishia na kisha inawezekana

kuingia mstari wa pili na kadhalika. Aya

hazitumiki katika uandishi wa miswada ya

filamu, bali ni kuandika tu kwa mfululizo na

mwendelezo bila kuweka aya.

(vi) Mazungumzo ya wahusika yanaandikwa

katikati ya mstari chini ya jina la mhusika.

(vii) Jina la Mhusika linaandikwa kwa herufi kubwa

na chini yake linapigiwa mstari. Kisha

yanaandikwa maneno anayoyasema

mhusika huyo sambamba na jina lake.

Maandishi haya yanatakiwa yawe katika hati

ya kawaida ambayo siyo ya mlalo. Hebu

tupate mfano ambao utatuonesha namna ya

kuandika muswada wa filamu ili kupata

dhana tulilolijadili katika namba moja hadi

saba.

1. NDANI. CHUMBANI. USIKU.

Beti na Tuma wamekaa kitandani

wanatazamana. Chumba kina taa ya glopu

ambayo inatoa mwanga wa buluu.

BETI

Leo ni zamu yako ya kuzima taa.

TUMA

Zima wewe

BETI

Basi tulale hivyohivyo

TUMA

Sawa tu

Beti anajilaza na Tuma anajilaza pia. Beti

anavuta shuka na wanajifunika na wanalala.

FADE OUT.

Hivyo ndivyo skripti ya filamu inavyotakiwa

kuandikwa.

(viii) Baada ya kukamilisha yanayohitajika katika

onesho hilo, inapaswa kuandika aina ya

ifekti (effect) ambayo mtunzi atapenda

itumike katika uhariri wa kazi. Zipo aina

nyingi za ifekti kama vile: waipu (wipe),

suparimpozi (superimpose), fedi ini (fade in),

fedi auti (fade out), na kukata (cut).

Maelekezo hayo huandikwa mwishoni

mwa maelekezo ya onesho katika

upande wa kulia wa karatasi.

(ix) Wakati wa upigaji wa picha kunahitajika vitu

muhimu ambavyo vitawezesha onesho

kutokea kama alivyokusudia mwandishi.

Kuna suala la mavazi ya wahusika ambapo

kila mhusika anapaswa kuvaa kulingana na

uhusika wake. Bila shaka mtu wa mavazi

atapaswa kushughulikia jambo hili. Kwa

utaratibu, kila kazi inapaswa kufanywa na

mtu tofauti ili aweze kupata ushauri kutoka

kwa wenzake wa namna ya kuboresha kazi

yake. Mathalani mtu wa mavazi anapaswa

kufanya kazi kwa kushirikiana na

mwongozaji na vilevile na mtu wa mwanga ili

kuleta hisia iliyotarajiwa na mtunzi. Hapa

nyumbani filamu nyingi zinatobangwa kwa

kuwa unakuta kila kazi imefanywa na mtu

yuleyule - mtu anakuwa na vyeo zaidi ya

viwili- hii sio taaluma. Maadamu wasanii

wameamua kujiingiza katika fani hii, ni

lazima wafuate weledi wa taaluma yenyewe

ili kutoa kazi bora na sio bora kazi. Kama

wasanii hawatabadilika kazi zao zitazidi

kudoda kwa kuwa ni nani atakubali kuitupa

pesa yake kwa kununua kitu kilicho chini ya

kiwango? Bila shaka hakuna! Jambo hili

litaendelea kuwafanya wapenzi wa sanaa

waendelee kuvutiwa na filamu za Hollywood,

India, Japani, China, Nijeria, na kwingineko.

(x) Matumizi ya taa za mianga na riflekta

(reflector) ni muhimu ili kupata picha

inayofanania uhalisia wa maisha. Matumizi

ya reflekta yasiwe bila sababu kwani

yakifanywa bila utambuzi wa tahadhali hii -

huleteleza kazi chapya ambayo hakuna mtu

atavumilia kuitazama. Mathalani kuna kazi

moja niliwahi kuitazama ya hapa nyumbani

ambapo taa za mianga na reflekta zilitumika

vibaya na hivyo kuifanya picha nzima kuwa

nyekundu utafikiri watu wamepakwa damu,

nyumba zao zimepakwa damu, kila kitu

wanachokishika kimepakwa damu. Haifai

kufanya mambo bila kuwa na utaalamu - ni

jambo bora na la busara wasanii wakatumia

wataalamu katika maswala ya sanaa ili

waweze kutoa kazi zitakazo washika

watazamaji na hivyo kujijengea heshima

kama walivyojijengea wasanii na waongozaji

wa filamu za Kimarekani; na mahali

kwingineko ambako watu hawafanyi kazi

kwa vipaji tu - bali wameongezea na taaluma

kidogo. Kwa hiyo kunawafanya watoe kazi

bora.

(ix) Baada ya shughuli hiyo kuisha, inafuata

kazi ya studio ambayo itakuwa ni kuhariri

picha na kuingiza sauti zinazoshadidia

matukio mbalimbali pamoja na miziki ili

uundwaji wa matukio uweze kuleta hisia

na kuwashika watazamaji. Hapa zoezi la

kuhariri linafanywa na mhariri

akishirikiana na mwongozaji wa filamu ili

kuweza kufikia muafaka wa namna gani

onesho liwe. Matumizi ya efekti

mbalimbali hutawala katika hatua hii.

(x) Maswala mengine ya kiufundi

yanahusiana na mpangilio wa vitu mbele

ya kamera (katika jicho la kamera) ili

hatimaye tuweze kuona jinsi vitu

vilivyopangwa. Kwa Kiingereza jambo hili

linaitwa “mise en scene” ikimaanisha ‘kitu

gani kinawekwa wapi’, nini kinakaa

kushoto, kulia, katikati, juu, chini, na

kadhalika. Ni kama vile mwongozaji wa

michezo ya jukwaani anavyowapanga

wahusika wake na vifaa mbalimbali

vinavyomsaidia mwigizaji akiwa jukwaani.

Jambo la msingi na la kukumbuka ni

kuwa, kile kinachowekwa katikati ndicho

kinaonekana kina maana na kinawavutia

watazamaji na lazima mwongozaji wa

filamu au mchezo wa jukwaani azingatie

hilo. Kinachowekwa pembeni hakiyavutii

macho ya mtazamaji na kinaonekana

kuwa hakina umuhimu; na ikitokea, kuna

jambo linafanywa na mhusika aliye

pembezoni – ndipo hadhira itamtazama.

Pia kitu kingine ni kuzingatia ufuatiliaji wa

waigizaji wanakotazama na hadhira

itataka kutazama huko. Kwa hiyo, kama

mhusika anaonekana akielekeza macho

yake upande wa kulia – lazima kuna kitu

anakiangalia; kwa hiyo na watazamaji

tunataka kuona anachokiangalia

mwigizaji (mhusika). Kwa hiyo ikitokea

mwigizaji anatazama pembeni lakini

hakuna kitu tunachoweza kukiona, yaani

hadhira inatazama na hakuna

kitazwamacho – basi hapo sanaa

imeshindwa kufikia ubora wake

unaotakiwa. Wasanii wajifunze kwa

kuangalia kazi za wasanii wa Hollywood

na kwingineko ambako walianza

kujishughulisha na sanaa ya uigizaji kwa

karne nyingi.

(xi) Kitu kingine cha kuzingatia ni urefushaji

wa matukio bila sababu ya msingi. Katika

filamu, matukio yanapaswa kuoneshwa

kwa sekunde chache tu kama urefu wake

hauna mchango katika uendelezaji wa

hadithi. Kila urefushaji wa tukio uwe na

sababu zake katika mwendelezo wa

hadithi. Hili si tatizo kwa filamu za

wenzetu wa majuu ambao ni wabobevu

katika uwanja huu – hili ni tatizo huku

kwetu ambako watengenezaji wa filamu

wanarefusha matukio bila sababu

maalumu. Lazima kila urefu wa tukio

uhusike katika mwendelezo wa hadithi.

Mara nyingi utaona kwenye filamu zetu

mhusika anaonekana akiingia ndani ya

gari na gari lile linaondoka, tunaoneshwa

linavyokwenda zaidi ya dakika kumi – bila

kuwa na msingi wowote. Lazima kama

kuna kuoneshwa linavyokwenda kuwe na

mwendelezo wa hadithi la si kuonesha tu

ili mradi kuonesha.

(xii) Matumizi ya vifaa mbalimbali lazima

yawe na sababu. Mara nyingi katika

filamu zetu au hata michezo ya kuigiza

ya kwenye televisheni au jukwaani,

utamwona mhusika amebeba kifaa fulani,

lakini kifaa hicho hakina uhusiano

wowote na hadithi. Jambo hili halifai.

Mathalani, katika sanaa za wenzetu huko

majuu, ukimwona mhusika ameshika

kifaa labda tuseme ‘kisu’, basi kisu hicho

kinasimulizi katika hadithi. Labda

kitatumika kujeruhi mtu, au tukiona kisu

kina damu baadaye tukaoneshwa mtu

aliyechinjwa – basi hapo matumizi ya

kifaa hicho yanakuwa na mantiki. Hapa

nyumbani mambo ni tofauti, na hii bila

ubishi wowote inatokana na kutoelewa

kuwa kila kitu kishikwacho na mhusika

lazima kiwe na kazi. Mathalani tumewahi

kuona katika michezo ya televisheni,

mhusika amevaa manati kubwa shingoni,

au anaishika kila aendapo, lakini haina

matumizi. Au unaweza kuona mhusika

amebeba kikuyu na kila mahali

anakwenda nacho kakibeba tu, na hakina

matumizi. Kama mhusika huyu

angejengwa kuwa ni kichaa, ambaye

anajiokotea vitu na kuvibeba, hapo

isingeleta maswali. Lakini si mhusika

kichaa, ni mtu na akili zake timamu, lakini

anashika kifaa na kutembea nacho kila

mahali- hii haifai na siyo sahihi.

(xiii) Matumizi ya rangi za mavazi au maua na

hata vifaa mbalimbali pamoja na

mandhari nzima lazima visaidie katika

kuelezea maudhui ya kazi. Lazima fani

itumike kujenga maudhui. Kwa wenzetu

hili si tatizo kwa kuwa wanaelewa mambo

haya na hawafanyi kwa kubahatisha.

Utakuwa kuna wahusika wamebeba

dhamira ya mapenzi na wamevalishwa

mavazi meusi – hii maana yake nini?

Lazima rangi za mavazi zishadidie

maudhui. Katika sanaa, rangi zina maana

zake. Kwa mfano, rangi nyeusi

zinafungamana na maovu, dhambi, au

matendo mabaya, na ufisadi kwa ujumla.

Rangi nyeupe inafungamana na wema,

usafi wa moyo au utakatifu. Rangi ya

njano inafungamana na wivu wa

kimapenzi. Rangi nyekundu

inafungamana na mapenzi kati ya

wapendanao na ndio maana siku ya

wapendanao inatawala vazi jekundu.

Rangi ya zambarau inafungamana na

masuala yanayohuzunisha na ndio

maana katika baadhi ya makanisa – siku

ya ijumaa kuu, ambayo ni ya mateso ya

Bwana Yesu rangi za dhambarau

hutawala katika mavazi ya wachungaji,

watumishi na pia vitambaa

vinavyotandikwa altareni.

(xiv) Matumizi ya muziki au mapigo fulani

ambayo yanaleta ridhimu lazima

yafanywe kwa uangalifu mkubwa na pia

yanapaswa yaendane na dhamira

inayoibushwa. Katika kazi za wenzetu

udhaifu huu huwezi kukutana nao; ila

katika kazi zetu udhaifu upo. Unakuta

kuna tukio la hatari, labda kuna mtu

anaviziwa ili auawe, lakini unakuta

mapigo ya hatari hayasikiki bali

yanasikika ni kama yale yanayoendana

na mahaba – yaani mapigo ya polepole,

mazuri yanayovutia na kuleta uzuri fulani,

mapigo laini – hili ni tatizo. Mapigo

yanayoashiria hatari huwa ni makali

yasiyo ya kawaida, ya haraka haraka, na

ya kushitua. Na kinyume chake unaweza

kuoneshwa wahusika wako katika

mahaba, na muziki unaopigwa ni ule usio

mwololo yaani mziki mkali unaofaa

kwenye kipindi kilichochangamka kama

cha michezo au harakati. Hili ni kosa,

muziki unaofungamana na masuala ya

mapenzi na mahaba lazima uwe mwololo

ili kushadidia dhamira hiyo. Siyo kupiga

muziki kwa ajili ya kupiga tu- hapana, kila

pigo au ridhimu lazima iwe na maana na

mchango katika kuendeleza dhamira.

(xv) Matumizi ya bakigraundi (mahali pa

nyuma kama sehemu ya picha au

sanamu panapotumika kushadidia

mandhari ya onesho) lazima yawe na

maana katika kuibua maudhui. Utakuta

picha imepigwa na kwenye bakigraundi

kuna mandhari fulani inayoonekana.

Lazima bakigraundi hiyo isadifu dhamira

inayokusudiwa. Mathalani, katika nyimbo

mbalimbali za Injili hapa Tanzania,

utakuta mwimbaji anaimba na nyuma

yake tunaiona bahari. Lakini , je, bahari

hii inayoonekana kwenye bakigraundi ina

maana yoyote katika kuibua ujumbe

unaoimbwa? Wakati mwingine, utakuta

mwimbaji ameingia ndani ya maji – labda

baharini, lakini anachokiimba hakina

uhusiano kabisa na maeneo aliyopo; au

utakuta mwimbaji anagaragara kwenye

tope akiimba kuhusiana na jambo la

furaha na sio majuto na maombolezo –

hii haifai. Lazima sanaa ifanywe kwa

viwango vinavyotakiwa. Ni bora wasanii

wetu wakajifunza kwa kuangalia kazi za

wenzao wa Hollywood na kwingineko

ambao ni wakongwe katika uwanja huu,

ili wajue nini wanapaswa kufanya na wapi

wakifanye.

(xvi) Kitu kingine cha kuzingatia ni namna ya

uchezaji na kuendana na mapigo katika

miziki ya Injili ambayo tunaiona kwenye

televisheni. Wachezaji wanaiga namna

ya uchezaji bila kufanya mazoezi ya kina

ambayo yatawawezesha kuendana na

mapigo ya muziki. Nasema hili kwa

uchungu kabisa baada ya kuangalia kazi

ya baadhi ya wasanii wa muziki wa Injili

ambao wanaiga uchezaji wa Rose

Muhando lakini wanashindwa kuendana

na mapigo ya ngoma na hivyo

kuonekana kichekesho. Haifai kuiga, ni

vema kila mwanamuziki wa Injili

akamtafuta mtaalamu wa muziki ambaye

atamshauri namna ya uchezaji kuendana

na mapigo ya wimbo na maudhui yake.

