TAASISI YA TAALUMA ZA KISWAHILI

IDARA YA LUGHA YA KISWAHILI NA ISIMU

MSIMBO WA KOZI: KI 604

JINA LA KOZI: SEMANTIKI YA KISWAHILI 

PROGRAMU: M.A. KISWAHILI

MSIMAMIZI: Prof. MALANGWA, P.

AINA YA KAZI: KAZI YA SEMINA

MWASILISHAJI: ESTER AMOS MWAKISITU

NAMBA YA USAJILI:

TAREHE YA KUKUSANYA: 17/12/2020


SWALI 

 Jadili aina za maana.


                                                                    

IKISIRI

Makala hii imenuia kuelezea aina za maana zilizotajwa na kuelezewa na wataalamu mbalimbali duniani .Wataalamu kama vile Leech(1981), Lyons(1977,1996),Resani(2004), lakini tutajikita katika kuelezea aina saba za  maana kama zilivyotajwa na kufafanuliwa na Leech(1981) katika kitabu chake kinachoitwa Semantics. Leech (k.h.j) ameenda mbali zaidi kuliko wengine amezifafanua aina saba za maana kwa upana  kwa kufuata vigezo mbalimbali vya kiisimu. Aidha katika kujibu swali hili tutaligawa katika sehemu kuu tatu ambapo sehemu ya kwanza ni utangulizi hapa tutajadili dhana mbalimbali zilizojitokeza katika swali , sehemu ya pili ni kini cha swali ambapo tutabainisha aina saba za maana  kama zilivyobainishwa na Leech(1981) katika kitabu chake cha Semantics na mwisho hitimisho la swali.

1.0 UTANGULIZI

Dhana ya maana ni wazo lililoshughulikiwa kwa mitazamo tofautitofauti na wanazuoni tofauti. Mathalani Habwe na Karanja (2007) wanasema dhana ya maana ni ya kidhahania kwa sababu haina muundo thabiti, hivyo maana ni dhana tata ambayo si rahisi kueleweka kwa uwazi. Kamusi ya Oxford Advanced learners (2010) imefasili maana ya maana kuwa ni kitu au uwezo ambao ishara, neno ama sauti huwakilisha. Aidha Leech (1981) anawaonesha wanazuoni Ogden and Richard kuwa wao waliorodhesha maana za maana takribani ishirini ikiwemo inayodai maana ile ambayo mtumiaji wa ishara anapaswa kurejelewa.

Kwa ujumla tunaona kuwa maana ni dhana tata kwani wanazuoni wengi hawakubaliani hususani kwenye kueleza kuhusu  maelezo yapi yanaweza kubeba maana ya maana. Pamoja na hayo tunaweza kusema kuwa maana ni alama, ishara au dhana maneno au neno linalotumika kuelezea kuhusu kitu, mtu au jambo fulani 

2.0 Aina za Maana 

Uainishaji wa maana upo katika mitazamo tofauti tofauti ya wanaisimu. Hata hivyo kuna mitazamo kadhaa iliyochambua aina mbalimbali za maana. Zifuatazo ni aina  saba za maana kwa mujibu wa Leech (1981).



2.1.1 Maana Msingi 

Ni kiini cha mawasiliano katika lugha. Aina hii ya mawasiliano hubeba sifa za kisintaksia na kimofolojia. Leech (1981) anafananua kuwa hii ni maana ambayo haibadiliki kulingana na miktadha mbalimbali kwani  huwa na sifa bainifu na sifa ya kimuundo kwani neno huweza kupata maana baada ya kuwekewa sifa bainifu; kwa mfano,

                Mvulana   + mtu Mwanamke +mtu

+Me(jinsia) -me(jinsia)

-umri mkubwa +umri mkubwa

Iwapo nduni mojawapo  ya dhana fulani  itabadilika basi maana  nayo hubadilika,    haiwezi kubaki ileile.Tunaweza kuchunguza maana za msingi  za vitu  kwa kuangalia  jinsi nduni  zake zinavyotofautiana. Aidha maana ya msingi  inatusaidia kutofautisha  maana ya tungo  moja na ile ya tungo nyingine. Kimsingi, lugha hutegemea  maana ya msingi  ili kufanikisha  mchakato wa mawasiliano . Maana ya msingi  ndiyo msingi wa aina nyingine  zote za maana.

