Inaweza kuwa pigo? Ni swali ambalo unaweza kujiuliza kueleeka mechi ya Ligi ya MabingwaAfrika kati ya Simba dhidi ya AS Vita ya Congo Jumamosi hii ambapo mshambuliaji na Nahodha John Bocco ataukosa mchezo huo.

Bocco ambaye amekuwa hana fomu nzuri kipindi cha hivi karibuni aliumia kwenye mechi iliyopita dhidi ya JS Saoura na kutolewa nje huku nafasi yake ikichukuliwa na Meddie Kagere.

Hali ya Bocco mpaka sasa haijawa vizuri na kwa mujibu wa Daktari wa timu amethibitisha kuwa anaendelea kupata matibabu ambayo yatasababisha ashindwe kuwa sehemu ya mechi hiyo kubwa Jumamosi.

Kukosekana kwa Bocco kunatoa nafasi kubwa ya Kagere kuchukua nafasi yake sambamba na Emmanuel Okwi katika safu ya ushambuliaji.

Simba itasafiri siku yoyote kuanzia leo kuelekea Congo kwa ajili ya mechi hiyo ya Ligi ya Mabingwa Afrika ikiwa na kumbukumbu ya kuwanyoa Waarabu kwa mabao 3-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Wakati huo kikosi cha wekundu hao wa Msimbazi kinaendelea na mazoezi ya kufa mtu hapa Dar es Salaam tayari kukoleza moto kuwakabili AS Vita