Utaweza kuona wachezaji wa nyimbo

wanaimba wimbo wa polepole lakini

wanacheza kwa haraka na kurukaruka

kama Rose Muhando; au wanaimba

harakaharaka na wanacheza kwa

mwendo wa pole. Huu ni ukiushi na

ukengeushi – haipaswi kufanya hivyo! Ni

lazima kuendana na maadili ya sanaa hii

ya vielelezo (yaani runinga na filamu)

kama ambavyo kanuni na kaida zake

zimejengwa katika nadharia hizo za

uigizaji. Kila mdundo au ridhimu iendane

na mwendo na mapigo ya muziki au

wimbo; na vilevile yaendane na uchezaji.

3.4 Hitimisho

Filamu ni sanaa inayopendwa na watu wengi

duniani. Jambo hili lina ushahidi kutokana na watu

kutazama hata filamu wasizoelewa ‘ulimi’ wake

(lugha inayotumika), lakini wanajitahidi kupata

ujumbe kupitia picha za mwendoni. Wasanii wetu

wajitahidi ili sanaa zao zibebe utamaduni wetu na

zivutie hata watu wengine ambao hawaelewi

Kiingereza wala Kiswahili, ila mvuto tu wa filamu

yenyewe inawafanya waipende na kuifuatilia.

 

 

 

 

 

SURA YA NNE

UANDISHI WA MISWADA YA REDIO

Usuli wake

4.0 Utangulizi:

Kwa mujibu wa Moshiro (1979:1) anaelezea

mchezo wa redio kuwa ni:

Ni igizo lifanyikalo redioni, ambalo wahusika

wake hutumia sauti zozote zilizo katika

mazingira yahusikanayo na mchezo huo ili

kutoa picha ya kile kielezwacho. Sauti hizo ni

maneno ya wahusika, zile zitokanazo na

vitendo vya wahusika na nyingine zozote za

asili zinazoyasanifu mazingira yahusikayo.

Katika michezo hii mara nyingi muziki

hutumika kama kielelezo cha ziada.

Kulingana na fasili hiyo ya Moshiro

kuhusiana na mchezo wa redio, tunaweza

kudondoa mambo ya msingi aliyoyataja ambayo ni:

igizo linalofanyika redioni - ina maana msikilizaji

atasikiliza kinachoigizwa ambacho kinapaswa

kimpe picha katika akili yake. Pili, ameelezea

wahusika hutumia sauti mbalimbali ili kukamilisha

dhana ya uhusika wao - sauti hizi zinaweza kuwa

milio ya vitu, ndege, wanyama, au sauti za

binadamu zinazoelezea hisia mbalimbali kama

kulia, kucheka, kusonya, na kadhalika au maneno

wayaongeayo.

Tatu, ametaja muziki - ambao unaweza

kutumika ili kutambulisha mandhari ya mchezo, au

wakati mwingine hutumika kusindikiza dhamira

fulani. Maana ya mchezo wa redio kama

ilivyoelezwa na Moshiro tunaikubali na hivyo

itatumika bila maboresho ya aina yoyote.

Moshiro anaendelea kuelezea hatua za

uandishi wa mchezo wa redio ambao ni pamoja na:

kwanza inatakiwa uitunge hadithi. Hadithi hii

inapaswa ichukuliwe katika maisha ya mahali fulani

na wakati fulani, kisha ifinyangwe kisanaa ili

kumwezesha msomaji au msikilizaji aione katika

fikara. Kwa mfano, hadithi kuhusu kijana wa kiume

kuchaguliwa mke wa kuoa.

Hatua ya pili ni uundaji wa migongano.

Inabidi ufikirie kisa chako kitakuwa na migongano

ya aina gani. Mathalani, tuchukulie mfano wa

msichana na mvulana wanakuwa na mahusiano ya

mapenzi kabla ya ndoa, siku moja baba wa

msichana anawafuma na kuwafungisha ndoa ya

mkeka. Sasa unda migongano kwa mkasa huu.

Hatua ya tatu ni kuupangilia mtiririko wa kisa chako

katika hadithi. Mwandishi anapaswa aamue kuwa

anataka aianze hadithi yake moja kwa moja au

atumie muundo wa kioo. Ni uamuzi wa mwandishi

mwenyewe. Hatua ya mwisho ni uandishi wa

mchezo wa redio ambao kaida zake zitaelezwa

katika sehemu ifuatayo.

4.1 Uandishi wake

Uandishi wa mchezo wa redio kwa mujibu wa

Moshiro unapaswa uwe na vitu vitano ambavyo ni:

kwanza, kuna usimulizi anauelezea kwa namna

mbili: kwanza ni msimulizi ambaye anaitambulisha

hadithi; na pili, ni mazungumzo ya wahusika

wanapowasiliana.

Pili, anazungumzia suala la uzungumzaji

kwamba, katika maisha ya kila siku, watu

wanaanza kuongea jambo moja na kisha wanarukia

jingine. Katika mchezo wa redio, sikio la msikilizaji

haliwezi kusikiliza kwa muda mrefu, hivyo inatakiwa

mazungumzo yawe haraka haraka, na ya

kueleweka kwa urahisi, licha ya kisa chenyewe

kuwa cha kusisimua.

Tatu, anazungumzia hulka kwamba, kila

binadamu ana tabia na hulka tofauti na mwingine.

Hivyo, wahusika katika mchezo wa redio hawana

budi kutofautiana hulka na tabia zao.

Nne, anazungumzia wahusika kuwa

hawatakiwi wawe wengi kwasababu

watambabaisha msikilizaji hata asijue nani ni nani

katika igizo hilo. Pia anaelezea kuwa majina ya

wahusika yatajwe mara kwa mara hasa mwanzo

wa mandhari yoyote; na pia anamzungumzia

mhusika ambaye hasemi lolote na kuwepo kwake

mahali hapo ni muhimu, mhusika huyu hana budi

kutajwa jina lake mara kwa mara ili msomaji

asimpoteze.

Mwisho ni sehemu ya mchezo, kwamba kila

mara msikilizaji anaposikia maongezi katika

mchezo, huwa kwanza anakisia mahali ambapo

wahusika wako kutokana na sauti au milio

atakayoisikia2.

Moshiro katika ukurasa wa 4-7 anaongezea

‘namna ya kuandika mchezo wa redio’ lakini

anachokifanya hakimsaidii mwandishi chipukizi kwa

sababu, anataja na kuelezea vitu muhimu

vinavyotakiwa ili uweze kuuandika mchezo wa

redio; lakini namna ya kuuandika hakuielezea.

Japokuwa ameandika mchezo wa Kusadikika

katika umbo la mchezo wa redio, lakini jambo hili

halimsaidii mwanafunzi kupata 'abc' za utunzi. Sisi

tutadokeza namna ambayo mwanafunzi wa

uandishi wa mchezo wa redio, ataitumia ili aweze

kuipangilia kazi yake, iwe ya mchezo wa redio.

Pamoja na kuzingatia vitu vitano alivyovitaja

Moshiro.

4.2 Mchezo wa redio:

Mchezo wa redio unatumia mlango wa fahamu wa

kusikia (masikio) ambao unapaswa umwezeshe

msikilizaji kuona, kuonja, kunusa, na kugusa.

Msikilizaji anapaswa akutanishwe na milango

mingine ya fahamu kupitia katika masikio yake.

2Moshiro Gervas, 1979, Michezo ya Kuigiza-10. Mchezo wa Redio

Kusadikika uk 1-7 . Tanzania Publishing House

Mchezo wa redio unatawaliwa na maneno mengi

ambayo yanakusudia kuelezea matendo mbalimbali

ili msikilizaji aweze kuona, kunusa, kuonja, kuhisi,

kupitia katika kusikia.

Kwa mfano, mazungumzo kati ya wahusika

wa mchezo wa redio yanapaswa yampatie

msikilizaji fursa ya kuona ‘akilini’ kinachoendelea;

na vilevile maelekezo ya msimulizi ambayo

yanaandikwa kwa hati ya kawaida na ambayo

msimulizi anayasema yanatakiwa pia yasaidie

kuipata picha halisi ya mandhari. Pia kuna

maelekezo ambayo yameandikwa kwa hati ya

mlazo haya yana kazi maalumu. Kazi ya maelekezo

haya ni kumwezesha mhusika (mwigizaji au

msimulizi) ili aingie kwenye uhusika wake. Ni

maelekezo ya jukwaani kama yalivyo kwenye

tamthiliya.

4.3 Ufundi wa fani:

1. Uwasilishaji wa mchezo wa redio una vipengele

vya kuzingatia ambavyo ni pamoja na:

(a) Wahusika kutofautishwa sauti zao ili ijenge

ukubalifu na kuaminika. Mathalani kusiwe na

wahusika ambao sauti zao zinafanana au

zinaelekeana. Mfano ni mchezo mmoja wa redio

ambao ulikuwa unarushwa na Redio ya Deusche

Welle huko mjini Borne nchini Ujerumani

unaojulikana kama Tega Sikio Jenga Maisha

yako.

Ulipokuwa unaanza mchezo huu mwaka

2008, kulikuwa na wahusika wawili ambao ni mama

na mtoto, wahusika hawa walikuwa wote na sauti

nyembamba ambazo zinafanana kabisa na hakuna

namna yoyote inayomwezesha msikilizaji

kuwatofautisha na kuona ni watu wawili tofauti.

Ilikuwa ni vigumu kukubali kuwa ni wahusika wawili

au ni mmoja ambaye anatamka maneno ya

wahusika wawili (ambao ni mama na hapo hapo ni

mtoto). Huu ni udhaifu, haijalishi kuwa ukweli

ulikuwaje lakini kinachopaswa ni kuwatofautisha

wahusika ili sauti zao zisifanane na kuwawezesha

wasikilizaji kuwaona wahusika wawili wenye haiba

toifauti. Ni vema umri pia ukazingatiwa katika

kuteua wahusika. Yaani kama kuna mama na

mtoto, au mzee na kijana, au mwanamke na

mwanaume. Lazima sauti za watu hawa

zitofautiane kwa kuwa msikilizaji hawaoni kwa

macho bali ni kwa masikio, hivyo inapaswa

awezeshwe kuwaona watu hawa kupitia katika

masikio yake. Jambo hili linawezekana kwenye

usaili ambapo mkurugenzi atachagua

wahusika/waigizaji kulingana na umri, sauti n.k.

(b) Uandishi wake hautofautiani sana na ule wa

tamthiliya ila tofauti inakuja kwenye maelekezo ya

matendo mbalimbali. Katika mchezo wa redio,

maelekezo husomwa na mtu anayeitwa msimulizi

ambaye naye sauti yake lazima itofautishwe. Na

jinsi sauti yake ilivyo na anavyozungumza, laziwe

iwe katika nadharia hiyo ya kusimulia na sio

kuzungumza. Msimulizi anatakiwa asimulie na

msikilizaji aone kuwa ‘anasimulia’. Kinyume cha

maelekezo haya ya mchezo wa redio tunakiona

katika maelekezo ya tamthiliya ambako, maelekezo

haya humsaidia mhusika kuingia katika uhusika bila

maelekezo hayo kuyataja. Umeelewa?

(c) Utendekaji wa matukio mbalimbali

hutegemea sauti ambazo humwezesha msikilizaji

kuipata picha na hivyo kujiona anakiona kila kitendo

kinachofanywa na wahusika. Kwa mfano ni tukio

linalohusu mgeni kufika katika katika nyumba fulani.

Lazima isikike sauti ya mtu anayetembea, kisha

tusikie mlango ukigongwa, halafu tusikie mtu

akiitikia ‘karibu’ na kisha kusikia sauti ya mlango

unapofunguliwa, na kisha maongezi ya hao watu

wawili ambao wamekutana. Watasalimiana kwa

kutajana majina ili wasikilizaji wawaone kupitia

‘macho ya masikioni’.

(d) Msimulizi ndio kiungo cha matukio yote

yanayotendeka hasa ubadilishaji wa mandhari na

uongezekaji wa wahusika wapya. Msimulizi

anapaswa atuambie kuwa wahusika wako kwenye

mandhari gani, na mwonekano wa mandhari hiyo

ukoje. Kwa mfano, msimulizi akituambia kwamba,

tuko pwani na kuna mawimbi makali ya bahari.

Tutatarajia tusikie mvumo wa mawimbi hayo ukiwa

ni mkubwa au mdogo; na vikorombwezo vingine

vinavyofanya ukubalifu na uaminikaji wa masimulizi

yake, kuhusiana na anachotuambia. Sio atuambie

tuko katika mandhari ya ufukwe wa bichi mojawapo

halafu tuanze kusikia kelele za ng’ombe au kuku

wakiwika, hapana! Huu utakuwa ni uongo mkubwa!

(e) Kila mhusika anayezungumza hupaswa

kutaja jina la yule anayezungumza naye ili

kumfanya msikilizaji asipotezwe kwa kushindwa

kufuatilia na kujua ni nani anayezungumza. Kwa

hiyo, kuwe na namna ya kuwataja wahusika katika

mazungumzo yao; na vile vile msimulizi huifanya

kazi hii kama ni mhusika mpya anaingia katika

tukio. Yaani anaposema ‘x’ anakwenda nyumbani

kwa ‘y’ na kisha ndipo aendelee na simulizi. Au

mhusika mwenyewe anaweza kulitaja jina la

mhusika mwenzake wakati wa mazungumzo yao.

(f) Mandhari hutofautishwa na kutambulishwa

kupitia katika sauti zinazopatikana katika mandhari

hizo. Jambo hili ni kama tulivyoligusia katika

kipengele ‘d’. Lakini kutokana na umuhimu wake –

tutalijadili tena hapa kwakuwa ndio ‘moyo na uti wa

mgongo’ wa mchezo wa redioni. Tutatoa mifano

mbalimbali ili mada hii iweze kueleweka. Kwa

mfano, katika mandhari ya msituni - bila shaka sauti

za ndege hazitakosa kusikika. Au kama mandhari

ya katikati ya jiji hapa Dar es Salaam kwenye kituo

cha mabasi ya Daladala - kelele za wapiga debe na

milio ya honi na mingurumo ya magari haitakosa

kusikika na kadhalika. Mambo yote haya

humjengea msikilizaji picha ya mandhari na

kumfanya aone kila kinachoendelea.

Tutatoa mfano wa kuandika mchezo wa redio kama

ifuatavyo:

Msimulizi: Ni mchana wa jua kali siku ambayo

Tuma alikwenda kazini akiwa

amevalia suruali nyeusi, shati jeupe,

viatu vyeusi, na koti jeusi ambalo

alilivua baada ya kujihisi joto na

kulishika mkononi. Tuma anapofika

mlangoni, anagonga mlango na

kusubiri kidogo. Sauti inasikika ikiitikia

“karibu” na mlango unafunguliwa.