Lakini katika upande wa kimuundo maana huweza kupatikana baada ya viambajengo kuungana na kuunda kiambajengo kikubwa chenye maana; kwa mfano

            N+V+T+E=S

       Mtoto mdogo anatembea polepole =sentensi 

           N         v            T                 E         

      Mfano huo umedhihirisha kuwa muungano wa viambajengo  vidogo vidogo                      (N+V+T+E) hupelekea kufanyika kwa kiambajengo kikubwa zaidi  ambacho ni sentensi.

Aidha, maana msingi huweza pia kupatikana katika kamusi. Resani (2014) anaeleza kuwa maana msingi ni maana inayowakilishwa na vidahizo katika kamusi. Hivyo maana msingi lazima iwiane na maana ya kamusi na huwa haibadiliki badiliki kufuatana na muktadha.

Kwa mfano:

Mama  Ni mzazi wa kike 

Neno la heshima ambalo hutumika kumwita mwanamke 

Hii ni kwa mujibu wa kamusi Peru ya Kiswahili (2016)

Hivyo ni dhahiri kwamba maana ya msingi hupatikana kwenye kamusi na huwa haibadiliki badiliki kutokana na muktadha fulani.

2.2 Maana ya Ziada 

Hii ni maana ambayo hutegemea uelewa, uzoefu na tajriba ya mtu mmoja mmoja katika kutumia lugha, kuielewa na hata kuichangua. Pia Leech (1981), anaendelea kusema kuwa aina hii ya maana inatofautiana kulingana na tamaduni, nyakati za kihistoria na tajriba ya mtu binafsi.  Baadhi  ya  viumbe mbalimbali  hususani wanyama na wadudu , miongoni mwa  matendo na tabia zao  zimetumika kurejelea tabia za watu  kutokana na  miktadha mbalimbali.

         Kwa mfano,

Simba  Ni kiongozi mwenye nguvu kutokana na muktadha wa kisiasa.  

Kupe  mtu mnyonyaji katika muktadha wa jamii

Aidha, neno simba  limemrejelea kiongozi mwenye nguvu kutokana na muktadha wa kisiasa. Vilevile neno ‘kupe’ limebebeshwa maana  nyingine ya mtu asiyependa kufanya kazi  ingawa  anataka kufaidika kutokana  na jasho la watu wengine .  Kutokana na maelezo hayo tunaona kuwa, baadhi ya maneno yana maana zaidi ya ile ya msingi ambayo huibuka kutokana na uelewa na tajriba za watumiaji wa lugha husika kutokana na miktadha mbalimbali. 

2.1.1 Maana Hisi 

Leech (k.h.j) anaeleza kuwa maana hisi inazingatia vipengele viwili vya mawasiliano ambavyo vimejigawa kutokana na hali pamoja na mazingira ambapo neno au sentensi ilivyotumika katika lugha. Massamba (2009) anafafanua kuwa hii ni maana ambayo si ya moja kwa moja bali inakuwa  ya kuashiria kutokana na hisia ambazo mtu anakuwa anaelezea hisia binafsi au mtazamo wake juu ya mtu fulani. Pia hisi hizi  huhusiana na mtazamo wa  mwandishi  au msemaji na maana hii yaweza kuwasilishwa kwa  namna mbili  kama ifuataatavyo:

Kwa kutumia  maana ya msingi  au dokezi :"wewe mwanaume mzembe kweli"au umelegea kama mwanamke! ni wazi kuwa msemaji akitoa mojawapo ya msemo atakuwa anamdharau  msikilizaji.

Kwa njia isiyo ya moja kwa moja  kwa mfano badala ya kutoa amri : nyamazeni au fungeni midomo ! msemaji anaweza kusema kwa staha : Samahani mnaweza kupunguza sauti zenu?  Au kama yuko maktaba, na kuna vijana wanaopiga kelele  anaweza kusema jamani  hapa ni maktaba! (sauti hizo zimemuudhi na kumkera!). 

