Kikosi cha Simba.

UONGOZI wa Simba umebainisha kuwa wapinzani wao Horoya AC kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika watakutana na kitu kizito kitakachobaki kwenye kumbukumbu zao daima.

Mchezo wao dhidi ya Horoya unatarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa, Machi 18. Kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa Guinea Simba ilipasuka kwa kuchapwa bao moja na kwenye msimamo ipo nafasi ya pili ikiwa na pointi sita, vinara ni Raja Casablanca wenye pointi 12.

Horoya wao wapo nafasi ya tatu wakiwa na pointi nne na wale Vipers wapo nafasi ya nne wakiwa wamesepa na pointi moja kibindoni.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally alisema kuwa wanakumbuka walipoteza mchezo wa kwanza jambo lililowaongezea mzigo kuwafikiria.

“Kila mchezaji alikuwa anahitaji ushindi kwenye mchezo wa kwanza na hata benchi la ufundi pamoja na mashabiki lakini mpira ulitukatili na tukapoteza sasa wanakuja Dar hakika watakutana na kitu kizito ambacho ni kuacha pointi tatu.

“Sisi hatuna matatizo hasa baada ya kupoteza dhidi ya Raja Casablanca tukakubaliana kushinda mechi zetu mbili kukusanya pointi sita hizi ni muhimu na tumeanza na Vipers kisha wao waafuata ambao ni Horoya.

“Mashabiki tunawaomba mzidi kuwa pamoja nasi kwa kuwa wamekuwa pamoja nasi katika kazi hizi ambazo tunafanya tunatambua wachezaji wapo tayari hivyo wazidi kuwa pamoja nasi bega kwa bega.”