Beti: Karibu Tuma wangu. Pole sana kwa kazi.

Tuma: Asante Beti wangu. Habari za hapa?

Beti: Nzuri tu, habari za kazi?

Tuma: Safi tu.

Msimulizi: Baada ya Beti kumkaribisha Tuma na

kumpokea koti aliloshika mkononi, Tuma

anajitupa kochini na anachukua rimoti ya

kiyoyozi anawasha kiyoyozi. Anajifungua

vifungo vya shati lake na kisha

anajiegemeza kochini. Mara anachukua

rimoti ya runinga na anaiwasha na kutafuta

stesheni mojawapo.

Tuma: Nataka kuangalia taarifa ya habari.

Beti: (Anacheka Kidogo) He! Babu wewe, taarifa

ya habari mchana wote huu inatoka wapi?

Tuma: (Akionesha kukata tamaa) Ah! Nilidhani

kuna taarifa ya habari muda huu…

Beti: Kweli dunia imekupita. Taarifa ya habari

mchana huu?

Tuma: Nitalijulia wapi hilo bibi wewe wakati kila siku

mimi ni kiguu na njia?

Beti: Subiri saa moja au saa mbili usiku ndio kuna

taarifa.

Tuma: Basi naenda kujipumzisha kidogo. (Anapiga

mwayo) Maana nimechoka kweli.

Beti: Nakutakia njozi njema babu wewe.

Msimulizi: Tuma anakwenda kulala (sauti ya nyayo

za mtu anayetembea harakaharaka

zinasikika na mlango unafunguliwa na

kufungwa) na Beti anaendelea kutazama

runinga.

Muziki: (kunasikika muziki wa ala au wa taratibu

ukipigwa).

Pili, hatua inayofuata baada ya kuandika

mswada ni kuutengeneza ili uweze kurushwa

redioni. Moshiro katika ukurasa wa 9-13 anaelezea

namna ya utayarishaji wa mchezo wa redio

ambapo mwongozaji baada ya kuwasaili waigizaji

na kuwagawia husika zao, hutakiwa mwongozaji na

waigizaji wake kuusoma mswada wote na

kuuelewa. Kisha, mwigizaji mmojammoja anasoma

sehemu yake anayoiigiza na kuelewa uhusika wa

kila mmoja. Mazoezi hufuata ambayo hufanyika bila

kurekodiwa. Mwongozaji anaporidhika na mazoezi

yanayoendelea, zoezi la kurekodi onyesho moja

baada ya jingine hufuatia.

Kitu kingine alichokielezea Moshiro ni

nidhamu ya waigizaji ambayo inapaswa iwe ya hali

ya juu kwa kuwa, bila nidhamu kazi ya kuigiza

redioni itakuwa ni ngumu na sio rahisi.

4.4 Hitimisho

Sanaa ya uigizaji ina kaida na miiko yake kama

tulivyoona katika uandikaji na utengenezaji wa

mchezo wa redio. Jambo la msingi kwa mwigizaji

na mwongozaji ni kuwa na ushirikiano wa hali ya

juu ili kinachopendekezwa kufanywa, kiweze

kufanyika kwa usahihi. Kazi hii itawezekana kama

nidhamu ya kuwahi mazoezini itazingatiwa na

nidhamu kwa ujumla wake.

Jambo jingine kwa mwigizaji ni kufanya

utafiti ili aweze kuujua ‘uhusika’ anaouigiza. Kwa

kuujua uhusika kwa undani, itamwia rahisi mwigizaji

kuigiza kwa umahiri mkubwa.

SURA YA TANO

UANDISHI WA MISWADA YA TAMTHILIYA

Usuli wake

5.0 Tamthiliya

Tamthiliya ni andiko la kiuigizaji ambalo hutumia

wahusika wanaojibizana au wanaozungumza peke

yao ili kuwasilisha ujumbe wa mwandishi.

Tamthiliya ina mpangilio wake katika msuko wa

matukio ambao una sehemu tatu: mwanzo, kati, na

mwisho. Msuko huu ni muhimu kwa kuwa

unawezesha kujua kisa kilivyoanza, kinavyokua, na

kinavyohitimishwa. Katika sehemu ya mwanzo

ndipo utambulisho wa wahusika hufanyika na ni

sehemu ambayo wahusika huanza kukutana na

kuhusiana ili kujenga migogoro inayoaminika.

Katika sehemu ya kati, hapo ndipo kuna

kuwa na mgogoro au kutofautiana kwa mielekeo

ambako kunasababisha malumbano na hatimaye

mchezo unabadili mwelekeo, hicho kinaitwa kilele

au taharuki.

Sehemu ya mwisho wa mchezo ni pale

penye mshuko wa matukio. Katika sehemu

migogoro iliyokuwa ikifukuta inatatuliwa na

kuhitimishwa. Huo ni msuko wa kawaida ambao

unapatikana katika tanzu zote tatu za tamthiliya,

filamu, na michezo ya redio. (Aristotle; Semzaba).

5.1 Uandikaji wake:

Uandishi wa mswada wa tamthiliya una namna

yake inaoutofautisha na mswada wa filamu na

redio. Tutachunguza vipengele kadhaa vifuatavyo:

a) Kuna maelekezo kwa mwongozaji au

msomaji yanayomsaidia kuipata picha halisi ya

tukio linaloandamana na majibizano ya wahusika.

Maelekezo haya (stage directions) yanatakiwa

yawe katika hati ya mlalo na kwenye mabano.

Maelekezo haya yanatakiwa kuonekana mwanzoni

kabla ya kitendo husika hakijafanyika na sio baada

ya hapo. Mathalani unataka mhusika wako acheke

kabla hajaongea neno, itakubidi maelekezo hayo ya

kucheka yaje mwanzoni na ndipo acheke. Mfano

ukisema (Beti anacheka na kisha anamtazama

Tuma na kusema) Nakupenda laazizi!

b) Maneno ya wahusika yanapaswa kuwa

katika hati ya kawaida ambayo siyo ya mlalo.

Majibizano haya yanafuata baada ya kutaja jina la

mhusika.

c) Majina ya wahusika yanaandikwa upande

wa kushoto wa karatasi (au tuseme mwanzo wa

ukurasa) na kisha maneno ya mhusika yatafuata

mbele ya jina lake.

d) Nukta pacha - hizi hutumika katika

kutenganisha jina la mhusika na maneno yake

anayoyatamka.

e) Majibizano ya wahusika yanapaswa kufuata

mara tu baada ya kuandika nukta pacha.

f) Onesho linaweza kuwa na sehemu au lisiwe

nazo. Likiwa na sehemu inabidi sehemu hizi

zijengwe kwa mfuatano unaoleta mantiki katika

ujenzi wa kisa au tukio. Wakati mwingine,

baadhi ya wasanii huliita onesho - kitendo; vilevile

kitendo kinaweza kuwa na sehemu au la. Kikiwa na

sehemu kifuate utaratibu kama tulivyoeleza hapo

juu. Kwa hiyo, unaweza kuwa na onesho la kwanza

lenye sehemu tatu ambazo ni: sehemu ya kwanza;

sehemu ya pilil; na sehemu ya tatu. Tutatoa

mfano wa kuandika mswada wa tamthiliya katika

ukurasa unaofuata.

5.2 Ufundi kuhusu fani

Ufundi huu hujumuisha mambo mengi pamoja na

mambo muhimu ya kumalizia shughuli nzima ya

kuubadili mswada ili uwe kitabu.

a) Jalada la tamthiliya litakuwa na jina la kitabu

ambalo linapaswa libuniwe kisanaa ili liweze

kujenga hamu ya msomaji kukinunua na kukisoma.

Jina lazima liwe na mvuto.

b) Rangi za jalada lazima zielekeane na

dhamira kuu inayojengwa katika kitabu. Rangi hizi

zinapaswa kutumika kwa malengo maalumu na sio

kinyume chake. Japokuwa wakati mwingine

mwandishi huchagua rangi kutokana na mvuto

wake na siyo maudhui! Mathalani katika uwanja wa

sanaa, rangi zina maana yake na matumizi yake

yanapaswa kutiliwa maanani. Rangi ya njano

inabeba dhamira ya wivu na ndio maana hata

katika filamu kukiwa na mhusika ana wivu kwa

mpenzi wake anaweza kumpa ua la rangi ya

manjano au anaweza kuvalia nguo za rangi hiyo.

Rangi nyekundu inafungamana na mapenzi

na ndio maana kuna kupeana maua mekundu au

kuvalia nguo nyekundu. Rangi nyeupe

inafungamana na utakatifu, usafi wa moyo, na

tabia. Rangi nyeusi inafungamana na uovu na

uchafu wa moyo na uasi. Haya yote ni katika

muktadha wa sana aza maonesho

Rangi ya buluu hasa ikiwa inatumika katika

chumba huleta mandhari ya kimahaba katika

chumba husika. Kwa hiyo, kila rangi ina maana

yake katika uwanja wa sanaa na haipaswi

kuzitumia mchafukoge. Kwa mfano, kama

tamthiliya inahusu maasi, uovu, na uchafu wa moyo

- rangi za jalida hazipaswi kuwa nyeupe kwani kwa

kufanya hivyo, itatathminiwa kuwa msanii

ameshindwa kutumia weledi wake. Au kama ni kwa

makusudi maalumu ya kuonesha ukinyume - ni

lazima isemwe tangu mwanzoni ili kazi itathminiwe

kwa haki.

(c) Kuna maelezo ya ndani kabla ya kufikia penye

tamthiliya yenyewe. Maelezo haya ni pamoja na:

ukurasa wa haki miliki ya mwandishi au

mchapishaji ikiambatana na mwaka

kilipochapishwa kitabu na kampuni ya uchapishaji

iliyohusika. Vilevile kuna ukurasa wa dibaji,

shukrani, utangulizi, na yaliyomo. Kipengele hiki

kinaweza kuandikwa mwisho mara baada ya

kuikamilisha tamthiliya yako.

d) Nyuma ya kitabu kunakuwa na blabu. Blabu ni

maelezo mafupi kuhusiana na wasifu wa mwandishi

na muhtasari wa kazi yake ambao utamfanya

mnunuaji wa kitabu avutiwe na kukinunua. Watu

wengine huweka maoni ya baadhi ya wasomaji

kuhusiana na kazi hiyo ambayo kwa pamoja

huongeza mvuto kwa mnunuaji wa kitabu, na

kupata hamu ya kukisoma.

5.3 Uwasilishaji wake:

Tamthiliya ni kazi inayokusudiwa kutendwa

jukwaani kwa hiyo maneno au majibizano ya

wahusika yalenge utendekaji na sio mahubiri.

(a) Tamthiliya haihitaji maneno mengi kama

mchezo wa redio kwa kuwa watu wanatazama kwa

macho yao na wanasikia maneno ya waigizaji. Kwa

hiyo hapo tunapata tofauti ya kazi hizi mbili. Kwa

mfano una wahusika wawili ambao ni wapenzi -

hebu tuangalie uwasilishaji huu:

(i) Beti: (Tuma anafungua mlango na mkononi

ameshika kofia lake, anaingia sebuleni.

Anamkuta Beti anaangalia runinga. Beti

ananyanyuka anampokea kofia Tuma na

analiweka mezani) Karibu laazizi.

Tuma: Asante asali wangu. (Anaketi.

Wanatazamana). Habari za hapa?

Beti: Nzuri tu, za kazi?

Tuma: Safi.

Hebu angalia uwasilishaji mwingine huu hapa chini

kati ya Beti na Tuma.

(ii)Beti:(Tuma anafungua mlango, mkononi

ameshika kofia lake, anaingia sebuleni.

Anamkuta Beti anaangalia runinga. Beti

ananyanyuka na kumpokea kofia Tuma na

kuliweka mezani). Hebu nikupokee hili kofia

lako na niliweke hapa mezani. Karibu laazizi.

Tuma: Asante asali wangu. (Anaketi). Hebu nikae

kwanza. (Wanatazamana). Habari za hapa?

Beti: Nzuri tu, za kazi?

Tuma: Safi.

Mfano huo mmoja unatosha kuonesha kuwa

utanzu wa tamthiliya haupaswi kuwa na maneno

yote hayo. Matendo yaonekane kupitia vitendo na

sio kusimulia vitendo hivyo. Maneno yote hayo

yangefaa kama ingelikuwa ni katika utanzu wa

mchezo wa redio. Kwa hiyo, ukiangalia majibizano

ya wahusika Beti na Tuma katika (i) na (ii) yaliyopo

hapo juu, yale yaliyopo katika (i) ndiyo bora; na yale

yaliyomo katika (ii) ni uwasilishaji mbovu wa

tamthiliya.

(b) Kila sehemu ya tukio inapobadilika hapo

tayari kuna matukio mawili na sio moja. Kama

onesho lilikuwa linafanyikia sebuleni, mhusika

akinyanyuka na kuingia jikoni - tayari hayo ni

maonesho tofauti na yanapaswa kutochanganywa.

Jambo hili pia linatofautisha tamthiliya na igizo la

runinga au mchezo wa redio.

5.4 Historia ya Tamthiliya ya Kiswahili

Kwa mujibu wa Edwin Semzaba, tamthiliya ya

Kiswahili ilianzia kwenye sanaa za maonesho za

jadi ambazo zililenga kusaidia jamii katika mambo

mbalimbali. Sanaa hizi za maonesho za jadi ni

kama vile ngoma, maigizo simulizi ya (watoto, au

watani wakati wa misiba); sherehe za kuzaliwa

watoto na kutoa majina; sherehe za jando na

unyago; majigambo, na utani; na kadhalika.

Matendo haya yalikuwa ni ya dhati kutokana na

jukumu lililokuwepo katika jamii.

Baadaye matendo haya ya dhati

yaliondolewa kutoka katika udhati wake na

kufanywa kuwa maigizo ya matendo hayo (yakiwa

ni maigizo ujue kuna masihara ndani yake); ni

kama vile waigizaji wanafanya sherehe za jando na

unyago jukwaani, au kwenye mchezo wa redio,

runinga, au kwenye filamu. Yale wayafanyayo siyo

ukweli wenyewe bali ni mwigo wa ukweli huo.

Chanzo kingine kilichofanya tamthiliya ya

Kiswahili ichipuke ilikuwa ni wakati wa ukoloni

ambapo Waingereza walikuja na drama zao

(tamthiliya za William Shakespeare ambazo

ziliingizwa mashuleni). Wanafunzi walitakiwa

kuigiza tamthiliya hiyo katika siku ya kufungua

shule; siku ya wazazi; au wakati wa mashindano

ambapo shule mbalimbali za sekondari

zilishindanishwa na mshindi alipewa zawadi.

