Editors Choice

3/recent/post-list

Mbowe akimbilia mahakamani kunusuru nyumba yake iliyokamatwa kwa amri ya mahakama


MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe amekimbilia Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kuinusuru nyumba iliyokamatwa kwa amri ya mahakama ili kulipa Sh milioni 62.7 za mishahara ya waandishi wa habari 10 wanaomdai mtoto wake, Dudley Mbowe ambaye ni Mkurugenzi wa Gazeti la Tanzania Daima.

Mbowe leo kupitia Wakili wake John Mallya aliwasilisha shauri hilo chini ya hati ya dharura mbele ya Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mary Mrio.

Mbowe kafungua shauri dhidi ya Maregesi Paul, Fidelis Felix, Christina Mwakangale, Janeth Josiah, Exuperius Kachenje, Hellen Sisya, Kulwa Mzee, Nora Damian, Makuburi Ally, Mkurugenzi wa Gazeti la Tanzania na Kampuni ya Udalali ya JJ Auctioneers& Debt Collectors.

Wakili Mallya alidai wajibu maombi tayari wamepewa madai yao pamoja na hati ya kiapo iliyopwa na Mbowe Februari 26 mwaka huu.

“Mheshimiwa wajibu maombi tumeshawapa nakala hivi karibuni tusikilize kama wamekuja na majibu,”alidai Mallya.

Akijibu hoja hizo, mmoja wa wajibu maombi, Kulwa Mzee, alidai ni kweli wamepokea nyaraka hizo, zikiwa zimeambatanishwa na hati ya kiapo iliyoapwa na Mbowe, akiomba nyumba iachiliwe na Mahakama itoe amri wajibu maombi wamlipe gharama kutokana na utekelezaji wa amri hiyo ya Mahakama.

” Mheshimiwa tumepitia nyaraka wenzetu wametupa siku 15 tujibu, tunaihakikishia Mahakama kwamba tutajibu ndani ya muda tuliopewa,”alidai Kulwa.

Wakili Mallya aliomba kujibu hoja hiyo, alidai shauri lao wameliwasilisha chini ya hati ya dharura, maombi yao ni kuiondoa nyumba hiyo kwani tayari ilishabandikwa matangazo kwa ajili ya kupigwa mnada.

Alidai ikiendelea kuwa kama ilivyo inaweza kupigwa mnada kwa sababu suala hilo lina muda wa utekelezaji.

Akijibu Kulwa alidai ni kweli maombi yako katika hati ya dharura lakini lazima wasome vizuri ili wajibu kwa kuwasilisha hati ya kiapo kinzani kwa sababu katika maombi hayo kuna suala la kumlipa mwombaji gharama .

Aliomba kama siku 15 nyingi watajibu ndani ya siku saba, Mahakama ilikubali majibu yawasilishwe mapema, shauri hilo litasikilizwa Machi 12 mwaka huu .

Mbowe katika madai yake anadai nyumba hiyo iliyokamatwa si mali ya Dudley na kwa kuthibitisha hilo amembatanisha na hati ya nyumba hiyo yenye jina la Freeman Mbowe.

Mahakama hiyo pia imepanga kuendelea na shauri la madai ya waandishi hao kwa Mkurugenzi wa Gazeti la Tanzania Daima, Dudley Machi 12 mwaka huu.

Februari 13 mwaka huu, Mahakama ilikubali maombi ya wadai na kumteua dalali wa Mahakama kukamata nyumba kwa ajili ya kuipiga mnada.

Februari 28 mwaka huu, dalali wa Mahakama, Jesca Massawe alifanikiwa kubandika matangazo ya kukamata nyumba ya Mkurugenzi tayari kupigwa mnada kufidia deni la malimbikizo ya mishahara wafanyakazi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mary Mrio alitoa amri hiyo baada ya kupitia hoja za washinda tuzo katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi(CMA) Julai 2023.

Shauri hilo namba 28461 la mwaka 2023, wadai Maregesi Paul na wenzake tisa dhidi ya Mkurugenzi wa Gazeti la Tanzania Daima, Dudley Mbowe.

Baada ya mdaiwa kukaidi kulipa, wadai walikubaliana njia sahihi kukamata nyumba yake namba 9 iliyopo Mtaa wa Feza , Mikocheni B barabara ya Chipaka na Mahakama ilikubali.

Walalamikaji hao walipata tuzo Julai 17 mwaka 2023 mbele ya Msuluhidhi wa CMA Ilala, Bonasia Mollel.

Madai ya awali yalikuwa jumla ya Sh milioni 114 baada ya kukaa mezani kwenye majadiliano kwa pamoja kiwango hicho cha fedha kilishuka na kufikia Sh milioni 62.7.

Dudley alikubali kulipa fedha hizo kwa awamu tatu, Oktoba 30, Desemba 30 mwaka 2023 na awamu ya mwisho ilikuwa mwishoni Februari mwaka huu lakini hakulipa.

Source: bongo5

Post a Comment

0 Comments