Jopo  la wataalam kutoka ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, maofisa Ustawi wa Jamii, Wanasheria pamoja na askari Polisi wa dawati la Jinsia  wamemuhakikishia Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda wamejidhatiti vyema kuwasikiliza akinamama ambao wametelekezwa na hawapati fedha za matunzo ya watoto kutoka waume zao.

Ofisi ya Mkuu wa Dar es Salaam ilitangaza kutoa msaada wa kisheria kwa kuwasikiliza wanawake hao na kwamba watatoa msaada huo kwa siku tano kuanzia Aprili  mwaka huu.

Akizungumza na wataalamu hao jana, Makonda alisema tatizo la wamama waliotelekezwa ni kubwa na limekuwa likisababisha kinamama na watoto kuishi maisha ya tabu na kusababisha ongezeko la watoto wa mitaani na vizazi vya watoto wenye chuki na baba zao.

Makonda alisema lengo la mchakato huo si  ugomvi bali ni kumwezesha mtoto kupata mahitaji ili aweze kuitumia vyema fursa ya elimu bure chini ya Serikali ya awamu ya tano.

Pia alisema amewahimiza wataalamu hao kuhakikisha wanawasikiliza kinamama kwa umakini na kusimamia haki pasipo upendeleo.

Pamoja na hayo Makonda alisema wapo kinababa ambao wameanza kutoa fedha ya matunzo ya mtoto baana ya kusikia tangazo ambapo amewaomba kinamama kufika Aprili 9 mwaka huu kwa ajili ya kuonana na watalaamu ili waingie kwenye mfumo rasmi wa kimaandishi.

"Ifike hatua mwanaume ukimpa mwanamke ujauzito bila mpangilio aogope kama ilivyo kwenye ubakaji,"alisema Makonda.