Baadaye Watanzania waling'amua kuwa

michezo hiyo ya kuigiza haikuyahusu maisha yao

na hata kilichokuwa kikiongelewa hawakukielewa.

Kutokana na matumizi ya lugha ya Kiingereza;

kilichowavutia ilikuwa ni uigizaji, uvaaji wa mavazi

maalumu; matumizi ya taa; majukwaa maalumu ya

kuigizia; na utamkaji wa maneno ya Kiingereza.

Watanzania wakaanza kutengeneza sanaa

zao zenye mwelekeo wa kidrama. Wakatumia

vichekesho ili kuwacheka washamba mbalimbali

ambao walikuwa hawajua tamaduni mpya za

Kizungu ambazo zilikuwepo katika jamii.

Vichekesho kama Mshamba wa Kioo vilishika kasi

katika jamii yetu. Vichekesho vililenga kuwacheka

Waafrika ambao bado walikuwa ni washamba

kutokana na vitu vya kigeni ambavyo vilikuwepo

katika jamii na waliojua kuvitumia ni wale werevu

(wasomi) waliosoma katika shule za Wazungu.

Baadaye dhima ya vichekesho ilibadilika

kwa wasanii kutunga vichekesho vinavyowacheka

Wazungu weusi ambao walionekana ni

malimbukeni. Huu ulikuwa ni wakati wa kujitambua

na kudai ukombozi wa Bara la Afrika na Tanzania

ikiwemo. Vichekesho vikaacha kuwadhihaki

Watanzania ambao hawajui mila na tamaduni za

Kizungu - na vikaanza kuwacheka Waafrika ambao

walijifanya Wazungu-weusi.

Baada ya baadhi ya wahitimu kumaliza

shahada ya chuo kikuu cha Dar es Salaam,

wakaanza kuandika tamthiliya zenye mwelekeo wa

drama za Wazungu. Tamthiliya za Penina Muhando

kama vile Hatia, Heshima Yangu; na za Ibrahim

Hussein kama vile Wakati Ukuta na Kwenye Ukingo

wa Thim; tamthiliya za Semzaba Ngoswe Penzi

Kitovu cha Uzembe na Tendehogo (kwa kuzitaja

kwa uchache) zikafuata mwelekeo wa drama za

Kizungu. Tamthiliya hizi zilizingatia vipengele vya

tamthiliya kama vilivyotajwa na Aristotle yaani:

maudhui; ploti; uteuzi wa lugha; wahusika; kionwa;

na muziki vikatiliwa maanani sana.

Kisha, wasomi hawa kwenye miaka ya 1980

na kuendelea, wakaanza kubadili mawazo yao na

kutaka kutunga Tamthiliya za Kitanzania ambazo

zitajumuisha sanaa za maonesho za Kiafrika

(sanaa za jadi) katika utunzi wa drama hizo. Ndipo

mabadiliko haya yakatupeleka kwenye tamthiliya

kama: Lina Ubani na Nguzo Mama (Penina

Mlama); Mkutano wa Pili wa Ndege (Amandina

Lihamba); Jogoo Kijijini na Ngao ya Jadi (Ebrahim

Hussein); Kija (Shani Kitogo); Safari ya Chinga

(Shani Omari), na Changamoto (Elizabeth Godwin

Mahenge) kwa kuzitaja kwa uchache tu. Tamthiliya

hizi zilichanganya miundo ya tamthiliya za Kizungu

na vipengele vya sanaa za maonesho za Kiafrika

katika kutunga tamthiliya ambazo tunajivunia

kusema kuwa ni 'Tamthiliya za Kitanzania

barabara'.

Watunzi hawa wa tamthiliya walipoanza

kutunga kazi zenye mwelekeo wa Kiafrika, kukawa

na mwamko katika kumbo zingine za fasihi andishi

ambayo ni ushairi wa Kiswahili. Ni kipindi hiki ndipo

mgogoro wa ushairi ulipozuka, ukipambanisha

washairi wa kimapokeo na washairi wa kisasa.

Mgogoro wao ulijikita katika hoja ya uasili wa

ushairi kwamba, mwingine ndio ulikuwa na asili ya

Kiafrika na mwingine ulikuwa ni mwigo wa tungo za

Kimagharibi. Si hivyo tu, bali kipindi hiki ndipo

tunapoona fasihi ya majaribio ikijichomoza. Ni

majaribio ambayo pia yalijitokeza katika kumbo ya

tamthiliya.

Hivyo, kwa mujibu wa Semzaba, tamthiliya

ya Kiswahili inaweza kuwekwa katika vipindi vinne:

Kabla ya ukoloni (sanaa za maonesho za jadi);

wakati wa ukoloni (vichekesho na drama za

Kizungu); baada ya ukoloni na wakati wa Azimio la

Arusha (1960's-1990's); wakati wa vyama vingi vya

siasa (1995 na kuendelea).

5.5 Vipengele 6 vya Tamthiliya

Tamthilia ni utanzu wa sanaa za maonesho ambao

uliletwa na wakoloni wakati wa ukoloni. Kabla ya

ukoloni, jamii yetu ilikuwa na tamthiliya ambazo ni

za ufaraguzi (yaani ambazo zilitungwa bila

kuandikwa) na waigizaji walichukua husika

mbalimbali. Wakati wa ukoloni, mambo yalibadilika

kidogo ambapo, wakoloni wa Kiingereza walitafuta

namna ya kujiburudisha na kukumbuka nyumbani

kwao Ulaya. Katika kutimiza hilo, wakaleta

tamthiliya za Shakespear ambazo ziliigizwa na

Watu wa Afrika Mashariki.

Baadaye, tamthiliya ya Kiswahili ilitumia

tafsiri kwa kuwa baadhi ya tamthiliya za

Shakespear zilitafsiriwa kama vile Juliasi Kaisari

(Mwalimu Nyerere) na Mfalme Edipode (Mushi).

Tamthiliya hizi kwa Kiswahili zilileta changamoto

kwa wasomi na waandishi wa Kiafrika na hapo

wakaanza kutunga tamthiliya zao kwa kutumia

muundo wa tamthiliya za Ulaya. Hadi kufikia hatua

hiyo, tamthiliya ya Kiswahili ilikuwa imeshazaliwa.

Kwa mujibu wa Aristotle ambaye ni gwiji

katika fani hizi za sanaa za uigizaji alitaja vitu sita

muhimu ambavyo vinatakiwa viwepo ili utanzu

uweze kupewa hadhi ya kuitwa tamthiliya (drama).

Vipengele hivi ni pamoja na: muziki, kionwa,

maneno/dayolojia, wahusika na uhusika, dhamira,

na msuko wa matukio. Tutaangalia kipengele

kimoja baada ya kingine ili tuweze kuelewa vizuri.

5.5.1 Msuko wa Matukio/Ploti

Ploti au msuko wa matukio ni ile namna ya

mpangilio wa kisa katika simulio. Msuko huu

unaweza kuwa wa moja kwa moja au unaweza

kuwa wa urejeshi. Jambo la msingi kwa

mwongozaji wa mchezo wa kuigiza ni kuelewa

msuko huo ili aweze kuwaelekeza waigizaji wake

waweze kuiwasilisha dhamira ya mwandishi kwa

ufanisi.

Msuko wa matukio/ploti (au kisa) ni lazima uwe

na mwanzo, kati, na mwisho; lakini si lazima kwa

mchezo kufuata huo mpangilio, na ndio maana

tumetaja kuna namna mbili za kuwasilisha hadithi

(ama moja kwa moja au kwa mrejesho). Ploti ina

mwanzo, kati na mwisho.

MWANZO

Katika sehemu hii ya mwanzo, mwandishi anajaribu

kutambulisha mahusiano kati ya wahusika ili

ikitokea mtazamaji anaona hawapatani – swali hilo

liweze kujijibu kutokana na mwanzoni ilivyoonesha

wasifu wa kila mhusika. Mathalani tunaoneshwa

kuna wahusika ambao ni ndugu wa kuzaliwa (yaani

kaka wawili ambao wamezaliwa na baba mmoja na

mama mmoja, kaka hawa wanapendana sana na

haiwezi kufikiriwa kuwa wanaweza kugombana).

Pia katika sehemu hii ndipo tunapotambulishwa

mandhari ya mchezo husika ni wapi; na vilevile

tunaweza kujua mwelekeo wa kazi husika kama ni

ya huzuni, majonzi, mapenzi, au vita.

KATI

Sehemu hii ya kati ndio ile inayokuza mgogoro.

Mgogoro huu unakuzwa kwa kuonesha mielekeo

tofauti ya wahusika na hata yale mambo

wanayoyasimamia. Tuchukulie mfano wa hao kaka

wawili ambao wanaelewana sana na kupatana;

kwamba, itokee wanachangia mwanamke (yaani

mmoja awe na rafiki yake wa kike halafu yule

ndugu wa pili naye aingie hapohapo). Hebu fikiria

hawa ndugu watakuwa katika hali gani? Je, kule

kupendana kwao kutaendelea vilevile? Jibu ni

hapana, na katika jibu hili ndipo tunapoweza kuona

mgogoro ukikua na hata kaka hawa kudiriki

kufanyia matukio mabaya.

Inawezekana mmojawapo akapanga kumwua

mwenziwe. Katika harakati hizi za kuuana ndipo

mchezo unapofikia kwenye kilele chake na

mwelekeo wa mchezo utabadilika – tukikumbuka

ulianza vizuri kwa akina kaka hawa kupendana –

sasa tunaona ni maadui wa kutupwa.

MWISHO

Sehemu hii sio lazima iwe suluhisho kwani kuna

matatizo ambayo ni magumu na mwandishi

huyaepuka kutoa suluhisho ambalo linaweza

kuonekana ni la uongo. Tunaweza kusema kuwa,

sehemu hii ni ya hitimisho la kisa. Kama mkasa au

kisa kilisababisha ndugu hawa kuuana – je, ikitokea

kweli mmoja akafanikiwa kumuua nduguye, je

mahusiano yake na yule msichana yatakuwaje; na

mahusiano yake muuaji na familia, au marafiki zake

yatakuwaje? Katika kupata majibu ya maswali

haya, ndipo tunapoweza kuona mshuko wa mkasa

na inaweza kuwa ndio mwisho wa mchezo.

Kwa hiyo, ni jambo la msingi kabisa kwa watunzi

wa kazi za kiubunifu wazingatie msuko wa matuki

na sio kukurupuka na kuandika visa visivyo na

mzizi. Mathalani, hapa nyumbani kuna baadhi ya

drama au filamu ambazo zikichezwa hadi

unashangaa kuwa hawa watu wanajua watendalo

au wamedandia gari kwa mbele. Utakuta kunaibuka

tu mgogoro ambao chanzo chake hakiko bayana na

hivyo kuondoa ukubalifu na uaminikaji wa jambo

husika mbele ya macho ya hadhira (believability).

5.5.2 Wahusika na Uhusika

Wahusika ni nyenzo inayomwezesha mwandishi

kufikisha ujumbe wake kwa hadhira aliyoilenga.

Kuna wataalamu wamejadili kuhusiana na dhana hii

ya wahusika. Tutawadondoa hapa chini ili tuweze

kueleweka.

Kwa mujibu wa Kamusi ya Fasihi, Istilahi, na

Nadharia, mhusika ni:

Kiumbe anayepatikana katika kazi ya kifasihi na

ambaye anafanana na binadamu kwa kiasi fulani.

Wasifu wa mhusika unategemea mkabala uliopo.

Kazi zinazoegemezwa katika mitazamo ya kihalisia

zinamsawiri mhusika kwa namna inayokaribiana sana

na binadamu katika ulimwengu wa kawaida

(Wamitila, 2003 uk.123).

Brockett (1964) kwa upande wake anaelezea kuwa

mhusika ni kitu muhimu sana katika msuko wa

matukio ya hadithi. Msuko huu huweza kuelezwa

kupitia migogoro na matamanio tofauti tofauti ya

wahusika, ambao kwa kutumia mazungumzo na

tabia zao tofauti huwezesha kuukuza mgogoro.

Brockett anaeleza sifa za aina nne za mhusika

kuwa ni: za kimaumbile, za hali ya kisaiolojia, za

nafasi yake katika jamii, na za kimaadili.

Kimaumbile – tunaangalia: je, mhusika

anaonekanaje kiumbo ? Je, ni mnene au

mwembamba? Je, ni mweupe au mweusi ? Je, ni

mfupi au mrefu. Kisaikolojia mhusika anatazamwa

hali yake ya kiakili – je anapenda nini na hapendi

nini? Kijamii mhusika anatazamwa kuwa anafanya

kazi gani – je ni mkulima, mwalimu,

mfanyabiashara, mchungaji na kadhalika.

Kimaadili - mhusika anachunguzwa namna

anavyoweza kufanya uchaguzi au uamuzi wa

jambo moja kati ya mawili ambayo yako mbele

yake (Brocckett, 1964 uk.30).

Kutokana na maelezo hayo hapo juu,

inaonekana kuwa dhana ya uhusika na dhana ya

uigizaji haitofautishwi. Wamitila (2003) na Brockett

(1964) wanamjadili mhusika kuwa ni kiumbe (mtu)

lakini hawaongelei lolote kuhusu mhusika kama

mashini, mnyama, mawe, na viwakilishi vingine

ambavyo si binadamu. Hata hivyo, dhana ya

uhusika ni ya jumla na dhahania zaidi

ikilinganishwa na dhana ya uigizaji ambayo ni

mahususi. Mwigizaji ni lazima awe binadamu, lakini

mhusika si lazima awe binadamu. Dhana hii na

utofauti uliopo ni mambo muhimu katika

kuchambua wahusika wa kazi za kimaandishi kama

tamthilia ; na waigizaji ni muhimu katika kazi za

utendaji kama drama na filamu. Maana na tofauti

hizi za wahusika na waigizaji zimefafanuliwa wazi

katika nadharia ya usimulizi

Scholes na Kellogg (1966) wanaelezea

dhana ya uhusika katika nadharia ya usimulizi kuwa

haiwezi kutenganishwa na usimuliaji wa tukio katika

hadithi. Mhusika ni nyenzo anayoitumia mwandishi

ili kusimulia tukio au jambo fulani. Scholes na

Kellogg (1966 :160) wanasema:

Mhusika ni kitu gani kama sio kiwakilishi cha tukio?

Tukio ni kitu gani kama hakitafafanuliwa kupitia

mhusika? Je picha ni kitu gani au novela (riwaya) ni

nini pasipo kuwepo mhusika? Je ni kitu gani tutakuwa

tunakitafuta kwenye riwaya au picha kama

hatutatumia au kuwahusisha wahusika?...

