Kama una tabia za kuigaiga mambo kutoka kwenye tamaduni usizozijua, ipo siku mambo hayo yatakutokea puani.


Miongoni mwa habari zinazofuatiliwa mno kwa sasa kwenye vyombo vya habari vya kimataifa ni kuhusu mwanamke mwenye umri wa miaka 32 aliyetambulika kwa jina la Anaya Peterson kutoka nchini Ireland ya Kaskazini ambaye amejikuta akipoteza uwezo wake wa kuona na kuwa kipofu kabisa baada ya kuchora tattoo kwenye nyusi.

Kwa mujibu wa mtandao wa New York Post, Anaya alipata ushawishi wa kuchora tattoo hizo kutoka kwa mwanamitindo Amber Luke wa nchini Australia ambaye alimchukulia kama role model wake.


Kwa sasa Anaya amepata upofu wa moja kwa moja baada ya kemikali zilizotumika kuchora tattoo hizo zenye rangi ya bluu na zambarau kumuingia machoni.

 



Anaya alichora tattoo hizo mwishoni mwa mwaka 2020. Alikaa nazo kwa miezi kadhaa bila kuona madhara yoyote, lakini mwaka 2021 aliamka na kukuta macho yake yakiwa yamevimba. Mpaka sasa amepoteza kabisa uwezo wake wa kuona. Mbali na kupoteza uwezo wa kuona, pia ameanza kuvimba usoni na kusikia maumivu makali.


Mbali na masahibu hayo yanayompata Anaya, pia ameupasua ulimi wake kama sehemu ya kutaka kuzidi kuwa mrembo na kuvutia huku akijichora tattoo hadi usoni na kujitoboa baadhi ya sehemu za mwili wake.


Anaya ambaye ni mama wa watoto 5 anasema kuwa, awali mwanaye wa miaka 7 alimuonya kuhusu tattoo za macho kuwa siyo kitu kizuri na sasa anajuta bora angesikiliza ushauri huo wa mwanaye.

“Nilikuwa nikienda tu kuchora tattoo ya jicho moja mwanzoni kwa sababu nilifikiri kwamba ikiwa nitakuwa kipofu, angalau ningekuwa na jicho lingine. Ningebaki na hilo.

“Binti yangu mwenye umri wa miaka saba aliniambia kwamba sitaki ufanye hivyo, akiuliza, je, ikiwa utapofuka?
“Kwa bahati mbaya, msanii wangu alizama sana kwenye mboni ya jicho langu, kwa sasa najuta.” Anasema Anaya.