Aidha maana hisi mara nyingi hutegemea kiimbo katika usemaji. Tungo ileile inaweza kuwa na maana tofauti kulingana na kiimbo kilichotumika lakini pia mtu akiwa amechukia hutumia kiimbo cha juu kuonyesha hisia kuwa ameudhika. 

2.1.2 Maana Jamii 

Hii ni maana ambayo hutokana na lugha inayotumika katika mazingira ya jamii fulani ambapo lugha hiyo inaweza kueleweka na mtu wa ndani ya jamii hiyo. Aidha lugha hiyo inakuwa si rahisi kueleweka na watu ambao hawatoki katika jamii hiyo. Pia maana jamii hutofautiana kulingana na tofauti za kilahaja na mtindo wa mazungumzo. Aidha maana kijamii inafanana na namna mtu anavyolitumia neno katika lugha.

       Kwa mfano,

i) Tembo-kiunguja   neno  hili linamaanisha mnyama lakini kimakunduchi  humaanisha sehemu za siri za mwanamke.

ii) Kinu-kwa watu wa kaskazini humaanisha sehemu za siri za mwana mke lakini kwa watu wa pwani neno kinu ni kifaa kinachotumika kutwangia nafaka mbalimbali.

iii) Bibi-matumizi ya neno ‘bibi’ kwa Tanzania na Kenya ni tofauti. Neno bibi kwa Tanzania humaanisha mama mzaa baba au mama mzaa mama,lakini kwa nchi ya Kenya neno bibi  linatumika kwa maana ya mke. 

               

Aidha katika mifano hiyo utaona kwamba, maana ya maneno hayo hutofautiana kutoka jamii moja na nyingine sababu kubwa  ni tofauti za kilahaja.

2.1.3 Maana Akisi

Hii ni maana ambayo huibuka pale neno linapokuwa na maana msingi moja au zaidi ya moja. Maana ya neno moja huzalisha au inapelekea kuibuka kwa maana nyingine. Aidha  maana akisi huwa  ni maana inayoashiria maana fulani , mara nyingi vikundi vya vijana ndio wanaokuwa na maana akisi katika mazungumzo yao .Aidha maana akisi hutumika kama lugha za  mitaani.  

                


                       Kwa mfano

                   

Neno  shoga- ni mtoto wa kiume mwenye tabia za akina dada kama vile kushiriki umbea,  kupaka manukato kama vile poda,  kupaka rangi kwenye kucha ,kuvaa heleni na bangili.

Neno papa  ni sehemu ya uzazi wa mwanamke

Hivyo, katika mifano hiyo tunagundua kwamba, pindi maneno hayo yanapotumika katika mazungumzo huweza kuibua maana nyingine miongoni mwa wazungumzaji.

2.1.4 Maana Ambatani 

Hii ni  maana ambayo inatokana na uhusiano wa neno na neno ambapo husababishwa na tabia au mazoea ya utokeaji wa pamoja wa maneno. Aidha katika maana  ambatani  maneno   huteuana yale tu yanayoendana ili yaweze kuleta maana isiyo kinzana, pia maneno  haya sharti yaendane na misemo ya jamii.

                    Kwa mfano,

    

Bibi kizee - Ajuza ( katika maneno ‘bibi kizee’  yanapoambatana na neno ajuza huleta maana isiyokinzana  isipokuwa maneno hayo yakiambatana na neno ‘shaibu’ yataleta maana inayo kinzana  kwani kinyume cha neno ajuza ni shaibu).                  .

Mrembo - msichana (neno mrembo  huambatana na jinsia  ya kike tu. Jamii mbalimbali hususani katika Tanzania hutumia neno ‘mrembo’ kumaanisha msichana mzuri). Hivyo neno mrembo likiambatana na neno  mvulana   litaleta maana inayokinzana.

Kudamshi - Mwanamke ( neno kudamshi hutumika kumwambia mwanamke au jinsia ya kike huwa amependeza. Kwa maana hiyo, neno ‘kudamshi’ haliendani na jinsia ya kiume.