Hoja inayowasilishwa na (Scholes na Kellogg,

1966) inadhihirisha kuwa si rahisi kuelezea dhana

ya uhusika pasipo kuelezea tukio linalotendwa; si

rahisi kutenganisha tukio na mhusika katika

simulizi, vitu hivi vinajengana na kutegemeana.

Wahusika na tukio ni kama pande mbili za sarafu

moja ambazo haviwezi kutenganishwa.

Kwa mujibu wa (Bal, 1985), uhusika na

uigizaji ni dhana mbili ambazo hazina budi

kutofautishwa. Dhana moja inajikita katika kueleza

ujumla wa mambo, ikihusishwa na matendo (au

tukio); na nyingine ikieleza jambo mahsusi.

Mhusika ni wakala ambaye anafanya matendo

fulani. Mhusika si lazima awe binadamu, lakini

lazima awe mtendaji (Bal, 1985, uk5).

Uhusika ni istilahi inayojumuisha wigo

mpana (au wa jumla) kuliko ilivyo kwa istilahi finyu

ya uigizaji. Kwa maneno mengine, mbwa, mashini,

na kitu chochote kisicho binadamu kinaweza kuwa

mhusika na sio kinyume chake. Kwa upande

mwingine, mwigizaji anafafanuliwa katika nadharia

hii kama kiumbe ambacho kinasimama badala ya

kitu kingine katika usimulizi. Kiumbe hiki awe ni

binadamu au la, hupewa sifa za binadamu ili

kukamilisha usimulizi. Mwandishi anawezesha

kumpa mwigizaji sifa (wasifu) kwa kutumia

ufafanuzi ambao unamfanya mwigizaji aweze

kuvaa sura ambayo inamfanya afanane na

binadamu halisi kwa kuwa na haiba, saikolojia, na

itikadi (Bal, 1985 uk. 115).

Kwa hiyo, mhusika hupewa wasifu wa aina

mbalimbali ili dhana ya uigizaji iweze kupatikana.

Jambo hili linafanywa na mwandishi kwa uteuzi

maalumu ili jambo analotaka kuliongelea liweze

kuiwakilisha jamii anayoisemea. Na kwa hiyo hapa

tunaona hatua tatu muhimu ambazo ni: mwandishi,

wahusika wake na jamii, hatua hizi zinatokeza

uigizaji anaoufanya mwandishi kupitia katika kazi

yake.

“Dhima za wahusika kinadharia si za mtunzi

binafsi bali ni miundo inayopatikana katika jamii

kwa ujumla” (Wafula na Njogu, 2007 uk.16). Ukweli

huu unadhihirisha mambo mawili katika nadharia ya

naratolojia. Kwamba, mtunzi anajiondoa yeye na

kuwafanya wahusika kusema kwa niaba yake; na

pili ni kuwa, wahusika wenyewe hawajisemei wao

kama wao, bali pia wao kama wawakilishi wa jamii

wanamotokea. Upekee wa lengo la mwandishi

unajitokeza kwa jinsi anavyochagua mhusika wa

kumsemea na kuisemea jamii na kumpa mhusika

huyo lugha inayoendana na dhima yake.

Wakiandika kuhusu “Freud, Ndoto na Fasihi

Wafula na Njogu (kama ilivyotajwa hapo kabla)

wanasema:

Nao wahusika wanaopatikana katika fasihi ni

wanadamu wanaoishi katika ndoto na njozi za

mwandishi. Hawa ni kama vile wanadamu wa kweli

wanaoshirikiana na mwandishi katika matatizo na

matarajio yake” (Wafula na Njogu, 2007 uk 79).

5.5.3 DHAMIRA

Dhamira ni yale yazungumzwayo katika kazi ya

sanaa; ni lile wazo; au hoja; au jambo ambalo

linajadiliwa na mwandishi. Mathalani, katika

tamthiliya ya Machozi ya Mwanamke iliyotungwa na

Ibrahimu Ngozi (1977), inahusu ukombozi wa

mwanamke kutoka katika uonevu wa mwanaume.

Tutathibitisha jambo hili kupitia katika sehemu ya

utangulizi ambayo aliiandika mwandishi

mwenyewe. Mwandishi anasema:

Mwaka 1975, ulitangazwa na Umoja wa

Mataifa kuwa ni mwaka wa kina mama.

Wanawake wapate haki zaidi na usawa kati

yao na wanaume. Kwetu sisi Watanzania

wanawake walio wengi wako vijijini. Hivyo

basi itakuwa ni kujidanganya iwapo kama

tutapiga kelele juu ya ukombozi wa

mwanamke tukimfikiria mwanamke afanyaye

kazi mjini tu, kwamba apate madaraka zaidi

na nafasi zaidi za kuonesha uwezo wake, hali

tukimsahau kabisa, mwanamke aliye kijijini,

akigandamizwa, kunyanyaswa, na kuonewa

na mwanaume miaka nenda rudi!

(Ngozi, 1977uk. iii).

Kutokana na nukuu hiyo hapo juu,

tunaweza kuiona dhamira ya mwandishi ambayo

inaweza ikawa na vijidhamira vidogodogo ambavyo

vinasaidia katika kuijenga. Kila kazi ni lazima iwe

na ujumbe,dhamira, wazo, hoja, au jambo ambalo

linaongelewa. Bado hakujawahi kuwa na ‘sanaa

kwa ajili ya sanaa tu’ (art for art sake) – kila sanaa

inao ujumbe au inayo dhamira inayoongelewa na

mwandishi.

5.5.4 MANENO/DAIOLOJIA

Maneno au daiolojia ndio roho ya mchezo wa

kuigiza. Mchezo wa kuigiza wa redioni unahitaji

maneno mengi kwa kuwa lengo ni kuwafanya

wasikilizaji waone yale yanayoigizwa kulingana na

muktadha huo; kwa hiyo kuna uzungumzaji mwingi

katika michezo ya kuigiza ya redioni.

Michezo ya kuigiza ya jukwaani inapaswa

iwe na daiolojia inayosaidia kusukuma mchezo

mbele. Hakupaswi kuwa na mahubiri ambayo

yatalenga kuelezea au kusimulia jinsi matendo

yanavyofanyika – hapana! Mchezo wa kuigiza wa

runinga au jukwaani hauhitaji maneno mengi- bali

unahitaji maneno machache ambayo yatakuwa

yanausukuma mchezo na hivyo kuendelea mbele

na sio ‘gari kukwama kwenye mchanga’.

Kwenye filamu ndio kabisa haitaki maneno

mengi- kinachotakiwa ni matendo (picha) ieleze

hadithi na sio maneno. Kwa ujumla, maneno ni

muhimu katika fani hii ya uigizaji ila inategemea

kinachoigizwa ni kwa ajili ya nini – je ni kwa ajili ya

redio? Runinga? Au filamu?

5.5.5 MUZIKI

Muziki kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu

(2000:268) ni mpangilio wa sauti za ala, uimbaji au

vyote viwili, unaoleta athari fulani kwa kiumbe;

wimbo. Muziki katika dhana nzima ya uigizaji sio tu

zile sauti ziimbwazo pamoja na mapigo ya vyombo

(ala za muziki) - hapana! Muziki unajumuisha

mpando na mshuko wa sauti za waigizaji pale

wanapojibizana katika kuifanya drama isonge

mbele.

Vilevile ule utofauti wa sauti za waigizaji

kama vile: sauti kali, ya juu, nzito; na kwa upande

mwingine sauti ya upole, nyororo, na nyembamba

hufanya mazungumzo yanoge katika igizo. Hali hii

inathibitisha umuziki uliopo katika uigizaji. Kwa hiyo

katika uigizaji, dhana ya muziki ni pana zaidi kuliko

ilivyo finyu katika muktadha wa uimbaji.

5.5.6 KIONWA

Kionwa ni dhana inayojumuisha vile vitu vyote

vinavyoonekana jukwaani vikimsaidia mhusika

kuutoa ujumbe unaotakiwa. Ni kila kitu kilichopo

jukwaani ambacho kinawezesha igizo kutendeka.

Tunaweza kujumuisha mavazi, vifaa vya kushikwa

au kutumiwa na waigizaji katika husika zao, na hata

maleba; vyote kwa pamoja vinaunda dhana hii ya

kionwa.

Kionwa au vionwa vinapaswa vitumike

kulingana na sababu husika kwa maana kuwa,

mhusika hapaswi kubeba au kushika kifaa

ambacho hakitamsaidia kuuvaa uhusika wake na

kutoa ujumbe uliotarajiwa. Kama mhusika

anaonekana akibeba kibuyu – lazima kuwe na

sababu ya yeye kubeba kibuyu hicho; na sio kama

inavyotokea katika sanaa zetu za hapa nyumbani –

ambazo utamwona mhusika katika kila onesho

amebeba manati au ameshika kibuyu ambacho

hakitumiki katika onesho. Mambo haya yanafanyika

isivyo – hakuna budi kubadilisha na kufanya kama

taaluma ya uigizaji inavyotaka na kuelekeza.

5.5.7 Hitimisho

Vipengele sita vya tamthiliya ni muhimu sana katika

sanaa yoyote ya maonesho. Hivyo mwanasanaa

hana budi kuvielewa vipengele hivi kwa undani na

kuvizingatia atungapo kazi yake; au aingiapo

kwenye uhusika wakati wa kuigiza.

5.6 Aina za Tamthiliya

Tamthiliya ni mtu akiwa kitendoni (Semzaba, 1997);

au kwa maneno mengine, tamthiliya ni umithilishaji

wa maisha ya binadamu katika jukwaa. Tamthiliya

ni pale msomaji anapofungua ukurasa wa kitabu na

kuisoma – inapokuwa inachezwa, sio tamthiliya

tena, bali ni drama. Drama hii inaweza kuwa katika

maumbo mbalimbali kama vile: mchezo wa

jukwaani, mchezo wa kwenye runinga, mchezo wa

kwenye redio, au filamu.

Tamthiliya iko katika makundi mawili ambayo ni

ramsa na tanzia. Tutatumia maarifa tuliyoyapata

darasani wakati Mwalimu Edwin Semzaba (wa

Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam) na

Daktari Aldin Mutembei (wa Idara ya FAMU Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam) walipokuwa

wakifundisha mada ya tanzia na ramsa. Kwa kiasi

kikubwa, mada hizi zimechukua maarifa yao kwa

kuwa nilikuwa mwanafunzi wao na hivyo nikajifunza

kutoka kwao.

5.6.1 TAMTHILIYA YA KIRAMSA

Tamthiliya ya kiramsa au kikomedia inatakiwa

onesho lake liivutie akili. Yaani onesho hilo lisivutie

hisia au mihemko. Chukulia mfano wa tamthiliya ya

AMEZIDI, ambayo inavutia akili na kujiuliza

‘mantiki’ ya mambo wafanyayo wahusika.

Sifa nyingine ya ramsa ni lazima kuwe na

matendo yanayotendwa bila ya kufikiria. Lengo la

kufanya matendo bila kufikiria ni kwa ajili ya

kumcheka mhusika kutokana na upumbavu

wakewake.

Sifa ya tatu ya komedia ni kuwepo na desturi au

mila ambazo hadhira inazifahamu kutoka katika

jamii yake ambazo zinazodokezwa katika onesho.

Kwa mfano ni katika onesho la Mizengwe la

Jumapili, ambapo Mjumbe wa Nyumba kumi

(kiongozi wa watu) anavyoshikwa kwa ugoni na

wake za watu ambao anawatongoza kwa nyakati

tofauti. Kwa hiyo, mila na desturi za jamii husika

zinaona uzinzi kuwa ni kitendo kiovu. Kwa hiyo

kuna ucheshi kwa watakaokamatwa na tukio hili.

Anapokamatwa na kupigwa, hadhira haimwonei

huruma bali itamcheka.

Sifa ya nne ni kuwa, mazingira ya onesho na

vipengele vyake visiwiane au kupatana. Hii ina

maanisha kuwa, ile ploti haina nafasi katika ramsa.

Na ndio maana kila juma kuna mkasa tofauti katika

vipindi hivi vya ramsa za runingani ambazo hazitoi

mwendelezo wa visa. Tazama Ze Comedy au

Origino Comedí, Mizengwe, na Futuhi.

Sifa ya tano ni kutokuwaogopesha hadhira.

Inatakiwa kuwa, hadhira inapoangalia isiogope au

kupata uchungu bali icheke kwa kejeli kutokana na

ama tabia mbaya au matendo mabaya ambayo

mhusika anayatenda (Mwalimu Edwin Semzaba,

Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;

Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam)

5.6.2 Sifa za Shujaa wa Kimramsa

Sifa za shujaa wa kiramsa ni pamoja na:

- Asiwe mtu maarufu katika jamii. Anaweza kuwa ni

kichaa au mwendawazimu fulani ambaye yuko

katika jamii.

- Awe ni mtu duni katika jamii lakini matendo yake

ni ya kiucheshi-ucheshi. Mtu huyu historia humlea

na kumkuza hata akatokea kuwa “fulani” katika

jamii na akaishi raha mustarehe.

- Anatakiwa awe mhusika wa kufurahiwa na

watazamaji kutokana na mafanikio yake. Mhusika

ambaye akifanikiwa kila mtu atafurahia na baada ya

igizo atakuwa ameridhishwa na mwisho huo mzuri

wa kuishi raha mustarehe. Lengo ni kuwafanya

hadhira watue mioo yao baada ya kumwona

mhusika anafanikiwa na kuishi raha mustarehe.

Katika ramsa haitakiwa kuwachosha hadhira kwa

kuwatwisha huzuni katika nyoyo zao (Mwalimu

Edwin Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha

Dar es Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya

FAMU Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

5.6.3 Uhusika wa Wahusika wa Kiramsa

- Wahusika wanaotakiwa kuonekana katika kazi ya

kiramsa ni watu wa kawaida ambao wana kipato

cha kati na chini kama vile: washona viatu, wauza

mitumba, wakata nyama, wachoma mishikaki,

wanafunzi, walimu, wasukuma mikokoteni, n.k.

Tamthiliya ya kiramsa haihusu watu wa juu ambao

ni wafalme, au malkia, au viongozi. Kwa ujumla,

ramsa haihusu watu wote wa nasaba BORA badala

yake ni wale wa nasaba DUNI (Mwalimu Edwin

Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

5.6.4 Dhamira za Kiramsa

Tamthiliya za kiramsa zinahusu mambo ya kawaida

ya watu duni katika jamii. Miongoni mwa dhamira

hizo ni: kufanikiwa kimaisha, kupata marafiki wapya

au kurudisha wa zamani, kupanda cheo n.k.

