Na Mwandishi Wetu, MWADUI
KOCHA Msaidizi wa Mwadui FC, Jumanne Ntambi (pichani kulia) amefariki dunia usiku wa leo baada ya kuanguka bafuni wakati anaoga nyumbani kwake Mwadui mkoani Shinyanga.
Taarifa za awali zinasema mwalimu Ntambi baada ya kuanguka bafuni alikimbizwa hospitali ambako walikofika, wakasema tayari amekwishafariki dunia.
Imeelezwa Ntambi alikuwa anasumbuliwa na shinikizo la damu na jana alikwenda hospitali kwa matibabu akaambiwa apumzike, ingawa leo aliwatembelea wachezaji mazoezini Uwanja wa Mwadui Complex.
Mmoja wa wachezaji wa Mwadui FC, Athumani Maulid ameiambia masshele –Blog usiku huu kwamba; “Tumepata msiba, kocha wetu Ntambi amefariki dunia usiku huu”.
Maulid mmoja wa wachezaji wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys ya mwaka jana ameongeza; “Kocha alikuwa anaumwa na leo hakuja mazoezini kikazi. Alikuja tumekwishamaliza akatusalimia, tukazungumza naye, akaondoka ndipo baadaye zikaja taarifa za kifo chake,”amesema.
Bado linasubiriwa tamko la Mwadui FC kuhusu utaratibu mzima wa mazishi ya marehemu, ambaye pamoja na kwamba familia yake ipo Moshi mkoani Kilimanjaro, yeye ni mzaliwa wa Musoma mkoani Mara.  Mungu ampumzishe kwa amani marehemu Jumanne Ntambi.