Mtanashati -mvulana (neno ‘mtanashati’ huendana na jinsia ya kiume tu na hivyo huwezi  kusema "Yule msichana ni mtanashati".

Kutokana na mifano hiyo ni dhahiri kuwa maneno katika lugha huweza kuambatana. Aidha, iwapo maneno hayataleta maana  kinzani   na  maneno mengine si rasmi kutumika katika mawasiliano yakiambatana  na baadhi ya maneno  kwani huleta maana kinzani.  Mfano huwezi kusema  ng`ombe amejifungua mtoto’ badala yake utasema ‘mama amejifungua  mtoto’ pia  huwezi kusema ‘waziri wa pesa’ badala yake utasema ‘waziri wa fedha’ kwani  neno ‘fedha’ na neno ‘pesa’ yana maana inayokaribiana  lakini   neno ‘fedha’ lina urasmi fulani hasa  unapotaja  cheo cha  ngazi fulani katika uongozi hususani  waziri wa fedha kwani huwezi kusema waziri wa pesa. Aidha neno  ‘kuoa’ katika mila na desturi za Kiafrika huambatana na kuendana na  jinsia ya kiume. Hivyo  huwezi kusema ‘Neema ameoa’  badala yake unapaswa kusema ‘Musa ameoa’ .Vivyo hivyo katika  neno ‘kuolewa’ huwezi kusema ‘Musa ameolewa’  badala yake utasema ‘Neema ameolewa’. Hii ndiyo maana halisi ya maana ambatani kwani maneno yanapoteuana na kuendana na kuwa kitu kimoja huleta maana isiyokinzana.

2.1.5 Maana Kidhima 

Ni ile ambayo kile kinachozungumzwa na msemaji au mwandishi katika kupangilia ujumbe wake kwa kuzingatia mtiririko, lengo na msisitizo katika kufikisha ujumbe. Pia maana kidhima inaweza kuelezwa kwa kutumia mkazo na kiimbo kuonyesha msisitizo katika sehemu mojawapo ya sentensi. Pia katika kiswahili msisitizo wa jambo katika sentensi mara nyingi huwa ni mwanzoni mwa tungo. Kwa mfano

           i. Wanafunzi walipewa zawadi na mwalimu 

Msisitizo upo kwenye neno wanafunzi” 

          ii. Zawadi ilitolewa na mwalimu kwenda kwa wanafunzi 

Msisitizo upo kwenye neno zawadi 

         iii. Kesho nitakuja kukutumbelea 

Hapa msisitizo upo kwenye neno “kesho”

            Maana ya kidhima  huonesha  zaidi kusudio la mwandishi  ama msemaji. Aidha pale                palipowekewa msisitizo  ndipo panapobeba maana, hivyo maana hupatikana  mahali  palipowekwa  vipamba lugha kama vile kiimbo.

                                                                                                     

3.0 Hitimisho 

Kwa ujumla, baada ya kuzitazama aina saba za maana kwa mujibu wa Leech (1981) tunaweza kusema kuwa Leech (keshatajwa) amewasaidia watumiaji wa lugha katika kutofautisha maana kwani katika kila aina ya maana ameonyesha ni kwa namna gani neno moja linaweza kuwa na maana zaidi ya moja kimuktadha. 

Marejeleo

Habwe . J na karanja P.(2004). Misingi ya sarufi ya Kiswahili. .Nairobi: Phoenix Publishers Ltd. 

Leech .G..(1981). Semantic A study of Meaning London : Penguin 

Massamba. .D.P. B.(2009).Kamusi ya Isimu na falsafa ya lugha.Dar es salaam :TUKI

Resani. M.(2014). Semantiki na Pramatiki ya Kiswahili Dar es Salaam: Karjamer Print Technology. 

TUKI. (2014). Kamusi ya Kiswahili sanifu. Nairobi: Oxford University press 

Wamitila, K.W. (2016) .Kamusi Pevu ya Kiswahili. Nairobi:Vide Muwa