Tazama komedia zinazooneshwa kwenye runinga

utapata dhamira za kutosha za ramsa. Kwa hiyo

kinachoangaliwa katika ramsa ni mafanikio ya

mhusika ambaye alikuwa hafanikiwi; na mwishilizo

mzuri wenye furaha na kicheko (Mwalimu Edwin

Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

5.6.5. Aina za Ramsa

1) UTANI/ VICHEKESHO

Utani ni aina mojawapo ya ramsa ambayo inalenga

kuchekesha kwa kugeuza mambo ili yawe kinyume;

kuvaa vinyago ili kuchekesha watazamaji. Lengo ni

kuchekesha na maana hupatikana humohumo.

2) MAHABA/ MAPENZI

Aina hii ya ramsa inahusu mapenzi au mahaba.

Kinachofanyika hapa ni kuwawekea vikwazo

wahusika ili wasifanikiwe. Vikwazo vinaweza kuwa

ni pamoja na umaskini, utajiri, ulemavu, ukabila,

udini nk. Lakini wapendanao hawa hufanya mambo

ya kuchekesha ambayo hatimaye huwawezesha

kufanikiwa kutimiza malengo yao.

3) TASHTITI/ DHIHAKARamsa

ya kitashititi ni zile kazi zinazolenga

kuwadhihaki viongozi wa kisiasa, au kidini kutokana

na matendo yao. Kwa mfano zamani Original

Comedy (akina Joti) ilipokuwa ikirusha vipindi

vyake kupitia East Africa Television (EATV).

- Pia tashititi huhusisha hudhihaki wahalifu,

matapeli, wanafiki, wala rushwa, wafanya

magendo, waongo n.k. Kwa hiyo, katika aina hii ya

ramsa, kiongozi ambaye ni mhusika mkuu mwenye

tabia hizo mbaya, anadhihakiwa ili aache. Kwa

mfano, kama kiongozi anapenda ‘dogodogo’ yaani

watoto wa shule, anadhihakiwa ili aache tabia hii.

5.7 TAMTHILIYA YA KITANZIA

- Tamthiliya ya tanzia hutumika kuonesha

kuanguka na kushindwa kwa mhusika maarufu,

mhusika mbabe, au shujaa. Tamthiliya hizi

hutumia mhusika atokaye katika tabaka la juu,

yaani ni mtu mwenye nasaba bora kwa maana

amezaliwa katika nyumba ya kifalme au

kimalkia. Tanzia ilianzia kwenye miviga ya kidini

katika Ugiriki ya kale ikihusishwa na sherehe za

Dionisius.

Lengo la tanzia ni kuwaingizia watazamaji

hisia za woga kutokana na yanayompata

mhusika mkuu, ambayo yanasababisha anguko

lake (Mwalimu Edwin Semzaba, Idara ya

Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; Prof.

Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU Chuo Kikuu

cha Dar es Salaam).

5.7.1 Utokeaji wa Tanzia

Tanzia inatakiwa iwe na uwezo wa kuamsha hisia

za woga na huruma miongoni mwa hadhira. Hisia

za woga na huruma zinatokana na mikasa

inayompata mhusika wa kitanzia ambaye ni

mwema, mzuri kwa sura na umbo, ambaye kila mtu

anampenda na hatakiwi kupata baya lolote. Mfano

mzuri wa mhusika wa aina hii ni wa filamu ya

Second Chance – aliyeitwa Salvado Solenza.

- Mhusika mkuu anatakiwa apate anguko

linalotokana na uamuzi wake mbaya au kosa

analolifanya. Lengo ni yeyé mwenyewe kujiona ana

hatia na hakwepi hatia hiyo. Mhusika wa tanzia

anaikabili hatia iliyopo mbele yake. Kama ni

kunyongwa basi atakwenda kwa hiari kukikabili

kinyongeo na wala hatoroki (Mwalimu Edwin

Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

5.7.2 ISTILAHI KATIKA TANZIA

HAMARTIA

Ni kosa kubwa sana ambalo mhusika mbabe

analifanya na kosa hili humtumbukiza katika kifo

(Mwalimu Edwin Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa

Idara ya FAMU Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

HUBRISI

Hii ndiyo dhambi yenyewe. Ni kule kutenda kosa

kwenyewe. Mfano, Mfalme Edipode kulala na

mama yake mzazi. Kitendo hiki ndicho

kinachomwingiza katika hamartia (Mwalimu Edwin

Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

ANAGNORISIS

Huu ni utambuzi wa ndani ya nafsi ya mkosaji.

Hapa anakuwa ameshalifahamu kosa lake ambalo

limeshamwingiza katika anguko (Mwalimu Edwin

Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

PERIPATEA

Haya ni matendo muhimu ambayo humtoa shujaa

katika hali iliyoonekana kuwa afadhali kumdidimiza

katika hali mbaya kabisa. Kwa mfano, baada ya

Mfalme Edipode kutambua kosa lake, anaamua

kujitoboa macho (Mwalimu Edwin Semzaba, Idara

ya Sanaa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; Prof.

Aldin Mutembei wa Idara ya FAMU Chuo Kikuu cha

Dar es Salaam).

NEMESIS

Hii ni adhabu ambayo haina budi kutendeka

kutokana na kuwapo kwa matendo ya Hubrisi

(Mwalimu Edwin Semzaba, Idara ya Sanaa Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam; Prof. Aldin Mutembei wa

Idara ya FAMU Chuo Kikuu cha Dar es Salaam).

5.8 Hitimisho:

Tamthiliya ni utanzu wa muhimu sana wa sanaa

tendaji ambayo inakusudiwa kutendwa jukwaani.

Kwa mtengenezaji au mtunzi wa drama za runingni,

jukwaani, redioni na filamu, hana budi kuzingatia

maudhui haya yanayoihusu tamthiliya kwa kuwa ni

pande mbili za sarafu moja. Ninamaana kuwa, hiyo

drama ni tathiliya iliyotendwa tayari ambayo

inaonekana mbele ya watazamaji. Kwa upande

mwingine tathiliya ni lile andiko lenyewe la kiuigizaji

ambalo lina wahusika na majibizano yao

yanakuwepo, lakini inakuwa vado haijawekwa

vitendoni.

SURA YA SITA

UANDISHI WA MISWADA YA USHAIRI

6.0 Utangulizi

Ushairi kwa mujibu wa Mulokozi (1996) ni:

Sanaa iliyopambanuliwa kwa mpangilio

maalumu wa maneno fasaha na yenye

muwala, kwa lugha ya mkato, picha, sitiari au

ishara, katika usemi, maandishi au mahadhi

ya wimbo, ili kuleta wazo au mawazo, kufunza

au kuelezea tukio au hisi fulani kuhusu

maisha au mazingira ya binadamu kwa njia

inayogusa moyo. Mulokozi na Kahigi,

(1982:25) kama walivyonukuliwa katika

(Mulokozi 1996:96).

Mtu mwingine aliyeelezea maana ya ushairi ni

Mathias Mnyampala (1965) yeye anasema kuwa:

Ushairi ni msingi wa maneno ya hekima tangu

kale. Ndicho kitu kilicho bora sana katika

maongozi ya dunia kwa kutumia maneno ya

mkato na lugha nzito yenye kunata

iliyopangwa kwa urari wa mizani na vina

maalumu kwa shairi” (Mnyampala,1965:vii).

Mnyampala anaendelea kusisitiza kipengele cha

kutosheleza shida ama haja za shairi

akitahadharisha wale wenye mtazamo kuwa shairi

linapaswa liwe fupi na kwamba shairi refu ni bayalahasha;

kila shairi linapaswa lijitosheleze haja yake

kama ni fupi au refu. Haipaswi kulazimisha shairi

fupi liwe refu, na refu liwe fupi. Kila moja

litategemeana na kile akisemacho mwandishi kama

kimejitosheleza ama la.

Mtu mwingine aliyezungumzia kuhusu ushairi ni

Shabaan Robert yeye anasema:

Ushairi ni sanaa ya vina inayopambanuliwa

kama nyimbo, mashairi, na tenzi zaidi ya

kuwa sanaa ya vina ushairi una ufasaha wa

maneno machache au muhutasari. Mwauliza

wimbo, shairi , na tenzi ni nini? Wimbo ni

shairi dogo, shairi ni wimbo mkubwa, na

utenzi ni upeo wa ushairi. Mwauliza tena kina

na ufasaha huweza kuwa nini? Kina ni

mlingano wa Sauti na herufi. Kwa maneno

mengine huitwa mizani ya sauti; na ufasaha

ni uzuri wa lugha. Mawazo, maoni, na fikira

za ndani zinapoelezwa kwa muhutasari wa

ushairi huvuta moyo kwa namna ya ajabu

(Robert, 1968:61).

Abdilatifu Abdala (1973) anaelezea kuwa ushairi ni:

... na utungo ufaao kupewa jina la ‘ushairi’ si

utungo katika kila ubeti wake kuna ulinganifu

wa vina vitukufu vilivyopangwa kimoja baada

ya chenziye; wenye vipande vilivyo na

ulinganifu na mizani zisizopungua wala

zilizozidi; na vipande hivyo viwe vimetandwa

na maneno ya mkato maalumu na yenye

lugha nyofu, tamu, na laini, lugha ambayo ina

uzito wa fikira, tamu kwa mdomo wa kuisema,

tumbuizi kwa masikio ya kusikia na yenye

kuathiri moyo uliokusudiwa na kama

ulivyokusudiwa...

Tatizo la fasili za Robert (1968), Mnyampala

(1965), na Abdala (1973) ni kule kuona kwamba

shairi linapaswa lipambanuliwe kwa vina na mizani.

Wachambuzi hawa wanaona kuwa vina na miziani

ni uti wa mgongo wa Ushairi wa Kiswahili.

Kwa upande mwingine, fasili ya Mulokozi na

Kahigi (1982) ndiyo yenye mawanda mapana

ambayo inaelezea ushairi ni nini kwa kuzingatia

kanuni na misingi ya utanzu huu. Fasili yao ndiyo

tunayoiunga mkono na inashadidiwa na Massamba

(1983) anapoelezea tanzu za ushairi wa Kiswahili

kuwa ni pamoja na: tumbuzi, nyimbo, shairi, tenzi,

mashairi, na ngonjera (ukurasa wa 60-94).

Anaendelea kuelezea aina za mashairi, mitindo, na

miundo ya mashairi. Pia amegusia sifa za mtunzi

wa ushairi kwamba anapaswa awe na kitu

kinachomsukuma na sio kuwa na vina tu bila wazo.

Vilevile ameongelea kitu muhimu kwa mtunzi ni

kuelewa falsafa za maisha za watu wengine na

kuona anatofautianaje nao au anafanananao vipi.

Pia mtunzi huyu anapaswa kujua hisia za watu

wengine kuhusu falsafa yake na wanapingana naye

kwa vipi na kwa nini (Massamba, 1983:81).

7.1 AINA ZA USHAIRI

Aina za ushairi katika Kiswahili ni pamoja na:

• Tumbuizo

• Nyimbo

• Shairi

• Utenzi – khamziya & takhamisa

• Ngonjera

Mwanafunzi anashauriwa asome makala hii ya

Massamba katika kitabu cha FASIHI III

kilichochapisha na TUKI (1981). Massamba

anadadavua aina hizo za ushairi kwa mapana na

marefu. Vilevile, mwanafunzi anashauriwa atafute

vitabu vinginevyo ambavyo pia vimejadili aina za

ushairi ili aweze kujijuvya kwa kina kuhusu utanzu

huu. Kwa kufanya hivyo, itamwezesha mwanafunzi

kuchagua anataka kuwa mshairi wa ushairi upi?

7.2 VIPENGELE VYA FANI KATIKA USHAIRI

• Vipengele vya fani katika ushairi ni pamoja

na:

• Jina / anwani

• Mandhari

• Wahusika

• Muundo –tathnia, tathlitha, tarbia, tathamisa,

sabilia (soma makala ya Massamba, 1981)

• Mtindo – pindu, msisitizo, beti kubadilishana

vina, kurudiwa kipande kizima cha mstari wa

mwisho kikiwa ni chanzo cha ubeti

unaofuatia (Massamba, 1981) katika TUKI,

FASIHI III.

7.3 MAUDHUI YA USHAIRI

Maudhui ni nini? Maudhui ni yale mawazo ambayo

mtunzi anayawasilisha katika kazi yake ya ubunifu.

Kuna vipengele vya maudhui ni pamoja na:

migogoro, ujumbe, falsafa, msimamo, mtazamo, na

dhamira za mwandishi. Ushairi unaweza kuwa na

matumizi mengi kama: kuomboleza, kubembeleza,

kuliwaza, kufundisha, kuburudisha, kukosoa, na

kadharika

7.4 Hitimisho

Kila mtu ameumbwa kwa majaliwa

mbalimbali jambo ambalo linafanya tuwe tofauti

katika utunzi. Kuna mtu ni mwepesi sana kupata

mawazo ya kutunga shairi, mwingine ni mwepesi

sana kupata vina na mizani, lakini mwingine ni

mzito sana na anaweza kuchukua hata wiki moja ili

kutunga ubeti mmoja wa shairi. Wakati kuna

mwingine ambaye dakika moja ni kubwa sana

kuweza kukutungia ubeti. Kila mtu na majaliwa

yake.

SURA YA SABA

UANDISHI WA MISWADA YA HADITHI FUPI

7.0 Utangulizi

Hadithi fupi ni nini?

Alex Ngure (2003:2) anasema kuwa:

...ni masimulizi yanayojikita katika kisa kimoja

chenye uzito kimaana. Inambidi mwandishi

wa hadithi fupi achague tu yale mambo ya

lazima kuyaelezea”. Hadithi fupi aghalabu

huwa na mhusika mkuu anayehusishwa na

matukio makuu katika hadithi nzima.

Hadithi ni habari za mambo yaliyotukia; ni

mtungo wa habari unaosimulia mambo yaliyotukia.

Hadithi fupi ni mtungo wa habari za kubuni ambao

si mrefu sana – ni kama kurasa kumi hivi na

kunakuwa na wahusika wachache na hata kisa

kinakuwa ni kimoja na ndipo suala la ufupi wa

utanzu huu linapokuja.

Uandishi wa miswada ya hadithi fupi

inatakiwa uegemezwe katika masimulizi ya nini

kilitokea; wapi; lini; nani alihusika; na kwa nini. Ni

utanzu ambao unataarifu kuhusu jambo fulani lakini

taarifa hii inapaswa iwasilishwe kiubunifu kwa

mtindo wa nathari. Nathari ni maandishi ya moja

kwa moja, maandishi ya kawaida ambayo

hayajaandikwa kwa mpangilio wa kishairi.

