Na Ezekiel Mtonyole – Dodoma.
Kuelekea maadhimisho ya miaka 61 ya Uhuru ambayo huadhimishwa Desemba 9 kila mwaka Wizara ya Elimu Sayansi na
Teknolojia imesema itatumia maadhimisho hayo kwa ajili ya kuitangaza lugha ya Kiswahili
kimataifa kwa kupandisha bango maalumu Mlima Kilimanjaro bango lenye ujumbe wa kukitangaza Kiswahili kimataifa.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma Naibu
Katibu Mkuu Wizara hiyo Prof. James Mdoe amesema watatumia maadhimisho ya miaka
61 ya uhuru kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kiswahili Duniani ambapo kwa sasa
mataifa mengi yanahamasika kutumia lugha ya Kiswahili.
“Sisi Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia
ndio wenye dhamana ya kusimamia elimu hapa nchini kwahiyo tumeona ni wajibu
kusimamia katika kukitangaza Kiswahili zaidi Duniani” amesema.
Aidha amebainisha kuwa kwa sasa takribani watu
milioni 250 ulimwenguni wanazungumza lugha ya Kiswahili na ukizingatia Shirika
la umoja wa mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni UNESCO tayari imeitambua
lugha ya Kiswahili na kuitengea siku maalumu ambayo ni July 7 kila mwaka.
“Ukizingatia Kiswahili ni Lugha ya kwanza
kutambuliwa na UNESCO na kukitengea siku maalumu na sisi kama Wizara ya Elimu
tunawajibu kwa kuendelea kukitangaza Kiswahili zaidi kimataifa” amesema.
Ameongeza kuwa “Mwaka huu tutafanya maadhimisho ya miaka 61
ya uhuru kwa namna tofauti, tutapandisha bango la Kiswahili Mlima Kilimanjaro,
lengo ni kueneza Kiswahili kwa mataifa mengi zaidi kuliko ilivyo sasa,”amesema.
Hata hivyo, amesema lugha ya Kiswahili kwa
sasa inapendwa na watu wengi na kuzungumzwa ikiwamo nchini Misri ikiwa moja
katika ya nchi inayofundisha lugha ya Kiswahili tangu mwaka 1964.
“Kuna vyuo 150 vinafundisha Kiswahili, pia redio na runinga 300 ulimwenguni ambazo zinarusha vipindi kwa lugha hiyo hapo ni nje ya Vyuo vya hapa nchini pia vyuo vya Tanzania vina makubaliano na vyuo vya nje kwa ajili ya kuendelea kufundisha lugha hii na tayari mikataba minne imeingiwa na Wizara.”
“Tunaendelea na mazungumzo na wizara hizo za
nje ya nchi yakikamilika mikataba mingine mitano itasainiwa ili kuwezesha
uanzishwaji wa madarasa ya kufundishia lugha hiyo nchini,” amesema.
Aidha amebainisha kuwa kwa sasa nchi jirani na
Tanzania zinazungumza lugha ya Kiswahili nchi hizo ni kama Uganda, Kenya, Sudani
Kusini, Malawi na Mashariki ya Kongo.
“Na hivi juzi tu kwa kushirikiana na ubalazi
wa Tanzania nchini Malawi tumefungua
darasa la kufundisha lugha ya Kiswahili Malawi na tumekuwa tukisisitiza Mabalozi wetu
wote kuzungumza na nchi husika” amesema.
Kwa upande wake Mwalimu wa Lugha ya Kiswahili
na mwandishi wa vitabu kwa lugha ya Kiswahili Menna Yasser raia wa Misri
amesema Kiswahili kinanafasi kubwa kwa mataifa mbalimbali ni muhimu kuendelea
kukitangaza zaidi.
“Hii ni lugha ambayo mataifa mengi yanatumia,
kuna umuhimu wa kukuza lugha ya Kiswahili, hii lugha imenipa fursa nyingi na
nimeisomea,” amesema.
Naye, mtunzi wa mashairi kwa lugha ya Kiswahili Meja Mwinyikombo Ally amepongeza Wizara ya Elimu kwa kubuni njia hiyo kukitangaza Kiswahili na kuamini kuwa Kiswahili ni kama bidhaa inayouzika nchini na nje ya nchi.
0 Comments