7.2 NAMNA YA KUANDIKA HADITHI FUPI

Hadithi fupi zinaweza kuandikwa kwa kutumia

mianzo mbalimbali. Kwa mujibu wa Free advice

The 7 types of short story opening/ and how to

decide which is right for your story

www.http://109.com/5814687 wanaeleza kama

ifuatavyo:

i) Unaweza kuanza kwa kutambulisha

mandhari. Hii inafanyika katika aya ya

kwanza ili msomaji aweze kuwajua wahusika

na mandhari.

ii) Kuanza na mgongano – hii inawezekana

kwa kuanza simulizi wakati wahusika

wanakwaruzana kuhusiana na jambo fulani.

iii) Kuelezea jambo la kidhahania. Unampeleka

msomaji katika mambo ambayo hawezi

kuyaona wala kuyahisi. Mathalani,

unazungumzia namna mhusika alivyokuwa

akipanda ngazi za kuenda mbinguni.

iv) Kutumia msimulizi wa nje. Hii ni nafsi ya tatu

inapotumika katika simulizi inamfanya

msimulizi awe huru kuingia ndani ya simulizi

na kutoka. Usimulizi huu una mawanda

mapana.

v) Kutumia usimulizi wa nafsi ya kwanza. Hapa

msimulizi anabanwa na wakati, mazingira,

na muktadha. Msimulizi anasimulia vile vitu

alivyokutana navyo tu.

vi) Kuanza na nukuu. Katika uandishi wa habari

ndiko mtindo huu wa kiuandishi

hupendelewa. Huu sio mtindo mzuri kwa

mwandishi wa kubuni hadithi. Hivyo, uepuke.

vii) Taharuki. Unaweza kuanza hadithi yako na

migongano kati ya wahusika wako na

kumfanya msomaji awe na taharuki kwamba

nini kitatokea.

7.3 VIPENGELE VYA KIFANI VYA HADITHI FUPI

Vipengele hivi ni kama vilivyoelezewa katika

sehemu ya tamthiliya. Japokuwa huu ni utanzu

tofauti, dhana ni ileile.

• Matumizi ya lugha

• Muundo

• Mtindo

• Wahusika

• Mandhari

• Jina/anwani

7.4 MAUDHUI YA HADITHI FUPI

• Dhamira

• Migogoro

• Falsafa

• Mtazamo na msimamo

• Ujumbe

7.5 Hitimisho

Katika maisha ya utunzi, kanuni za jumla hutumika

katika utunzi mahsusi. Ninapotaja kanuni za jumla

ninarejelea mambo ya msingi ambayo

yanakuwezesha kutunga kazi yako. Kanuni

hizohizo unaweza kuzitumia ili kutunga kazi ya

kumbo yoyote ile. Vivyo hivyo mtunzi wa hadithi

fupi, nakushauri usome sehemu ya mwanzoni mwa

kitabu hiki ili ujue kanuni za jumla za utunzi ili

zikuwezeshe kutunga kazi yako.

SURA YA NANE

UANDISHI WA MISWADA YA RIWAYA

8.0 Utangulizi

Riwaya kwa mujibu wa Said Mohamed Abdula

imepata tafsiri nyingi katika nadharia ya fasihi.

Wapo waliozingatia kigezo cha urefu na kuonekana

kuna mapungufu katika kigezo hiki, kwa sababu je

ni urefu wa kimuundo, kimaudhui, kilugha, au yote

kwa pamoja? (Abdula, 1995:66).

Abdula anaendelea kufafanua kuwa, katika

riwaya kuna hadithi, yaani, kuna simulio

linalokwenda hatua kwa hatua katika mfunguko wa

matukio, visa, na mikasa inayojengwa katika

matendo fulani yanayofanywa na wahusika ambao

hutenda au kutendana kuisukuma mbele hadithi

kiwakati na kipahala, huku wakiibua humo au kile

kinachoitwa taharuki kwa hadhira. Pia anaendelea

kufafanua kuwa, riwaya inatakiwa ijibu maswali

matano ambayo ni pamoja na: nani anafanya nini;

wapi anafanyia; wakati gani anafanya; afanye nini

na nani; na kwa vipi? (Abdula, 1995:66).

Mtu mwingine anayetafsiri riwaya ni Njogu

na Chimerah (1999) wanafafanua kuwa ni: “utungo

mrefu wa kubuni, na wenye ploti, uliotumia lugha ya

nathari” (1999:35). Maelezo ya Abdula

tunakubaliana nayo bila shaka yoyote kuhusiana na

maana ya riwaya. Ila fasili ya riwaya kwa mujibu wa

Njogu na Chimerah ina kasoro kuhusiana na

kipengele cha ‘urefu’ kwa kuwa kigezo hicho tu

hakiwezi kuifanya riwaya iwe na sifa ya kuwa

riwaya. Lakini kwa upande mwingine tunakubaliana

nao kuwa riwaya inahitaji ploti (yaani msuko wa

matukio), na lugha ya nathari.

Mulokozi (1996) anaelezea kuwa wataalamu

katika Lugha ya Kiswahili wameelezea maana ya

riwaya kwa namna tofauti. Wataalamu hawa ni

pamoja na Muhando na Balisidya (1976:63); na

Mlacha na Madumulla (1991:1) ambao walizingatia

kigezo cha urefu. Mulokozi anaendelea kukiri

kwamba, fasili zao zina walakini lakini anaiona fasili

ya Senkoro ndiyo inayoelezea kwa uzuri maana ya

riwaya. Senkoro kama alivyonukuliwa katika

Mulokozi (1996:139) anasema kuwa riwaya ni:

Sifa ya uchangamano ni nzuri zaidi kuelezea

maana ya riwaya. Twaweza kusema kwamba

riwaya ni kisa mchangamano ambacho

huweza kuchambuliwa na kupimwa kwa

mapana na marefu kifani na kimaudhui.

Riwaya ni kisa ambacho urefu wake

unakiruhusu kitambe na kutambaa vizingiti

vingi vya maisha kama apendavyo mwandishi

wake. Riwaya basi, ni hadithi ndefu ya kubuni,

yenye visa vingi, wahusika zaidi ya mmoja, na

yenye mazungumzo na maelezo

yanayozingatia kwa undani na upana, maisha

ya jamii (Mulokozi, 1996:139).

8.1 UANDISHI WA MISWADA YA RIWAYA

Uandishi wa miswada ya riwaya inatakiwa

uegemezwe katika masimulizi ya nini kilitokea;

wapi; lini; nani alihusika; na kwa nini. Ni utanzu

ambao unataarifu kuhusu jambo fulani lakini taarifa

hii inapaswa iwasilishwe kiubunifu na kwa mtindo

wa nathari. Nathari ni maandishi ya moja kwa moja,

yaani maandishi ya kawaida ambayo

hayajaandikwa kwa mpangilio wa kishairi.

Riwaya ni hadithi ndefu ya kubuni

iliyoandikwa kwa maelezo ya kubuni aghalabu

inaelezea ukweli fulani wa maisha. Kuna

mchangamano wa visa na matukio na vilevile

kunakuwa na wahusika wengi ambao kila mmoja

ana matamanio yake tofauti na mwingine. Katika

kutofautiana huko kwa matamanio ndiko

kunakotupa hadithi ndefu kwa sababau kutakuwa

na visa na mikasa mingi ambayo inasimuliwa katika

hadithi.

Ili mtunzi aweze kutunga riwaya hana budi

kuwa na visa vingi ambavyo anataka kuvisimulia

katika hadithi yake. Baada ya kuvipata visa hivyo –

inatakiwa afikirie na apangilie kuhusu mtiririko wa

visa na matukio katika simulizi yake, ili kuleta mvuto

utakaomfanya msomaji asikiweke chini kitabu mara

tu atakapoanza kukisoma. Hapa kinachoongelewa

ni msuko wa matukio – jinsi utakavyoyapangilia

tangu mwanzo hadi mwisho; ili katika upangiliaji

huo kuweze kuwa na taharuki za kumvuta msomaji

asome au hata kama imetengenezwa filamu –

aiangalie bila kuudhika na kuzima televisheni yake.

Jambo jingine ni mtunzi kufanya utafiti wa

kina ili ajue undani na ukweli ulivyo kuhusiana na

mambo anayotaka kuyaandikia. Kwa kufanya hivyo,

atajiweka katika mazingira mazuri ambayo

yatawafanya wasomaji au watazamaji wa kazi yake

waamini yale anayowaambia ‘kuwa yana ukweli’

(believability).

Baada ya kuiandika kazi yako (kama ni

riwaya, hadithi fupi, tamthiliya, shairi, au filamu),

huna budi kumpatia mtu mwingine ayasome

maandishi yako kiyakinifu ili aweze kukushauri pale

penye tatizo na kwa kufanya hivyo utaiboresha kazi

yako na kujijengea heshima ya kuandika vizuri!

8.2 AINA ZA RIWAYA

Kuna aina kuu mbili za riwaya ambazo ni dhati na

pendwa. Lakini ndani ya riwaya hizi kuna aina

ndogondogo za riwaya ambazo ni pamoja na:

mahaba, uhalifu, upepelezi, ujasusi, kihistoria,

kijamii, kisaikolojia, vijana, majaribio, barua na

kadhalika.

8.3 VIPENGELE VYA KIFANI VYA RIWAYA

2) Matumizi ya lugha

3) Muundo

4) Mtindo

5) Mandhari

6) Jina/anwani

7) Wahusika

8.4 VIPENGELE VYA KIMAUDHUI VYA RIWAYA

• Dhamira

• Migogoro

• Falsafa

• Mtazamo na msimamo

• Ujumbe

8.5 Hitimisho

Mtunzi chipukizi unapaswa uzingatie mambo

mbalimbali uliyofundishwa kuhusu hadithi fupi,

kwani kwa namna fulani yanaingiliana na utanzu wa

riwaya. Kitu cha kuzingatia ni kujikumbusha kanuni

za utunzi na maelekezo mahususi yanayohusu

riwaya; kisha anza kutunga kazi yako.

Jambo la kukushauri ni kuwa, unatakiwa

uwe msomaji mzuri wa kazi za wenzako ili uone

wanaandikaje. Ukiwa msomaji mzuri na ndivyo

utakavyokuwa mwandishi mzuri. Zingatia jambo

hilo!

 

SURA YA TISA: UANDISHI WA KUBUNI:

NADHARIA

9.0 Uandishi wa kubuni unatakiwa uweje?

Uandishi wa kubuni ni taaluma kama zilivyo

taaluma nyinginezo. Ubunifu ni kazi kama zilivyo

kazi zingine ambazo zina kaida na kanuni zake –

vivyo hivyo uandishi wa kubuni una kaida na

kanuni.

Mwandishi wa kubuni ni yule ambaye

anatumia uzoefu wake pamoja na utafiti ambao

anaufanya kuhusiana na uzoefu mbalimbali ili

kuweza kutoa simulio kwa njia mbalimbali. Utoaji

simulio unaweza kuwa kwa njia ya utunzi wa

hadithi, riwaya, shairi, tamthiliya, mchezo wa redio,

mchezo wa televisheni, au filamu. Vilevile, anaweza

kutoa simulio kwa njia ya uigizaji, uchezaji ngoma,

uimbaji, au uchezaji muziki. Zote hizo ni njia

ambazo mwandishi wa kazi za kubuni anaweza

kuzitumia ili kusimulia kisa alichokuwa nacho katika

mawazo yake.

Uandishi wa kubuni unamtaka mwandishi

atumie milango yake ya fahamu ambayo ni: kuona,

kusikia, kunusa, kuonja, na kugusa katika kusimulia

hadithi au mkasa wowote ambao ama umempata

au umempata mtu mwingine. Mtu huyo anaweza

kuwa ni wa karibu au mbali – haijalishi kwa kuwa

mwandishi wa kubuni anatumia utafiti katika kupata

kitu cha kusimulia.

Katika usimulizi huo, mwandishi wa kubuni

ana uhuru wa kutumia nafsi zote tatu ili kuweza

kugusa hisia za msomaji au mtazamaji wa kazi ya

sanaa. Mtunzi huyu anaweza kutumia nafsi ya

kwanza ambayo inataja kitu kinachokuhusu mtu

binafsi kama vile 'mimi nina...' katika umoja au 'sisi

tuna...' katika wingi.

Akitumia nafsi ya kwanza inaonesha simulio

inamuhusu (kama ndiye au amejifanyisha kuwa

ndiye). Nafsi nyingine ni ya pili ambayo katika

umoja ni 'wewe una...' na katika wingi ni 'ninyi

mna...'. Hii pia inaonesha angalau mwandishi

hayuko mbali sana na simulio japokuwa nafsi hii

haitumiki sana katika uandishi wa kubuni –

hutumika katika uandishi usio wa kubuni ambao

unalenga kumwelimisha msomaji. Lakini si jambo la

ajabu kama utakutana na kazi ya sanaa ambayo

inatumia nafsi ya pili – huu ndio uhuru wa kuchagua

namna ya kusema jambo unalotaka kulisema.

Matumizi ya nafsi ya tatu yanaonesha kuwa

simulio liko mbali na mwandishi – inaonesha sio

yeye wala wakala wake, bali ni mtu mwingine ndiye

yamemkuta hayo anayotueleza. Faida ya kutumia

nafsi ya tatu ni kubwa kwa kuwa inakuwezesha

mwandishi kuogelea popote pale na kusimulia

mambo mengi yanayotokea mahali popote katika

wakati huohuo. Hii inawezekani kwa kuwa nafsi ya

mwandishi haipo hapo – iliyopo ni nafsi ya

msimulizi ambaye anatusimulia kilichotokea. Nafsi

hii ya tatu ni ile ya kusema 'yeye ana...' katika

umoja; na 'wao wana...' katika wingi.

Kwa hiyo, uandishi wa kubuni sio lelemama.

Ili mwandishi aweze kuandika au kubuni kazi

ambazo zinawashika hadhira kikwelikweli, hana

budi kuwa mtafiti na kujielimisha vya kutosha ili

ajue mbinu mpya zinazotumika katika uwanja wa

sanaa ili sanaa yake isipwaye kwa kuonekana

imepitwa na wakati.

9.2 Mchakato wa ubunifu

9.2.1 Mwandishi na zana zake

Uandishi ni nini?

Uandishi ni kazi ya kuandika (KKS, 2000:418).

Kuandika ni kitendo cha kuweka alama au michoro

kwa kutumia herufi ili kuwakilisha sauti.

Ubunifu ni dhana inayotokana na tendo la kubuni.

Kubuni ni kutengeneza kitu kwa mara ya kwanza;

kugundua. Vilevile, tunaweza kusema kuwa, kubuni

ni kuzua au kutunga jambo (KKS, 2000).

Zana ni nini?

Zana ni chombo au kifaa kinachohitajika ili kufanyia

kazi fulani. Katika muktadha wa uandishi wa

kubuni, zana ni pamoja na kalamu, karatasi, na

shajara. Kwa upande mwingine, zana ni lugha

ambayo inamwezesha mwandishi kueleza kile

kilichomo moyoni mwake.

Lugha ni nini?

Lugha ni sauti za nasibu ambazo zinatumiwa na

jamii fulani ili kuwasiliana.

Kuwasiliana au kupashana habari kunawezekana

kupitia njia tatu ambazo ni: sauti, maandishi, na

alama.

Mwandishi wa kubuni anatumia maandishi ili aweze

kuwasiliana. Katika njia hii ya mawasiliano,

anahitaji nyenzo zitakazomwezesha aeleweke kwa

hadhira yake. Nyenzo hizi ni alama za uandishi na

uakifishi.

Alama za uandishi

Alama za uandishi ni nini? Ili uweze kujua vema

jambo hili, huna budi kusoma kitabu cha Mwongozo

wa Wandishi wa Kiswahili cha BAKITA, 1994).

Alama hizi za uandishi ni pamoja na: nukta, nukta

pacha, nukta mkato, koma, kistari, kwa kuzitaja kwa

uchache.

Uakifishaji

Uakifishi ni nini? (Soma vitabu vya Wamitila,

Mwenge wa Uandishi (2009); na Mrikaria Utungaji

(1) cha mwaka (2009) na Kiango Utungaji (2) cha

mwaka (2009).

9.2.2 Mwandishi na mazingira yanayomzunguka

Mazingira ni nini?

Mazingira ni hali au mambo yanayomzunguka

kiumbe katika sehemu anapoishi au maisha yake

(KKS, 2000:238).

Mwandishi huzungukwa na mazingira mbalimbali

kama vile: nyumbani, shuleni, mtaani, kiibada,

kijamii, na kadharika.

Nyumbani:

Nyumbani – je katika familia yako mahusiano

yakoje kati ya wenza na watoto au wanandugu

wengine?

Je, wewe ni yatima? Uyatima wako ulitokana na

nini. Je, uyatima ulitokana na milipuko ya mabomu

ya Mbagala au Gongo la Mboto? Je, ni ajali ya MV

Bukoba au MV Spice Islander? Au je, uyatima

wako ulitokana na mashambulizi ya kigaidi

yaliyochoma Balozi za Marekani nchini Tanzania au

Kenya? Je, wewe ni yatima kutokana na ajali za

barabari au ajali ya ndege? Elezea mkasa wako

kinagaubaga ili uweze kuishika hadhira na

wasomaji wako.

Mahusiano ya wanandugu yakoje?

Je, baada ya wazazi kufariki - mali za marehemu

zilileta ugomvi baina ya ndugu? Je, mashemeji na

mawifi walivamia na kukwapua mali za marehemu?

Je kama kuna watoto wa marehemu – je wanapata

shida yoyote baada ya wazazi kufariki? Majibu ya

maswali haya yatakuwezesha kujua namna ya

kukuza migogoro na migongano katika tamthiliya

au drama

Shuleni – mazingira yakoje kuhusiana na

masomo au shule yako? Je, unakutana na

unyanyasaji wa kijinsia kutoka kwa walimu? Je,

wewe ni mlemavu na unakutana na vikwazo gani

katika mazingira ya shule? Je kama wewe ni

mlemavu unabaguliwa? Majibu ya maswali haya

yatakuwezesha kujua namna ya kukuza migogoro

na migongano katika tamthiliya au drama

Mazingira ya kiimani:

Je, wewe ni Mkristu, Mwislamu, Myahudi? Mhindu,

Mbuddha? Au unaamini katika Uafrika na mizimu?

Je imani uliyonayo inajitokeza katika uandishi wako

- kwa namna unavyotatua migogoro?

Je, imani yako unayoifuata uliipataje: je uliirithi

kutoka kwa wazazi au umebadili dini? Kama

umebadili dini je ni sababu gani zilizokufanya uache

dini x na kuingia katika dini y? Majibu ya maswali

haya yatakuwezesha kujua namna ya kukuza

migogoro na migongano katika tamthiliya au drama

Mazingira ya kijamii:

Unakaa wapi kijiografia: je uko sehemu gani ya nchi

ya Tanzania?

Je, jamii inayokuzunguka ina sifa gani? Je, sifa hizo

zinakuathiri kwa namna yoyote? Je, unaishi katika

jamii ya waliosoma au wasiosoma? Wewe una

kiwango gani cha elimu ukijilinganisha na

wanaokuzunguuka? Je, kiwango chako kinaleta

tatizo lolote la kimahusiano na jamii

inayokuzunguka?

9.2.3 Welewa wa mwandishi kuhusu uhalisi,

uhalisi sambamba, na uzoevu

Uhalisi:

Uhalisi ni nini?

Kwa mujibu wa Wamitila, ni dhana inayotumiwa

katika fasihi kuelezea hali ilivyo katika jamii

kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni (272)

Uhalisia ni mkondo unaosisitiza usawirii wa matukio

au maisha katika fasihi kama yalivyo katika maisha

ya kila siku. Mkabala huu unahusishwa na mfuasi

wa Karl Mark kutoka Hungary anaitwa Georg Lukas

Uhalisi sambamba:

Katika fasihi ni namna ya kuliandika jambo katika

mizania na ridhimu. Kwa kuzingatia hilo, ndipo

tunapopata umbo la kazi na mtiririko wake.

Usambamba huu unahusiana na matumizi ya

maneno yenye uzito sawa na ridhimu ili kuliweka

jambo husika katika mizania. Usambamba wa

'huzuni' ni ridhimu ya 'taratibu inayoonesha

majonzi'. Lakini usambamba wa 'mapambano au

harakati za kuondokana na udhalimu' ni ridhimu ya

'harakaharaka, ya kustua ambayo imechangamka.

Uzoevu au uzoefu:

Uzoefu ni hali ya kukaa au kujishughulisha na

jambo au kitu kwa muda mrefu (KKS, 2000:451).

Mwandishi ana uzoefu (uzoevu) wa kukabiliana na

maisha kwa kiasi gani? Je, ni matatizo gani

ambayo umekutana nayo katika maisha yako? Je,

ni mafanikio gani umekutana nayo katika maisha

yako? Kwa mfano, katika ajali ya MV Spice (2011)

kuna baadhi ya watu waliokolewa na magodoro ya

Tanzania? Magodoro haya yana nailoni na je kama

yasingekuwa na nailoni? Uzoefu wako ukoje katika

tukio fulani?

9.2.4 Uchunguzi sambamba dhidi ya mambo ya

kufikirika

Uchunguzi sambamba wa mambo ya kufikirika

maana yake ni nini?

Uchunguzi unapaswa ufanywe na mwandishi ili

aweze kuandika jambo au tukio bila kuongopa. Kwa

kufanya udanganyifu, mwandishi atapoteza imani

yake kwa wasomaji wa kazi zake.

Uchunguzi ili ufahamu au ujue mtu,

mnyama, mdudu na kadharika – anatembeaje,

anakulaje, analalaje, anaishije, anachekaje,

analiaje, anazaaje, anahusianaje na wenzane na

mazingira yake? Haya ni maswali muhimu katika

kumwezesha mtunzi kufanya utafiti wa kina ili ajue

kitu anachotaka kukiandika akiandikaje na

akiwasilishaje ili aweze kuikamata hadhira yake.

9.2.5 Mwandishi na jadi

Jadi ni nini?

Jadi ni asili ya mtu anakotoka; kizazi cha mtu;

nasaba; ukoo (KKS, 2000:126).

Mwandishi ni mtu wa kabila au mkoa gani?

Je, ni mtu wa nasaba bora au nasaba duni?

Je, ni mtu kutoka ukoo wa kichifu au kitemi au ukoo

wa kawaida?

MWANDISHI NA RASILIMALI ZAKE: RASILIMALI

ZA KIJADI NA KIUTAMADUNI

Rasilimali ni nini?

Rasilimali ni jumla ya mali aliyonayo mtu au nchi.

Mwandishi ana rasilimali nyingi ambazo ni za kijadi

na kiutamaduni; na kwa upande mwingine, ana

rasilimali za kiisimu na lugha.

Rasilimali za kijadi na kitamaduni – ni kuhusu mila,

asili, jadi na desturi za kundi la jamii fulani (KKS,

2000:445).

9.2.6 Rasilimali za kiisimu na za lugha alizonazo

mwandishi

Katika rasilimali za kiisimu: tunaangalia mwandishi

ana umahiri kiasi gani katika isimu ya lugha

anayoitumia kujieleza.

Je, kama anatumia Kiingereza anakimudu

barabara? Je, kama anatumia Kiswahili anakimudu

barabara? Au mwandishi anaandika Kiingereza au

Kiswahili chenye makengeza na matege?

Lugha za mwandishi: je yeye ni mlumbi au ni mtu

anayejua lugha mama peke yake?

9. 3 Hitimisho

Mwandishi chipukizi anapaswa aisome nadharia ya

uandishi wa kubuni ili aweze kujijengea msingi wa

kuifanya kazi hii. Kuandika si jambo rahisi, ndio

maana si kila mtu ni mwandishi bora; mwandishi

nguli; mwandishi maarufu. Kuandika ni kipaji au

tuseme karama ambayo Mwenyezi Mungu

amemjalia amtakaye kwa ajili ya sifa na utukufu

wake. Hivyo cha msingi ni kujitahidi kuzingatia

mambo tuliyokuelekeza ili uweze kuandika kazi na

wewe ujulikane katika ulimwengu wa fasihi kuwa

upo.

SURA YA KUMI NA MOJA: UANDISHI WA KUBUNI:

VITENDO

10.1 Utangulizi

Uandishi wa kubuni ni ule unaojitokeza katika riwaya,

hadithi fupi, ushairi, tamthiliya, na filamu; vitu hivi ni

miongoni mwa aina mbalimbali za uandishi wa kubuni.

Unaweza kujiuliza kwa nini nimerudia sehemu hii? Hii ni

kutokana na umuhimu wake, hivyo nakushauri usome

kwa furaha.

Semzaba (1997:75), anasema “sanaa huanza na

hisi ambazo kila mtu anazo”. Semzaba anaendelea

kuelezea kuwa, mtunzi huchagua umbo la kuwasilishia

wazo lake kama ni hadithi fupi, riwaya, tamthiliya,

ushairi (kimapokeo au kimasivina)-yote yanategemeana

na uchaguzi wa mtunzi.

Khamis (1983:246) yeye anaona kuwa uandishi

wa kubuni ni namna mtunzi anavyoweza kuyasawiri

maisha ya mwanadamu na kuyatungia taswira ambazo

ziko mbali na mazoea ya mwanadamu-kwakuwa ni

maisha kulingana na anavyoyaona mwandishi katika

dunia iliyomo kichwani mwake.

Uandishi wa kubuni unamtaka mtunzi atumie

milango yake ya fahamu kinagaubaga. Kuna milango ya

fahamu mitano ambayo ni pamoja na: kuona, kunusa,

kusikia, kuhisi, na kuonja.

• Kuona: je, mhusika unayemfikiria kichwani

mwako unamwonaje? Umbo lake ni la kuvutia au

kuchusha? Je, macho yake yakoje – je ni ya

golori au la? Ni makubwa au madogo? Je, ni

mlemavu wa macho?

• Kunusa: pua zako zinakufanya usikie harufu

gani? Je, ni harufu mbaya au nzuri? Je, ni

uvundo au marashi? Je, mhusika wako ananuka

kikwapa au uturi? Je, ananuka mdomo?

• Kuhisi: je, unapokaa karibu naye unajihisi nini?

Je, unapata mhemko wowote au huhisi

chochote? Je, akikupapasa mwilini mwako

unajisikia nini? Akikugusa bega unajisikia nini?

• Kuonja: je, ukiweka kitu hicho mdomoni

unaonjaje – ni chungu au tamu? Je, ina pilipili au

masala? Je, kuna chumvi au sukari? Je, kitu

hicho kina ukakasi au uchachu?

• Kusikia: je, sauti unayoisikia ikoje? Inamtoa

nyoka pangoni? Inakufanya ukose usingizi? Je,

ni sauti nzuri au mbaya? Ni nyororo au nzito?

• Kama ni sauti ya muziki – je, iko chini au juu

(kelele)?

Mahenge (2011) anasema uandishi wa kubuni ni

ule unatokana na hisia ambazo zinamsukuma mtunzi ili

atunge kazi yake. Hisia zinaungana na wazo ambapo

vitu hivyo vinamsumbua akilini na kumkosesha raha.

Mahenge anaendelea kufafanua kuwa, mwandishi wa

kubuni anataka aliwasilishe wazo lake ili hadhira

ifahamu kilichopo moyoni mwake. Mwandishi hukosa

usingizi na hivyo hulazimika kuamka na kuandika kile

kinachomsukuma akilini mwake.

10.2 Hitimisho

Uandishi wa kubuni unahitaji ufanywe kwa vitendo na

sio maneno matupu. Mwandishi ninakuhimiza ufanyie

kazi maelekezo yote niliyokupatia katika uandishi wa

kumbo za fasihi na kasha uanze kuandika mara moja.

Anza kwa kupitia zile kanuni za uandishi na kisha nenda

kwenye kipengele cha ‘utaanzaje kuandika’. Ukisoma na

kuelewa sehemu hizo, weka katika matendo yale

mambo unayoelezwa ili uanze kuingia vitendoni.

MAREJEO

BAKITA.Mwongozo wa Waandishi wa

Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam.1994.

Free advice “The 7 types of short story opening/

and how to decide which is right for your

story www.http://109.com/5814687/the 7

types-of-short-story-opening-and-how-todecide-

which-is-right- for-your-story

Mahenge, E. Uandishi katika

Kiswahili.www.lulu.com 2011

Mahenge, E. Sanaa ya Uigizaji: Mwongozo kwa

Waongozaji na Waigizaji wa Michezo ya

Kuigiza ya Jukwaani, Redioni, kwenye

Televisheni, na Filamu. Www.lulu.com 2011

Moshiro Gervas, Michezo ya Kuigiza-10. Mchezo wa Redio

Kusadikika. Tanzania Publishing House. 1979

Kiango, J.G. Utungaji 2:Stadi za Lugha ya

Kiswahili. TUKI. Dar es Salaam. 2009

Mrikaria, S.Utungaji 1: Stadi za Lugha ya

Kiswahili. TUKI. Dar es Salaam. 2009

Paul, E. Writer on Writing. 1963

Semzaba, E. Tamthiliya ya Kiswahili. OUT.1997

Syd Field katika kitabu chake cha Screenplay:

The Foundations of Screenwriting – A step by

Step Guide from Concept to Finished

Script. 1994

www.wikipedia.com

TUKI. Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es

Salaam. 2000.